Cover

Guide to Contents

Waathirika, utakuwa kushangazwa ambaye anapata kushoto nyuma.

Waathirika

 

written by

David Mckay

 

Translated by

Patrick Bunyali Kamoyani,

(Maragoli Kenya).

 

Smashwords Edition

Copyright 2015

 

Kutoka Kwa Zion Ben-Jonah

 

Jina langu la kweli sio Zion Ben-Jonah, halikadhalika wahusika waliotajwa kwenye kitabu hiki ni wakutungwa. Kwa kweli, hadithi yote imetungwa. Mengi tunayowajulisha ni bahatisho.

Zion Ben-Jonah amefuata mfano wa mtu mwingine aliyetajwa katika vitabu vilivyo andikwa na Tim LaHaye pamoja na Jerry Jenkins. Katika mfululizo wa vitabu hivyo, Tsion Ben-Jonah alikuwa mmoja wa wachezaji waliosaidia kueneza ukweli wakati ambapo ulimwengu ulikuwa umekumbwa na wanahabari ambao nia yao ilikuwa kutengeneza pesa badala ya kutangaza ukweli kamili.

Tuna amini kuwa hivi ndivyo mambo yalivyo sasa katika shughuli za ibada na dini zinazo enezwa kote. Waandishi wengi hawasemi ukweli, kwa maksudi (ukweli utakao tia wasiwasi na kuhangaisha sehemu kubwa ya watu wasiokubali kuupokea,) ili vitabu vilete faida kubwa.

Kama ilivyo desturi ya LaHaye kuhusu mhusika Tsion Ben-Judah, tutatia ukweli wote ndani ya hadithi hii, kulingana na yale tunayoamini yatatokea hivi karibuni, huko Amerika na mahali pote ulimwenguni.

Bila shaka baadhi ya utabiri hautatokea kama ilivyoelezwa katika kitabu hiki. Kitabu hiki hakifai kuchukuliwa kama hakikisho la unabii. Bali, madhumuni yake ni kujaribu kutumia unabii uliokwenye Bibilia na kuulinganisha na mambo yalivyo siku hizi. Itabidi msomaji aamue baina ya ukweli na utungo, kulingana na mambo yatakavyo jifunua miaka ijayo.

Kuvumbua ukweli kamili, itabidi tutambue na kukiri upungufu wa akili zetu. Kila mtu amezuiwa kadiri ya mpaka wa yale yaliyompata, pamoja na maarifa na mawazo yake mwenyewe. Hakuna mtu yeyote ambaye ana jumla ya ukweli wote isipokuwa Mwenyezi Mungu pekee. Kwa sababu hii, nina amini nimetumia ukweli ambao haujawahi kusomwa kamwe kwenginepo. Nina sadiki kwamba niliongozwa na Mungu nilipoandika kitabu hiki. Lakini mimi (ama mtu yeyote,) naweza kuamini kuwa nina haki kwa jambo ninalosema (ama analosema,) na niwe nimekosea. Kumbuka hivi, na utaweza kushika na kulinganisha kwa njia bora yale niliyoandika.

Kwa upande mwingine, nina jukumu (kama ilivyo kwa kila Mkristo,) nisiharibu au kubadilisha maana ya ukweli maksudi, kwa madhumuni ya kujifikiri mwenyewe bila kujali wengine. Ninaweza (kama wengine wanavyofanya,) kujitajirisha kwa kugeuza ukweli maksudi ili niwape watu habari wanazotaka kusikia. Kitabu hiki hakitafanya hivyo.

Badala ya uongo, utajulishwa yale unayohitaji kujua ili uwe tayari kwa yale ambayo hayana budi kutokea ulimwenguni katika miaka ijayo. Nimetunga hadithi, lakini nimejaribu pia kuambatana na maadili ya Bibilia kuhusu wakati ujao, hata kama haipendezi wala kufuata sifa bora. Mambo haya ni ya muhimu na uzito zaidi, na ni hatari sana kwa yeyote anayepoteza watu kwa madhumuni ya kutengeneza pesa.

Katika mwisho wa kila sura utapata maneno ya ukumbusho ambayo yata kusaidia kuelewa maana kamili ya sura uliyosoma. Nionavyo mimi, mashauri haya yanalinganisha maana kamili iliyokatika Bibilia na sehemu fulani ya hadithi hii.

 

-- Dave McKay.

 

 

KITABU CHA KWANZA

 

1. KUACHWA NYUMA

 

Kila mmoja alishtuka wakati taabu ilipozuka kwa ghafla. Lakini, waliogutuka zaidi ni wale ambao walidhani kuwa wanaelewa, toka mwanzo, mambo yatakayotokea.

Rayford Strait hakuwa muumini, kwa hivyo hakuwa tayari kwa lolote -- sio katika muda wa maisha yake, wala kwa maisha ya mtu mwingine. Alikuwa mtu aelezaye mambo kama yalivyo. Hali ya mambo ikibadilika (kama ilivyotokea baada ya shambulio,) itabidi atafute njia rahisi ya kurekebisha mambo muhimu na kufanya cho chote kinacho hitajika. Hivyo ndivyo alivyofanya.

Kwa upande mwingine, Bibi na kijana wake walikuwa na imani. Irene Strait alihudhuria kanisa, karibu na makao yao katika mji wa Prospect Heights, Illinois. Vernon Billings alikuwa Askofu wa kanisa la New Hope, ambalo Irene alishiriki. Mara nyingi Askofu Billings alifundisha kuhusu shida ambazo zitakumba ulimwengu mzima. Alikuwa na vitabu na sinema chungu nzima, zilizosimulia kinaganaga matumaini ya wakati ujao. Kiini cha habari hii kilijaza mawazo na moyo wake.

Irene alielewa kulingana na mafundisho kanisani, ya kwamba kutatokea kiongozi ambaye atapendwa na watu wote. Hatimaye atakuwa mtawala wa dunia nzima. Kwa amri yake waumini wote watapata mateso ambayo hayajawahi kamwe kuonekana. Irene alijua kutakuwa na maafa na mashaka tele kila mahali na hakuna yeyote atakaye weza kuepuka.

Irene alizungumza kuhusu mambo haya na kijana wake Raymie, mwenye umri wa miaka kumi na tatu. Alijaribu pia kueleza binti yake Chloe, lakini Chloe alikuwa -- kama Baba yake -- mwenye roho ngumu. Hakujali chochote ambacho hawezi kuona au kuguza.

Raymie alikuwa na moyo wa kupenda ushirika, vitabu na sinema zinazohusu unabii, ingawa mara kwa mara alijaa hofu. Lakini alituliza roho yake kwa sababu hakuwa na shaka kuwa atachukuliwa upesi hadi mbinguni kabla ya mwanzo wa mashaka . ghafula na bila maumivu . kwa sababu alisema ombi fupi lakualika Yesu Kristo ndani mwa roho yake. Raymie aliombea Baba na Dada yake kwa uaminifu akitarajia kuwa watatubu dhambi zao na kusema ombi hilo kabla ya kuchelewa. Alitaka wote pamoja waingie mbinguni.

Irene aliomba sawa na Raymie, kwa moyo wa bidii na nguvu zaidi. Hakutaka hata mmoja wa jamii yake awachwe nyuma. Hata hivyo, alikuwa na hakika kuwa Raymie pamoja naye hawatawachwa. Alikuwa na mkusanyiko wa vitabu, kanda, sinema na mafunzo mengi kutoka kwa waledi wa dini, ambayo yalitilia mkazo kuwa waamini wataepuka.

Alikuwa ameambiwa kuwa mateso yote yameachiwa watu wengine, wale ambao wanafaa kuteswa . kama Wayahudi. Hata hivyo, wamepata mazoezi zaidi kuliko sisi wengine kuhusu taabu na mateso!

Rayford Strait alikuwa rubani wa eropleni ya alfajiri iliyokuwa ikisafiri kutoka London hadi Chicago, Jumanne moja katika mwezi wa Mei, wakati shambulio lilipotekelezwa. Alikuwa amebakisha njia nusu wakati alipopata habari kutoka kwa kituo cha Wakuu wa Uelekezaji wa Ndege kutoka Chicago, kuwa kuna hatari ya ndege za vita na mizinga inayoelekezwa njia yake bila idhini (ilikuwa saa tisa na nusu ya usiku, saa ya Chicago.)

Mara ya kwanza, Rayford aliambiwa apitie mkondo mwingine lakini, wakati huo huo chombo cha mapokezi kilitangaza taarifa nyingine iliyoenezwa kote kote. Afisa aongozaye eropleni alisikika kuwa na wasiwasi alipoagiza eropleni zote ambazo zinapita sehemu ya milima ya barafu inayoelekea Amerika zigeuke mara moja.

Rayford alipouliza sababu, alipata onyo kali kwa sauti kuu, “Eropleni zote zinazoelekea Amerika Kaskazini lazima zigeuke mara moja. Hili ni jambo la lazima na hatari. Tumeonywa na Makao ya Wakuu wa Ulinzi wakutoka Washington, D.C. Nitarudia: Geuka! Usijaribu kutua kwenye kiwanja chochote Amerika Kaskazini!”

Ndege zisizo tambulika zilikuja kama bumba la nyuki, kutoka Kaskazini kupitia sehemu ya milima ya barafu na kuvuka mpaka wa Canada. Zilifuatiwa na mizinga na kombora . mia(kama sio elfu,) zilizokuwa zinapeperuka juu ya ndege za vita ambazo zinaelekea Amerika. Kila mzinga na kombora ulikuwa na azimio la kuangamiza mji fulani, ama kituo fulani cha maarifa ya kudanganya adui katika vita. Baadhi ya makombora yalizuiwa (moja kati ya kumi,) lakini kwa jumla ujuzi wa Wakuu wa Ulinzi wa Amerika ulithibitishwa kuwa dhaifu, bila nguvu pasipo dalili yakutosha kuhusu hatari.

Kila mzinga ulikuwa umefunikwa na aina ya mfuko mkubwa uliojaa namna ya hewa nyepesi, iliyokuwa na manufaa ya kubumbuaza vifaa vya kufuatia kwa kuangalia alama, inayotumiwa na waongozaji wa ndege za vita. Tisa kati ya kumi ya silaha za ulinzi wa Amerika zilikosa kabisa kutekeleza azimio lake. Katika harakati ya kufuatia mizinga, ndege nyingi za adui ziliingia Amerika kwa kujificha na kutumia uerevu bila kutambuliwa. Ndege za adui za vita zilipiga chochote kilichowachwa bila kuharibiwa na shambulio la mizinga.

Jumla ya watu wa Amerika waliamini uongo kwamba Amerika ina uwezo wa kujilinda, lakini mataifa mengi hayakuamini hivi. Hata hivyo, mataifa hayo yalielewa kuwa hakuna njia yoyote ya kuzuia Amerika iwapo iaamua kulipiza kisasi. Kwa kufanya hivyo, Amerika itamaliza kabisa maadui wake wakati ambapo Amerika yenyewe inaangamia. Vitisho kutoka kwa nchi adui kwamba “mapatano ya hakika ya maangamizi,” na sio silaha au mizinga ya ulinzi wa nchi fulani, ndio sababu pekee ya amani iliyodumu kwa wakati mrefu.

Lakini mambo yalikuwa yamebadilika sasa. Kutokana na shambulio hili, inaelekea kuwa Amerika ilijipata bila roho, au yenye uoga, au yenye akili timamu na busara, na haikutaka kulipiza kisasi kwa adui yake. Kwa bahati nzuri, mtu ambaye alikuwa na mamlaka ya kuamuru kisasi alikata shauri kuwa itakuwa ovyo kufanya hivyo. Alionelea kuwa hakuna njia ya kurudisha uhai wa watu zaidi ya milioni ambao tayari wamefariki na pia, hakuna haja ya kuongeza hangaiko la walimwengu.

Karibu saa kumi ya usiku wa kuelekea Jumanne, kabla ya kombora la kwanza kuanguka, ishara ya onyo la vita ilitangazwa na kusikika kote. Hadi sasa, watu walikuwa wameridhika kuhusu ishara kama hizo tangu mwisho wa Vita baridi, na hasa tangu 1990, ambapo hali ya kuwa watu hawawezi kuwa na mali yao pekee ila mali yote ni ya watu wote wakiwa wanashirikiana, ilipoondolewa kabisa. Mnamo mwaka wa 1992, Amerika iliwacha jitihada zake za kujenga majengo ya usalama kutokana na vita vya ghafula. Tangu wakati huo, ishara za onyo la vita zilidhaniwa kuwa za kazi bure, hasa zilipotangazwa katikati ya usiku.

Jumla ya watu kote nchini waliendelea kulala bila kujali. Hatimaye, watu wengi hawakujua kifo chao kimefika.

Lakini Irene hakuwa kama watu wengine. Kelele za onyo zilimfanya azinduke kwa mshtuko wa hofu. Aliamsha watoto kwa haraka, haidhuru kunung’unika kwa Chloe na Raymie. Walienda mbio kujificha kwenye gorofa ya chini ya nyumba, katika chumba walichotumia kama bohari na mahali pa kufanyia kazi.

Bila kufikiria, Raymie alipokonya simu iliyokuwa kwenye meza akidhani kuwa ni chombo cha kisasa cha mchezo. Walipofika boharini, Irene alifungulia redio iliyokuwa imewachwa pale, ili atafute taarifa kutoka kwa Wakuu wa Ulinzi. Wakati huo huo, walisikia shindo kubwa na tetemeko la ardhi lililosababishwa na kombora la kwanza kupasuka katika mtaa wa Chicago, zaidi ya maili ishirini kuelekea Kusini, kutoka Prospect Heights. Nuru isio ya kawaida iliingia kupitia kwa dirisha mbili ndogo zilizo kuwa juu, zikipimana sawa na njia ya mji. Dirisha zenyewe zilitetemeka. Baada ya dakika chache walisikia shindo kadha ndogo, moja kutoka kiwanja cha ndege cha O’Hare ambacho kilikuwa umbali wa maili sita.

Jamii ya Strait haikuwa na habari kwa wakati huo, lakini shindo moja walilo lisikia lilisababishwa na kombora kubwa lililoenda kombo na kukosea shabaha lake. Kombora hilo lilianguka upande wa Magharibi katikati ya De Kalb na Dixon, umbali wa maili themanini kutoka makao yao. Ilikuwa imeazimiwa shabaha lililo Kaskazini kutoka Prospect Heights. Kama lingaliteremka mahali lilipopangiwa, bila shaka makao yao yange fiatuliwa. Laiti wangaliponea chupuchupu kutokana na shindo hilo, wangalikuwa wamechomeka vibaya kutokana na miale. Hawangekuwa na budi kufariki baada ya siku chache tu.

Walipokuwa wamejificha mahali penye usalama kiasi, Amerika yote, mamilioni kadha ya watu walikuwa wanateketea, huku idadi sawa ikiwa na majeraha ambayo baada ya siku chache yatageuka kuwa magonjwa ya kuambukizana yasioweza kuponywa.

“Ni nini kinachotendeka?” Irene alijiuliza kwa mshangao na wasiwasi, huku ameshika kichwa chake.

“Inaweza kuwa tunashambuliwa?” Raymie aliuliza. “Haiwezi kuwa mwisho wa dunia,” aliongeza kama mtu ambaye anajaribu kujituliza. “Haiwezekani; tungeondoka kabla ya mashaka kuanza. Sio mwisho, waonaje Mama?”

“Sijui Raymie, wacha nifikiri.” Irene alijibu kwa sauti iliyojaa uoga.

“Nyamazeni,” Chloe aliinjilia, masikio yake yalikuwa kwenye matangazo ya redio. “Wanasema nchi ya Urusi imeanzisha vita. Makombora yametoka Urusi lakini wamesema Amerika inauwezo wa kujilinda.”

“Kweli, niambie ni wangapi wameuawa na shindo tulilolisikia.” Raymie aliendelea, “Nina hakika Chicago imeangamia, na sasa sisi pia tutakufa. Tutakufa, na Mungu anafanya nini? Hafanyi cho chote, ama? Kwa nini Mama? Kwa nini?” Raymie alianza kulia na kutetemeka kama mtu aliyeingiwa na pepo mbaya.

“Poa Raymie! Wacha tuombe,” Irene alisema.

“Ehee, kweli! Itabidi tuombe,” Raymie alijiongelesha kwa sauti iliyojaa maudhiko. “Tayari tumeomba, ili tuokolewe kutokana na taabu yote hii. Ninafaa kuwa mbinguni sasa hivi.” Raymie aligeuka kuangalia Irene. “Ni nini kimetuzuia Mama? Kwa nini hatujaenda? Sisi ni wazuri kama wale wengine. Mbona hao wamechukuliwa na sisi tukawachwa?”

Irene alimjibu, “

“Basi kuna haja gani kama sisi pia tutapata Hatujui kama wamechukuliwa, labda mbingu haijafunguka bado.”mashaka haya?” aliuliza Raymie.

Chloe alikatiza tena, “Nyinyi wawili mtanyamaza? Tuna bahati kuwa hai lakini itabidi tujitayarishe upesi.”

Irene alitoa shauri, “Tafuta mshumaa kwenye meza ya kufanyia kazi.” Kwa bahati, Chloe alipata mishumaa kadha na viberiti. Alipowasha mmoja, aligeuka na kusema, “Raymie, jaza chombo chochote utakachopata kwa maji. Fanya haraka!” Chloe alikuwa mfidhuli, na kama Baba yake, alitafuta njia rahisi ya kurekebisha matatizo yao. “Na wewe Mama, kaa karibu na redio ili utueleze mambo yanavyoendelea.” Kwa sauti ndogo alijiambia, “Lazima nitafute njia ya kuziba zile dirisha mbili. Hewa ya inje imejaa madhara na sumu.”

Chloe alitumia nyundo na misumari, pamoja na mbao alizopata kuziba dirisha. Alitumia makaa katikati ya mbao, ili yaweze kuchukua hewa yenye sumu. Alipomaliza kazi hii, alikuwa amejipaka makaa kila mahali. Lakini hakuwa na wakati wakujisafisha.

“Raymie, maji yako wapi?” Chloe aliuliza.

“Nimejaza viombo viwili vya kufulia nguo. Hakuna kitu kingine ninacho weza kutumia.”

“Umeangalia mikebe ya kuweka rangi? Mwaga rangi, lazima tuchote maji.”

Raymie alirudi kazini akinug’unika kuwa hatakunywa maji machafu kutoka kwa mikebe ya rangi, alisema “Hii rangi ni hatari kwangu kuliko kukosa maji. Je, tutakula nini?”

Chloe alijibu, “Hatuli chochote kwa sasa. Ni hatari kurudi gorofa ya juu, labda baada ya siku chache tutaweza kwenda jikoni kutafuta chakula.”

Raymie karibu alie, “Kwa siku chache?”

“Ndio, kwa siku chache. Hatutakufa.” Chloe alijibu.

Fikira za Irene zilikuwa mbali, hakuwa akisikiliza. Alikuwa anaomba kwa bidii ili Mungu awalinde na pia kuwa atapata njia ya kuzungumuza na Askofu Billings. Wakati huo huo ndipo alipoona simu(ambayo Raymie alichukua ghafula). Alishukuru Mungu.

“Askofu Billings! ni wewe?. Ni mimi Irene Strait. Ni nini kinachoendelea? Tafadhali niambie!”

“Amini Mungu Dada Strait,” Askofu alimrudishia kwa upole. “Kila kitu kitakua sawa. Anajua anavyofanya.”

“Lakini nchi yetu . ina shambuliwa! Hivi sivyo tulivyo tarajia mambo kutokea. Kwanini hatujachukuliwa? Huu ndio mwisho wa dunia ama sivyo?” aliuliza Irene.

“Niamini Dada. Kila kitu kiko sawa mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Jana usiku, nilizungumuza kwa simu na kikundi cha jeshi la askari Wakristo wa kutoka Montana. Walisema Yesu Kristo mwenyewe alijionyesha huko kwao. Ndio, Kweli kabisa! Tulikosea, lakini sasa Dada lazima tuongozwe na Roho Mtakatifu. Mwenyezi Mungu anawaita watu wake kutoka sehemu zote za Amerika waelekee Montana. Jana usiku, mimi mwenyewe nilikataa kuamini, lakini sasa nina fikira tofauti.”

Askofu alingojea jibu, lakini Irene alikaa kimya. “Ungali nami Dada Strait?”

“Ndio, sawa, nasikia,” Irene alisita kabla ya kujibu.

Askofu Billings aliendelea, “Tutaepuka mashaka haya Dada. Lakini, lazima uwe muaminifu. Elaine na mimi tunaomba sasa kuhusu jambo hili na tungetaka ufanye hivyo pia. Mungu ametuweka hai na sababu. Anakuja kutuchukua, Irene! Lazima uamini. Tulikuwa tumekosea kidogo tu, kwa yale tuliyodhani.”

“Kukosea kidogo tu?” Chloe aliuliza kwa maudhiko wakati Mama yake aliposimulia yale ambayo Askofu amemwambia. Kushambuliwa kwa Amerika ni jambo kubwa sana! ”

“Chloe, labda hii ni nafasi yako ya mwisho ya kutubu dhambi zako ili twende pamoja.” Irene alijawa na huruma alipotazama mtoto wake. Macho yake yalikuwa yamejaa machozi alipozungumuza.

“Siendi popote bila hakika kuwa hewa ya nje ni safi. Labda, serikali itatuma jeshi lije kutuokoa.” Wakati huo huo simu ililia, Irene alichukua na kusikikia sauti ya Bwanake.

“Irene, naomba msamaha kwa kukusumbua saa hii lakini, niko na wasiwasi.”

“Loo Rayford! Nina hofu. Tumesikia kwa redio kuwa Chicago na sehemu zingine zimeangamia. Sisi hatuna neno.hatujajeruhiwa, tulijificha.Wewe uko vipi?. Utarudi nyumbani lini?.London? Kwa nini London?.Utarudi leo, sio?.Mambo si mazuri hata kidogo!.Ndio, nimeelewa.Nitajaribu.Sema tena, sauti yako inapotea. ati. Siamini, simu imekatika.”

Irene alipinduka na kusema, “Baba yenu haji nyumbani, ameambiwa arudi London. Angalao yungali mwema, na anajua hali yetu pia.”

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika:

 

Kuna pingamizi katika swali kuhusu kama Wakristo watachukuliwa na kupelekwa mbinguni kabla au baada ya wakati wa Dhiki Kuu. Pande zote mbili zinakubaliana kwamba: (1.) ‘Parapanda’ saba zilizotajwa katika Ufunuo Wa Yohana, sura 8-10, zinatueleza kuhusu wakati wa “Dhiki Kuu”; na (2.) 1 Wakorintho 15:51-52 inatueleza kuhusu jambo linaloitwa Kufunguka Kwa Mbingu -- wakati ambapo Wakristo watabadilika na kunyakuliwa pamoja katika mawingu, ili wamlaki Bwana Yesu hewani atakaposhuka kutoka mbinguni. Itabidi tusome vifungu hivi ili tupate jibu sahihi kuhusu jambo litakalo tangulia.

1 Wakorintho 15:52 inasema kuwa, mbingu itafunguka “wakati wa parapanda ya mwisho.” Kwa hivyo, itakuwa lini? Kabla au baada ya parapanda saba za wakati wa Dhiki? Rahisi, sio?

Yesu mwenyewe alisema kuwa, “Mara baada ya dhiki ya siku zile, Mungu atawatuma malaika wake waje kuwakusanya wateule wake, ili wamlaki anaporudi duniani. (Mathayo Mtakatifu 24:29-31.)

Mafunzo kuwa Wakristo hawahitaji kuvumilia wakati wa Dhiki yanapendeza watu wengi, kwa sababu hivyo ndivyo watu wanavyotaka sana kusikia. Lakini, haidhibitishwi katika injili. Hili ni tumaini la uongo.

Swali kamili katika majadiliano haya ni hili: “Iko hatari kiasi gani ukilinganisha na kufafanua maana ya mashauri mawili tuliyotaja hapo mwanzo?” Mtu yeyote ambaye anajitayarisha kwa vyovyote hatakuwa na shida ikitokea kuwa amekosea. Lakini, mtu ambaye anatafuta njia rahisi ya kuponyoka atakata tamaa na kufa moyo bahatisho lake lisipodhibitishwa kuwa la kweli.

 

 

2.UBASHIRI

 

Vituo vya maafisa wakuongoza ndege vya Uingereza; Gatwick na Heathrow, vilijaa ghasia nyingi walipojaribu kuelekeza eropleini upande mwingine au zirudi . kwa kweli, hali hii ilienea Ulaya kote. Rayford Strait alipata habari kwa njia ya chombo cha kupokelea ndani ya mahali pa kukaa rubani wa ndege kubwa aina ya 747, kuhusu eropleni moja ndogo ambayo ilikuwa imepotea pwani ya Scotland. Ndege hiyo iliishiwa na mafuta ilipojaribu kurudi Uingereza. Hakuna njia ya kusema kitakacho tokea ndege zingine zikiishiwa na mafuta ya kuziwezesha kurudi Ulaya. Rayford aliwaza kuwa baadhi ya ndege hizo zitatua mahali popote Amerika Kaskazini, bila idhini au usaidizi wa waongozaji sahihi. Hatimaye, kutatokea misiba zaidi.

Rayford alipotua na kuiingia ndani ya kituo cha ndege cha Heathrow, alianza kupata picha bora kuhusu ukubwa na uzito wa taabu. Katika harakati za fujo kutokana na ndege zinazorudi ghafula, alisikia kelele za watu wakizungumza kuhusu shambulio la Amerika lililoanzishwa na Urusi. Ilikuwa inaelekea saa nane ya mchana huku London, na saa mbili ya asubuhi huko Chicago. Itachukua muda wa saa chache kabla picha za Runinga ziwe tayari kuenezwa kote. Jua halikuwa limechomoza Pwani Magharibi ya Amerika, hata hivyo vyombo vya habari za dunia vilikatiza vipindi vya Runinga vya kawaida, ili habari za kwanza kuhusu vita zienezwe.

Taarifa ndogo ya kwanza ilisema kuwa, hesabu za mapema zilionyesha kuwa watu Milioni tano wamefariki. Lakini taarifa iliyofuata baadaye ilidhibitisha kuwa hasara ilikuwa mara kadha zaidi ya hesabu ya kwanza. Bila shaka, itaendelea kuongezeka zaidi ya mara mbili, kwa muda wa majuma yajayo.

Maafa na hasara kwa miji mikubwa, barabara kuu, na vituo vya ndege ilimaanisha kuwa, kujenga upya hakutawezekana kamwe . hata kama vita havingetokea. Nchi nzima ya Amerika ilikuwa bila serikali, utawala, njia ya kupelekeana habari, wala kiini cha njia za kusafiri. Majimbo yaliyokatika eneo kuu la biashara, katika miji mia moja, yaliangamia. Hasara ya watu waliofariki ingekuwa kubwa zaidi, kama shambulio halingeanza katikati ya usiku.

Hospitali nyingi za miji mikubwa ziliteketea pamoja na wagonjwa na wafanyi kazi waliokuwa ndani. Ilibidi madaktari, wauguzi na wasaidizi waliokuwa na uwezo waendelee na kazi bila usimamizi. Bila kutazamiwa, Amerika ilijipata imerejea kwa hali ya mambo ya kale; ambapo kila mtu alijitegemea mwenyewe ili aendelee kuishi.

Huduma za usaidizi zilitayarishwa mahali pote ambapo Lugha ya Kiingereza inapotumika. Mipango ilifanywa ya kusafirisha kwa ndege vifaa mbali mbali, nguo za kujikinga, madaktari na wasaidizi, kwa madhumuni ya kupunguza maumivu na taabu za Amerika, Mexico na Canada. Watu waliojeruhiwa walihitaji matibabu kwa haraka, ingawa wengi wa watu zaidi ya Laki kadha, hawataokolewa na usaidizi wowote. Wale ambao wamefariki wata wachwa pale pale.

Nchi zisizozungumza Kiingereza zilikuwa na mawazo ya kuchanganyika. Bila shaka, jumla ya walimwengu walikuwa wameshtuka. Rais wa Amerika Gerald Fitzhugh, alikuwa na adui wengi kwa sababu kila wakati majeshi yake yaliingilia shughuli za dunia. Mara nyingi aliamurisha vita vya “kutoa nchi fulani utumwani,” yamkini ikiwa ya kumaliza “vitisho vya ukatili.” Washauri wake waliapa kwamba Fitzhugh anaamini kabisa kuwa anafanya hiari ya Mwenyezi Mungu. Walisema kwamba amejawa na uchungu wa kibinafsi kwa sababu ya watu waliouliwa na kujeruhiwa lakini, alionelea kuwa taabu yote iliyotukia haina budi kuleta aina ya amani takatifu duniani.

Xu Dangchao, wakutoka nchi ya Tibet, alichaguliwa mwaka uliopita kuwa Katibu Mkuu wa mambo ya Ushirika wa Umoja wa Mataifa, miaka miwili tangu Tibet ilipokaribishwa katika mwili wa mataifa, na miaka mitatu baada ya jimbo kuu la Umoja wa Mataifa kuhamishwa hadi mji mkuu wa Geneva. Ingawa mashauri ya Dangchao yalipendeza nchi za Urusi na jumla ya Mataifa Maskini, mikono yake ilikuwa imefungwa kutokana na amri ya Amerika ambayo ilipinga mashauri yake mbele ya Baraza la Ulinzi wa Umoja wa Mataifa. Nia ya Dangchao ilikuwa kufuta madeni ya Nchi Maskini na kuondoa masharti ya ushuru wa forodhani, uliodhuru bidhaa zinazoletwa au kupelekwa nchi zingine kwa madhumuni ya kuuzwa. Ushuru ulifaa nchi zenye mali hivi ukiendelea kudhoofisha na kupunguza manufaa ya Nchi Maskini. Amerika ilitoa sababu dhaifu ya kwamba, wanapinga mashauri hayo kwa sababu Dangchao anajaribu kufanya mabadiliko “kupita kiasi, kwa upesi kabla ya wakati uliopasa.”

Nchi za Urusi na China zilikubaliana na Dangchao. Hata hivyo, walikuwa wakaidi kama Amerika kuhusu pingamizi ya kuingilia kwa majeshi ya Amerika kwa mambo ya nchi zingine ambazo iliamini kuwa zinavunja na kutotii haki za binadamu. Lakini, Amerika ilikuwa na njia ya kuzunguka pingamizi kutoka kwa Urusi na China. Ilitumia nguvu za Jeshi na mali yake ili iweze kuumba jeshi moja kubwa la muungano wa mataifa marafiki, ambalo lilitumiwa kuanzisha vita bila usaidizi.

Jambo la huzuni ni kuwa, Amerika ilipoendelea kujifanya Mungu na aheri ya nchi ambazo ilidhani kuwa “zenye uovu,” ilirahisisha dhibitisho la kuingilia, hata kama maovu yanayotendwa na nchi iliyokuwa ikiisaidia, yamezidi maovu ya nchi iliyotaka kuimaliza.

Bila shaka watu wa Amerika walipendezwa sana na fikira hii. Jambo la muhimu zaidi kwao lilikuwa kwamba, Rais Fitzhugh hadi sasa hakushindwa kwa mapigano yoyote aliyoanzisha. Ilikuwa sawa akiendelea kujihadhari na kuanzisha fitina au kuasi serikali ndogo na dhaifu, kwa sababu alikuwa na hakika kuwa atashinda. Bila kupoteza wakati jeshi moja lilirudi nyumbani kutoka ugomvi mmoja ili jeshi lingine litumwe kuamua uzushi mahali pengine. Watu wa Amerika walijivuna kwa sababu ya nchi yao kuliko wakati wowote mwingine. Walijidhani kuwa mashabiki wakuu wa dunia. Kiongozi Fitzhugh, aliyedai kuwa ameokoka (kuzaliwa mara ya pili,) hakukosa nafasi ya kukumbusha wapiga kura wake kuwa Mwenyezi Mungu yuko upande wake.

Lakini sasa, Amerika ilivyokuwa na uchungu wa maafa; nchi za Urusi na China, pamoja na shujaa wao Dangchao, hawakuogopa chochote kutoka kwa Fitzhugh au nchi za Uingereza na Ufaransa--ambazo zilikuwa zenye nguvu na umashuhuri kwenye Baraza la Ulinzi wa Umoja wa Mataifa. (Ufaransa ilikuwa imeanza kujitenga mbali na Amerika.) Inaelekea kuwa nchi tatu zisizo kubaliana na Dangchao zilipunguza nguvu kwa muda wa masaa machache tu!

 

* * *

 

Rayford aliambiwa aende kupumzika huku akiendelea kufuatilia mambo yanavyotokea kwenye kituo cha ndege, ili apatikane kwa rahisi ndege yake ikihitajiwa kupeleka usaidizi. Ndege zote za kuenda Amerika Kaskazini zilifutwa. Serikali ya Uingereza ilitangaza hali ya wasiwasi kutokana na uzushi. Hii ilimaanisha ya kwamba, jeshi la Uingereza limeamurishwa kuchukua mamlaka juu ya vituo vya ndege pamoja na rubani wote watakaopatikana. Nchi zingine za, Australia, New Zealand, na Afrika Kusini, ziliiga mfano huo ili ziweze kusaidia. Vifaa mbalimbali vilihitajika Amerika Kaskazini kwa kasi, nao wakimbizi walikuwa wanangojea kusafirishwa kutoka huko. Ilibidi watu wote wa Amerika wahamishwe . wale ambao hawakufariki.

Hakukuwa na habari zozote kuhusu uharibifu wa nchi ya Canada, isipokuwa sehemu chache kavu zisizokuwa na wenyeji. Zilipigwa na mizinga na kombora zilizokosea na kwenda kombo. Ilionekana kuwa Urusi ilianza vita na Amerika peke yake.

Canada, Uingereza, Australia, pamoja na nchi zingine zilizokuwa marafiki na Amerika ziliepuka bila taabu yoyote. Kwa sababu hii, viwanja vya ndege vya Toronto, Ottawa, Montreal, Quebec na Vancouver(Canada,) vilitayarishwa ili ndege ziweze kutua na kuondoka saa yoyote bila shida. Rayford na rubani wenzake walikuwa na jukumu kubwa katika kazi ya wokovu.

Rayford alikosa usingizi ingawa alikuwa amechoshwa na safari. Alienda kwa chumba cha kupumzika katika Hoteli ya Hilton iliyokaribu na kituo cha ndege. Alilala juu ya kitanda bila kuvua nguo zake na kutazama upande wa chini ya dari, akiwa katika hali ya kushtuka ambayo ilikuwa imekumba dunia nzima kwa wakati huo. Aliwaza kuhusu Irene, Chloe na Raymie, akikumbuka kidogo tu jamii yake nyingine iliyokuwa Amerika, ambao labda walikuwa wameteketea.

Mazungumzo kwa kutumia simu(za kawaida) ilikuwa ngumu kwa sababu mtandao wa simu kote Amerika uliharibika. Hata simu za kisasa za rununu zilizo na nguvu zaidi zilipata shida. Kwa bahati nzuri, Rayford alikuwa amenunulia Irene simu ya aina nyingine, ambayo ilimuezesha kuzungumza kutoka hewani wakati anapopitia ufuo mwembamba wa njia ya kutoka London kuelekea Chicago. Sasa hii itakuwa njia pekee ya kufikia Irene. Huenda atajaribu tena atakaporudi Canada.

Rayford alijaa picha za Mamilioni ya watu walioangamia ambazo zilitia hofu akilini. Aligeuza mawazo yake tena kufikiria jamii yake ambayo ilikuwa imejificha boharini. Angalau wangali hai, baada ya masaa ishirini na manne atapata nafasi ya kuzungumza nao tena. Bila kusema chochote alishukuru Mungu, akitarajia kuwa atapata njia ya kuwaokoa baada ya siku chache.

Giza la jioni lilipoanza kuingia, Rayford aliamuka kutoka usingizi wa kugeukageuka; baada ya kuoga na kujitayarisha aliwacha habari katika meza ya kukaribisha wageni kwenye hoteli, ya kuwa anaelekea kituo cha ndege kwa kutumia motokaa ya kukodi. Alionelea kuwa atapata habari kamili kutoka kwa wafanyi kazi wenzake kuliko kutoka mahali popote pengine.

Alipowasili alielezwa kuwa ndege yake inahitajika kusafiri hadi Toronto, kesho yake saa kumi na mbili ya alfajiri. Atasafirisha abiria wachache (madaktari na wauguzi,) hema, vyakula, riziki, madawa na nguo za kujikinga kutokana na hewa yenye madhara na sumu. Tayari vifaa hivi vilikuwa vinatiwa ndani ya ndege yake katika banda la ndege lililokuwa Kusini mwa uwanja wa Heathrow.

Rayford alifahamishwa kwamba, masaa machache baada kombora na mizinga ya mwisho kuanguka, habari zilienea Amerika kuwa Canada haikupigwa. Hatimaye, dhoruba kuu ya watu waliondoka pamoja na kuelekea Canada. Barabara na njia kuu zakuelekea Kaskazini zilijaa vikundi vya watu waliokuwa wakijaribu kuepuka shida. Kwa upande mwingine, serikali ya Canada ilikuwa inajaribu kuanzisha vituo vya usaidizi wa wakimbizi.

Kwa bahati nzuri, ilikuwa karibu na wakati wa hari na Jua kali. Kwa sababu hii, Maelfu ya wakimbizi walitengenezewa makao ya nje, karibu na mpaka wa Canada na Amerika. Hii iliwacha huru makanisa na majengo ya shule, ambayo yaligeuzwa na kutumiwa kama hospitali. Namna ya eropleni ndogo zinazoweza kupaa na kushuka moja kwa moja kiwima, pamoja na vikosi vya magari ya kuchukulia wagonjwa na zana za madaktari vitani, zilianza kazi ya wokovu na kuvukisha waliojeruhiwa kutoka mitaa iliyokaribu. Vancouver ilichukua wagonjwa kutoka Seattle, Portland na Spokane; Toronto ilichukua waliookolewa kutoka Detroit, Cleveland na Buffalo; na miji ya Ottawa, Montreal na Quebec ilijitayarisha kupokea wakimbizi kutoka sehemu za Boston, Rochester, Philadelphia na mji mkuu wa New York.

Wakati huo huo, wakazi wa Canada walishikwa na uoga mkuu. Waliogopa kuwa uzushi unawakaribia. Vituo vyote vya ndege vilikuwa vimejaa abiria waliokuwa wanangoja viti vya bahati kwenye ndege zinazoondoka. Hesabu mia ya eropleini ambazo zingetua Amerika kwa sasa ziligeuka kwenda Canada, ambapo kila moja ilikuwa na dhibitisho la kujaza viti vyote bila kujali gharama au mahali abiria anapokusudia kufika. Maafisa wa kutoka Canada, ambao ni mazoea yao kukaa chonjo na kuwa tayari kutangulia kutoa huduma ya usaidizi kutokana na jambo la ghafula; walikuwa kama wenye wazimu walipojaribu kudhihirisha kanuni zitakazo tumiwa kuchagua watu ambao watasafirishwa kwanza.

Runinga iliyokuwa katika chumba cha wageni waheshimiwa ilitangaza hesabu ya miji mikuu na viwanja vya ndege vilivyoangamia. Ndege ndogo ziliweza kutua katika viwanja vidogo lakini, haikufaa kurekebisha kwa haraka matatizo ya miji mikuu -- kama Chicago -- ambayo ilipata hasara zaidi. Milwaukee na St. Paul/Minniapolis ilikuwa miji iliyokaribia Canada, kuliko Chicago. Miji hii pamoja ilitoa riziki na usaidizi wa kusafirisha watu hadi vituo vya wakimbizi vilivyoanzishwa na nchi jirani.

Rais Gerald Fitzhugh pamoja na jamii yake walidhaniwa kuwa wamenaswa chini ya makao makuu ya Washington D.C. Walikimbizwa kujificha kupitia mlango wa sakafuni wakuinuliwa juu na sio kwa upande, wakati kelele za kwanza za onyo zilipotangazwa. Kama kombora ilipasuka karibu na makao makuu, basi kuponyoka hakutakuwa rahisi.

Watu walioepuka walielezwa kwa njia ya redio watafute kimbilio au mahali pa kujificha hadi watakapo amurishwa vingine. Jitihada zilikuwa zinafanywa za kuhamisha wakimbizi wote. Lakini kwanza, itabidi wenye mamlaka wachague mahali watakapo wapeleka. Utabiri wa hali ya hewa ulionyesha kuwa upepo wa baridi unaelekea Kusini Mashariki kwa kupitia sehemu ya Magharibi kati kati ya Amerika. Mawingu yaliyobeba hewa ya madhara na sumu yalionekana kuwa yanaelekea upande huo.

Kuangamizwa kwa San Diego, Anaheim, Los Angeles, Fresno, Sacramento, Oakland, San Francisco, Portland, Eugene, Tacoma, Seattle na Spokane, kulionyesha kuwa hasara imekusanyika sehemu za Pwani Magharibi. Sehemu zilizo kati ya Boston na Washington zilikuwa zimepigwa zaidi ya zingine zote.

Rayford alielewa kutokana na picha za kwanza za wakimbizi zilizoenezwa kwa njia ya Runinga kuwa, nafasi ya kupatana tena na jamii yake haikuwa nzuri. Pande mbili za njia kuu zilikuwa zinatumiwa na magari yanayoelekea Kaskazini, ambayo yalikuwa yamekoma njiani na kutambaa polepole. Ilibidi magari yatumie njia zingine ili yaepuke barabara kuu na njia ambazo zilikuwa zimechimbuliwa na mizinga. Magari yaliyokuwa yakitumiwa katika shughuli za uokovu ndio yaliyokuwa yakielekea Kusini, peke yake.

Barabara kuu zenyewe zilikuwa zimezuiwa na magari yaliyoishiwa na mafuta, ambayo yalisukumwa na kuachwa kando. Ilibidi dereva na abiria wa magari hayo wathubutu kuendelea kwa miguu. Kila siku iliyopita ilimaanisha kuwa watembezi wako hatarini kutokana na hewa ya kudhuru. Wakuu wa Ulinzi walitoa onyo kali ya kuwa, raia wasijaribu kutoroka hadi watakapo thibitisha na kuwaelekeza mahali pa usalama, pasipo hatari. Lakini, Mamilioni ya watu hawakutilia onyo hilo maanani.

Mji wa Chicago ulikuwa mbali sana na Toronto, kwa hivyo hawakutarajia usaidizi kutoka huko. Watu wachache walijaribu kutumia ndege ndogo na meli kuvukisha wakimbizi kuelekea nchi jirani. Watoaji wa huduma na utimishi wa usaidizi walikuwa mashakani, walihitaji mavazi ya kujikinga kwa haraka.

Rayford alijituliza na fikira kuwa, hata kama hana uwezo wa kuokoa jamii yake ataweza kusaidia watu wengine. Huenda kuwa bidii yake itamfungulia njia ya kusaidia Irene na watoto wake.

Karibu saa moja ya jioni, Rayford aliondoka kutoka chumba cha kungoja wageni waheshimiwa na kuelekea kiwanja cha magari ya kupanga. Alitaka kupumzika kidogo kabla ya safari yake. Alipokuwa anapita sebule ya kituo cha Heathrow, alikaribiwa na mtu mmoja, mwembamba na mwenye nywele nyeupe, mwenye umri wa miaka Thelathini hivi. Mavazi yake yalikuwa yamechakaa na mbovu mbovu. Mtu huyo alichomoa kitabu kidogo na kukileta karibu sana na uso wa Rayford. Kwa tamuko la sauti ya Kijerumani, alimuuliza kama anataka kitabu hicho. Jina la kitabu lilikuwa “Kuanguka Kwa Amerika.” Jina hilo lilikuwa limebandikwa juu ya picha ya bendera ya Amerika ambayo ilikuwa imepinduka juu chini. Rayford alisukuma mtu huyo kwa upande akiwa amejawa na maudhiko.

Wazo la kwanza lililomjia ni kuwa, daima kuta kuwa na mtu aliye tayari kujitajirisha kutokana na mashaka ya watu wengine! Lakini, alipofika nje, mara moja alipata wazo lingine. Inawezekana aje kuwa mtu aliye Uingereza tayari ametunga na kutoa kitabu kidogo kuhusu mambo yanayotokea sasa? Alikimbia upesi kurudi ndani ya sebule ya kituo cha ndege, macho yake yaliangalia kila upande akitafuta yule mtu. Mara moja, alimuona mwanaume yule akiwa amesimama karibu na meza ya kuonyeshana tikiti za kusafiri. Alikuwa anazungumza na watu wawili au watatu ambao walionekana kuwa wanamfukuza.

“Ulipata kitabu hicho wapi? Mwandishi ni nani?” Rayford alinong’ona akiwa karibu kupaza sauti. Alifanya bidii ili isionekane kama anajaribu kuanzisha ugomvi, alipovuta mkono wa yule mtu. Alikuwa na haja kuu ya kuelewa mambo yanayotokea.

“Marafiki wangu . pamoja na mimi, tulikiandika,” alijibu mtu yule kwa uoga. “Unajali kujua?”

“Ndio, ninajali kujua,” Rayford alitilia mkazo. “Ninajali sana. Lakini, kwanza nieleze mulijuaje kitakacho tendeka?”

Kwa sauti ya upole na kwa kutumia Kiingereza kisicho sanifu kabisa, yule mtu alimjibu. “Tumechunguza unabii uliokatika Bibilia. Tunaomba pia. Tumekuwa tukitangaza kuwa mambo haya yatatokea. Tumekuwa tukisema hivyo kwa miaka kadha sasa. Ni jambo la muhimu. Lazima usome kitabu hiki.” Paji la uso wake lilikunjana na alionekana kama ambaye anatia chumvi ili kuonyesha uzito wa yale anayosema. Lakini, itawezekana aje mtu kuzidisha maana ya uzito wa maafa ambayo yametokea Amerika?

Kijana Mjerumani aliongezea, “Kuna mambo mengine ambayo yanakuja. mambo yenye maana nzito zaidi.”

Rayford alitaka kusoma kitabu hicho lakini, kwa sasa alikuwa anahitaji majibu ya haraka. Alijitolea kumnunulia yule mtu -- aliyeitwa Reinhard -- chakula, kama ataketi na kuzungumza naye.

“Jambo la muhimu kwangu, nikuondoka ili niwape watu vitabu hivi,” alijibu Reinhard. “Tunaweza kuongea baadaye.”

“Tafadhali!” Rayford alimsihi akiwa karibu kulia sasa. “Nina safiri kwenda Canada leo usiku. Jamii yangu iko huko. Lazima nijue kinachoendelea kabla niondoke.”

Reinhard aliona kuwa sauti ya Rayford imejaa bidii ambayo hajapata kuona kutoka kwa watu wengine hadi sasa. Aliacha kauli yake ya mbeleni na kuuliza, “Unataka twende kuongea wapi?”

Rayford alimpeleka kwa meza katika mkahawa uliokuwa karibu, aliwaagizia chakula chao halafu akamfungulia Reinhard sakafu ili amueleze anayojua.

“Kile kinachoendelea sasa . ni adhabu na hukumu kwa Amerika kutoka kwa Mungu. Lakini pia, njia inafunguka ili nchi ya Urusi itawale Ushirika wa Umoja wa Mataifa. Dangchao amechaguliwa na Urusi, unaelewa?” Rayford alikuwa anajua kuhusu msukosuko ulioko duniani, kwa sababu mataifa mengi yalionelea kuwa Amerika inatumia nguvu na uwezo wake vibaya katika Ushirika wa Mataifa. Hadi sasa maelezo ya Reinhard yalieleweka lakini, hayo sio aliyokuwa anatafuta.

“Unasema ya kwamba ulijua haya mambo yatatokea kwa sababu ya kusoma Bibilia?” aliuliza bila kuamini.

“Siwezi kukuonyesha yale yote unayotaka kujua kwa muda huu mfupi. Utapata majibu ukisoma kitabu hiki.”

Desturi ya Reinhard ya kufupisha mambo ilifanya agizo hilo lisikike kama amri. “Utajionea mwenyewe. Kwa sasa, tuna wakati mdogo tu. Nitaendelea kwa ufupi tu. Bibilia inatueleza kuhusu nguvu za nchi tano fulani za dunia.” Alihesabu kwa kutumia vidole vyake. “Inatueleza kuhusu mnyama mmoja mkali anayeitwa Dubu, aina ya ndege anayeitwa Tai, Simba, Chui na Jogoo. Wanyama hawa wametumiwa kama ishara ya nchi za Urusi, Amerika, Uingereza, Afrika na Ufaransa. Lazima uelewe, Chui anatumiwa sasa kama dalili ya kushirikiana pamoja kwa Nchi Maskini.”

Rayford hakuelewa lakini, alimuachia Reinhard aendelee.

“Uingereza, Ufaransa na Amerika wana uwezo wa kukataza mradi na nia ya Urusi na China katika Umoja wa Mataifa. Nchi zingine Kumi za Baraza la Ulinzi . zinaitwa washiriki wa kuzunguka . wanaotoka nchi zingine.

“Kwa hivyo?” Rayford aliuliza kwa utulivu, ingawa alikuwa na maswali alingojea nafasi yake.

Reinhard aliendelea, “Mabawa ya ndege Tai yame ng’olewa. Utaona kwa kitabu. Iko katika Bibilia. Shambulio hili, ndilo kung’olewa kwa mabawa ya Tai. Baada ya Tai kuanguka, Simba . yaani Uingereza . itapoteza uwezo wake. Mabawa ya Jogoo, yatashikana na Chui. Yaani, Ufaransa pamoja na nchi zote za Ulaya zitashirikiana na Nchi Maskini. Unaona, ni kwa sababu myama Dubu . Urusi . itapunguza nguvu . yaani, itashinda kwa kusimamisha nchi zenye nguvu ili zisiweze kupigana naye. Imefaulu kwa sababu ya kung’oa mabawa ya Tai. Kwa kutumia usaidizi wa mataifa mengine kumi, kiongozi mpya ataongoza dunia nzima.”

Rayford alikuwa anaanza kupoteza uvumilivu wake. “Sina haja ya kujua mambo ya utawala na serikali,” alisema kwa hasira. “Je, una majibu yoyote? Jamii yangu iko huko. Kama kweli unaelewa kinachoendelea, ninaweza kuwasaidia kwa namna gani? Ni nini nitakacho hitajiwa kufanya?”

“Ni adhabu ya Mungu,” Reinhard alimjibu kwa utartibu. “Kama watu wako wangali hai, itabidi waondoke. Hakuna mtu atakaye ishi huko tena. Mwenyezi Mungu amekasirishwa na watu wa kanisa la Amerika.”

“Watu wa kanisa?” Rayford aliuliza akiwa ameshangaa. “Kwa nini watu wa kanisa?” alikuwa anafikiria Irene.”

“Wanapinga mafunzo ya Yesu Kristo. Hawajitayarishi kwa yale yatakayo tokea, na hawaambii wengine ukweli.”

“Bibi yangu ni mmoja wa watu wa kanisa,” Rayford alijibu kwa uchungu. Wakati wote alikuwa anaongea kuhusu.hiki.kitu kinachoitwa Dhiki Kuu ya kupita yote.”

“Hapana, hapana! Hii sio Dhiki Kuu . bado,” alijibu Reinhard. “Huu ni mwanzo wa mambo yanayokaribia. Lakini, Bibi yako atahitaji kuwa na imani inayoweza kumsaidia kuvumilia Dhiki Kuu. Sidhani atapata imani hiyo kanisani.”

“Kama anavyosema ni kweli . ataepuka mashaka hayo,” Rayford alijibu. Alishtuka kuwa anatetea yale ambayo hadi sasa alidhani kuwa upuuzi. “Bibi yangu husema kuwa atachukuliwa hadi mbinguni kabla ya mashaka hayo kuanza.”

“Je, alikuambia kuwa Amerika itapatiwa adhabu kabla aende mbinguni?” Reinhard aliuliza kwa upole, macho yake yakiwa yanaangalia mapaja yake. Rayford aliposhindwa kujibu, Reinhard aliinua kichwa na nyusi za macho yake.

Mwishowe, Rayford alisema, “Sijui. Sikumbuki akisema chochote kuhusu jambo hilo.” Hata alipojibu alikuwa ana kumbuka namna Irene alivyokuwa na huzuni walipozungumza kwa simu. “Labda, alisahau sehemu hiyo.”

“Atahitaji usaidizi . usaidizi wenye asili ya mambo ya roho.” Reinhard alisema hivi kwa huruma. Aliendelea pole pole kama mtu anayejiongelesha: “Ni vigumu sana kwa watu wa kanisa . hawawezi kukubali makosa yao.” Reinhard alikuwa amefungua macho yake kabisa na kuangalia macho ya Rayford kiwazi alipotamuka pole pole, “Chunga, usiitikie akimbie. Atataka kwenda kutafuta Yesu wake.”

Rayford hakutaka kusikia Bibi yake akitajwa hivyo, wakati ambapo inaonekana kuwa yuko karibu kumpoteza. Alikuwa amekasirika. Hakupata majibu aliyotarajia au yatakayo msaidia kutatua mambo, kutoka kwa mtu huyu wa ajabu. Hata hivyo, alikata kauli kuwa atasoma kitabu alichopewa baadaye. Aliomba radhi na kuondoka, naye Reinhard akabaki pekee na chakula chake.

Alipotembea kidogo, Rayford alipinduka kuangali mhubiri huyo wa barabarani, aliyekuwa anamaliza chakula chake kwa upesi, kama mtu ambaye hajapata chakula kwa muda mrefu.

 

 

Zion Ben-Jonah Aaandika:

 

Asili ya utabiri kuhusu kuanguka kwa Amerika inapatikana katika mafunzo kutoka Kitabu Cha Danieli 7:1-7, pamoja na Ufunuo wa Yohana Wa Yohana 13:1-2. Unabii wa Danieli mara nyingi huchukuliwa kumaanisha ukoo wa Enzi Kuu ya Babeli (inayofananishwa na Simba mwenye mabawa ya ndege Tai), Enzi Kuu ya Uagemi (inayofananishwa na Dubu), Enzi Kuu ya Kigiriki (inayofananishwa na Chui mwenye mabawa manne ya ndege ambayo yako juu ya mgongo wake), na Enzi Kuu ya Roma (inayofananishwa na Mnyama wa “kutisha” mwenye nguvu na uwezo, ambaye alivunja na kumeza ulimwengu mzima.) Siku hizi, ishara hizo nne zinatumika kufananisha mataifa manne kati ya tano katika Baraza la Ulinzi wa Umoja wa Mataifa. (Ishara ya nchi ya tano, China, ni Joka lenye mabawa na miguu minne yenye kucha, linalotoa moto na moshi kinywani.) Chui peke yake ndiye mnyama asiye maarufu siku hizi, isipokuwa kama ishara ya Afrika, Jeshi la Watu Weusi, au, labda, Nchi Maskini.

Ufunuo wa Yohana Wa Yohana 13:2 unatuonyesha kuwa, katika wakati ujao kutatokea enzi moja yenye nguvu na amri kubwa, ambayo itakuwa na hali ya wanyama waliotajwa katika Kitabu Cha Danieli sura 7, isipokuwa ndege Tai. Inaonekana kuwa, wakati huo Tai hakuwepo tena!

Kuna washiriki kumi wa kuzunguka katika Baraza la Ulinzi wa Umoja wa Mataifa, ambao wanatoka nchi zingine. Bibilia inatueleza kuwa kwa kutumia usaidizi wa “Wafalme” kumi, enzi iliyofufuka itamaliza kabisa enzi nyingine inayofananishwa na Malaya . ambaye ni mtawala wa biashara kuu za dunia. (Ufunuo wa Yohana Wa Yohana 17:1-5, 12-16) Na jina lake ni Babeli.

Kitabu Cha Maarifa Yote Ya Kiingereza kinataja mji mmoja katika dunia ya sasa unaoitwa Babeli. Mji huo unapatikana katika kisiwa cha Long Island kilicho katika Mji Mkuu wa New York, karibu sana na jimbo kuu la biashara ya rasilimali ya serikali na mali iliyokopeshwa kwa matumizi ya shirika la makumpuni!

 

 

3.LOO, HAPA! NA LOO, KULE!

 

Jua lilipopambazuka, mwangaza wa kutosha uliingia kwenye chumba cha gorofa ya chini katika makao ya jamii ya Rayford huko Prospect Heights, na kuwawezesha wafungwa watatu kuona bila kutumia mshumaa.

Chloe alichagua pembe moja itakayo tumika kama choo, halafu akaagiza Mama na ndugu yake wakunywe maji ya kutosha kutoka kwa vyombo vidogo kwanza. Hii itawawezesha kutumia mikebe iliyotupu kushikia na kuweka mkojo wao. Hivyo ndivyo watakavyo fanya maji yakiendelea kupungua.

Chloe alitoa shauri, “Labda tutalazimishwa kutafuta njia ya kubadilisha mkojo kuwa maji tena, maji yakiisha kabisa.”

“Chafu, mbaya sana!” Raymie alijibu. “Kwa nini tusichote maji kutoka gorofa ya juu?”

“Tuna taabu moja,” Chloe alisema. “Hakuna maji. Inaelekea kuwa mfereji mkuu ulipasuka kutokana na pigo la mzinga. Huenda tutaweza kupata maji kutoka kwenye chombo cha kuumba barafu(kinachotumika kuhifadhi vyakula au kubadilisha maji ili yawe barafu), baada ya siku chache ijapokuwa sidhani kuwa tuta pata maji ya kutosha. Sisemi kuwa itabidi tunywe mkojo lakini, lazima tuwe tayari kwa jambo lo lote litakalo tokea.”

Chloe alikusanya vijisanduku vya karatasi na gazetti nzee, ambazo watatumia kushikia na kuweka mavi, na kuziweka katika pembe moja.

“Tutafanya nini na harufu mbaya?” Raymie aliuliza.

“Moja ya vitu viwili,” Chloe alimjibu ndugu yake kwa ukali, bila utulivu. “Tuvumilie au tupate maumivu ya tumbo. Tayari tunajua wewe utakavyo fanya.”

Irene alikaa kimya kabisa. Alikuwa na mawazo akilini kuhusu jinsi atakavyo tatua jambo nzito.

Kuelekea saa tatu ya asubuhi, saa tano baada ya kombora na mzinga wa mwisho kuanguka, jamii yote ilishtuka na kutazama juu pamoja waliposikia sauti ya miguu ikikimbia katika gorofa iliyojuu yao. Mara moja, mlango wa bohari ulifunguliwa na Vernon na Elaine Billings, ambao walianza kuteremka ngazi. Mwangaza kutoka gorofa ya juu ulitia kiwi kwa macho na kufanya waliyojificha kuwa kama vipofu. Kwa upande mwingine, giza iliyojaa katika bohari ilifanya Askofu na Bibi yake pia wawe kama vipofu.

“Haraka! Funga mlango!” Chloe alisema kwa sauti kuu. Elaine Billings alifuata maongozi, halafu akakamata bega la Bwana yake ili asianguke, akiwa anajikwaa gizani. Vernon Billings alikuwa na mwili mkubwa wenye nguvu. Kwa hivyo, hakuwa na shida alipomshikilia Bibi yake mwenye mwili mdogo.

“Kweli, kuna giza hapa!” Askofu alinena huku akishikilia ubao wa nguzo za kitalu cha ngazi kwa nguvu. “Hamuna mishumaa?”

“Tunajaribu kuhifadhi mishumaa tuliyo nayo,” Chloe alimjibu kwa sauti yenye baridi, bila upendo. Alijua kuwa anafaa kuongelesha Askofu na Bibi yake kwa heshima. Wakati wote walikuwa wazuri na wapole kwake. Lakini, kuna kitu ambacho hakuweza kutambua au kuelewa, ambacho kilimsababisha awe na hasira kwa ajili yao.

“Dada Strait, lazima tukueleze kilichotendeka!” Askofu alisema kwa ghafula. “Endelea! Waelezee Elaine!”

Bibi yake alisema kwa utiifu, “Unaona, Irene, tuliomba kuhusu jambo la kwenda Montana, baada ya Askofu kuzungumuza na wewe kwa simu leo asubuhi. Tuliuliza Mungu atupe ishara kama kweli ni yeye.

“Tulikuwa tumeketi pamoja katika ghala ya chini ya nyumba, tukila kifungua kinywa, wakati ilipotendeka. Vernon alisikia sauti. Kwa kweli, sote wawili tuliisikia,” aliendelea akiwa ameangalia Bwana yake kwa wasiwasi. “Ilisema ‘Njoo!’ Hivyo tu: ‘Njoo!’”

Askofu Billings aliendelea na hadithi kutoka hapo. “Tuliongea kuhusu sauti hiyo kwa muda, halafu Elaine akaenda jikoni na kurudi na kisanduku chake cha ahadi. Bila kuchagua tulitoa somo moja kutoka mwisho wa maandishi ya Marko Mtakatifu, anaposema, ‘. hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa.’

“Unaona vile Mungu alivyokuwa akisema, Dada? Alikuwa anatupatia ahadi kwamba atatulinda, kama tutaondoka kuelekea Montana bila kusita. Tumetayarisha mzigo wa chakula, maji na nguo chache, na sasa tuko tayari kuondoka.

“Lakini, tunataka kukupatia nafasi ya kuandamana na sisi. Utaenda na si, Dada?”

Elaine aliinjilia kwa sauti nyororo na tamu, “Tafadhali twende pamoja, Irene.”

“Ee! Sijui,” Irene alijibu. “Una hakika ya kuwa hakuna hatari? Kwa nini tusingoje kidogo kwanza?”

“Ili tuchelewe mbingu ikifunguka?” Elaine aliuliza. “Angalia, tumekuwa nje sasa kwa muda wa nusu saa na tungali wazima kama dhahabu. Hata mimi nilikuwa na uwoga mwanzoni, lakini sasa siogopi.”

“Mungu atakulinda, Irene.” Askofu Billings alisema kwa upole. “Nina hakika. Tafadhali, muamini, twende sote, Irene!”

“Mama, tunaweza kwenda?” Raymie aliuliza. “Ni bora kuliko kukaa mahali hapa. Angalia, wako sawa, hawajaumia!”

“Na wewe, Chloe? Utaenda na sisi?” Irene aliuliza, sura yake ikiwa imejaa huzuni alipokuwa akiomba bintiye amusikilize.

“Hapana! Siendi. Kama wewe unataka kufanya jambo pumbavu kama hilo, mimi . mimi sitaki kuwa hapo. Fikiria sana Mama, unadhani hivi ndivyo Mungu atakavyo fanya? Mimi ninaonelea kuwa nyinyi nyote mumeshikwa na woga mkuu wa ghafula, kwa sababu mambo hayakutokea vile mlivyo tarajia. Itikieni kuwa mulikosea. Si jambo kubwa!”

“Namkemea pepo huyu mwenye wasiwasi!” Askofu Billings alisema, macho yake yakiwa yamefinyana kwa uangalifu na akiwa ameinua na kunyoosha mkono wake kuelekea upande wa Chloe. Mwanaume huyo alionekana kuwa mkubwa zaidi. Alikuwa amesimama sehemu ndogo kutoka chini ya kipandio cha ngazi katika chumba hiki kilichokuwa na giza nusu, na nuru nusu. Chloe alirudi nyuma kwa mshtuko. Hakuwahi kuona Askofu akiwa hivi mbeleni, na hakupendezwa hata kidogo na ukali aliyouona sasa.

“Namkemea pepo wa wasiwasi, katika jina la Yesu!” Askofu alipaza sauti kwa njia ya kuigiza. Halafu, akaweka mkono wake chini na kuendelea kutumia sauti yake ya kawaida ambayo ilikuwa tamu kama sukari. “Gari inangojea, Dada,” alisema kwa upole. “Chaguo ni lako sasa. Unaweza kufuata imani yako au ubaki hapa na uchelewe na kufunguka kwa mbingu. Unasemaje, penzi? Ni wakati wa kuondoka.” Askofu alianza kupanda ngazi.

“Tafadhali, Chloe!” Irene alisema kwa sikitiko. “Tafadhali, enda na si!” Yeye pia alianza kupanda ngazi akielekea mlangoni.

“Mama, hapana! Hujui unavyofanya!” Chloe alimrudishia kwa sauti kuu, akiwa ameshtuka kuwa Mama yake anaweza kuamini watu wawili ambao walikuwa wamejidanganya. Walikuwa na haja kubwa ya kuamini kile ambacho walichotaka sana kuamini. “Je, haumjali Baba?”

 

“Mueleze kuwa nina mpenda.” Hayo tu Ndio Irene aliyoweza kusema kabla ya kupinduka na kukimbia, huku akiwa analia kwa sauti ya huzuni alipokuwa anapanda ngazi. Elaine na Vernon walikuwa tayari wamefungua mlango na kungojea katika sebule iliyokaribu na jikoni.

“Unakuja, Raymie?” Irene aliuliza swali hilo kama wazo la baadaye. Alikuwa amedhani kuwa Raymie atakubaliana na cho chote atakacho amua.

“Kwaheri, Dada,” Raymie alisema akiwa amemkumbatia Chloe na mkono mmoja, kwa upendo. “Pole kwa taabu zote nilizokupatia.” Halafu, yeye pia akaelekea kupanda ngazi.

Chloe alikuwa ameshtuka zaidi, hakuweza kusema cho chote. Raymie alikuwa amefika mlangoni kabla Chloe atamuke neno moja, halafu akasema, “Raymie.Hapana.”

Lakini, walikuwa wameondoka.

 

 

 

Zion Ben-Jonah Aaandika:

 

Maelezo ya hali ya mambo duniani kabla ya kurudi kwa Yesu, ni ya watu kuwa na wasiwasi na hofu kuu kwa sababu hakurudi wakati ambapo walipotarajia. Yesu alituonya katika maandishi ya Mathayo Mtakatifu 24:23-27, aliposema, “Wakati huo, mtu akikwambia ‘Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule’ msisadiki. Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule. Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele. Basi wakiwaambia, ‘Yuko jangwani,’ msitoke; ‘yumo nyumbani,’ msisadiki. Kwa maana kama vile umeme utokavyo Mashariki ukaonekana hata Magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja kwa Mwana wa Adamu.”

Tupilia mbali mafunzo yanaohusu “kufunguka kwa mbingu, kwa siri!”

Ukoo wa mafunzo hayo, pamoja na mafunzo mengine katika makanisa ya siku hizi, ni kuwa watu wanapendelea mwepuko au kuponyoka bila malipo. Ni rahisi sana kujidanganya na kuamini kile ambacho tunachotaka kuamini, ukipenda usipende hata ikiwa kweli au uongo.

Kwa mfano, tuseme kuwa ni funzo kuwa hatutapata ugonjwa wowote, au hatuna budi kufanikiwa, au kuwa tunaweza kuendelea bila kuogopa au kutii Yesu na Mungu atatusamehe, au kuwa haitabidi tuvumilie Dhiki Kuu. Mafunzo haya hupata sifa bora na yanapendeza watu wote. Lakini, sio kwa sababu ni ukweli, bali kwa sababu yanavutia. Yanasema vile ambavyo watu wanavyotaka kusikia.

Isipokuwa Wakristo wawe na nguvu ya kukubali kosa waziwazi wakionyeshwa (angalau kwa njia ya mambo na hali ilivyo, kama sio kwa njia ingine), au wataendelea kubadilisha mwepuko wa aina moja na hali ingine geni ambayo itachekesha au kutazanisha zaidi, kwa madhumuni ya kukataa kukiri kosa lao.

 

 

4. KUTAFUTA

 

Alipokuwa amerejea pale Hilton, Rayford alifungua kijitabu. Aligundua kuwa Reinhard na rafiki zake walijiita "Jesans". Aligeukia utangulizi wa kitabu.

Ni rahisi kwetu sote kupata makosa kwa watu wengine kuliko kuyaona kwetu sisi. Watu wa Marekani sio tofauti. Ukitazama shughuli zote za kidini Marekani hivi sasa, ni rahisi kuona watu (nje na ndani ya makanisa) wamepumbazwa kuichukulia dini kana kwamba ni imani halisi. Lakini shughuli za kidini, mila, na hata maono ya kiakili havina mengi kuhusu njia nzuri za zamani za kutii mambo aliyo fundisha Yesu katika Bibilia. Na ukaidi wa Marekani utaadhibiwa kabla wa yeyote ule kwa sababu wale wanaojua mengi wana mengi ya kujibu.

 

Utangulizi uliendelea.

 

Ikiwa ni faraja yoyote, Bibilia inaahidi kwamba kutakuwa na siku kubwa ya kuhesabiwa kwa ulimwengu mzima, kuliko ile itakayowafikia wamarekani. Lakini Bibilia pia, inasema kuwa hukumu lazima ianze na wale wanaodai kuwa watu wa Mungu (1Petro 4:17). Na jinsi tutakavyofafanua juu ya kijitabu hiki,hukumu ya Marekani itakuwa kama uharibifu wa Sodoma na Gomorrah kusikika kama safari fupi ya ushirika wa Jumapili wa watoto.

"Sawa, hayo yote ni kweli,"

aliwaza Rayford Strait. Na akaendelea kusoma

 

Imefanyika tu kuwa Mungu hutumia taifa ili kuwahukumu watu wake_ Israeli. Kwa sababu Marekani ni mfano wa Agano Jipya la Israeli, Mungu atatumia ujumla wa kutoamini kuhukumu Marekani. Si jambo kubwa. Sio mashindano ya kiroho kati ya Marekani na nguvu nyingine ya kisiasa. Ni swala la uajibikaji wa kibinafsi kwa wale wanaostahili kujua zaidi.

Billy Graham anaripotiwa kusema:

"Ikiwa Mungu hataiharibu Marekani, basi anastahili kuwaomba msamaha Sodoma na Gomorrah".

Dhana ni kwamba Mungu anastahili kuiharibu Marekani kwa sababu ya ushoga, au kutoamini kwake, au ukahaba wake, au kwa kamari, au madawa ya kulevya, au kwa kuavya. Ila sio kwa sababu ya dhambi za makanisa. Umiliki mali, maringo, unafiki, wokovu wa kujidhania ama mojawapo ya yale Yesu alikosa kukubaliana nayo.

Ibrahimu alidhania kuwa walikuwepo sio chini ya watu 100 waongofu kule Sodom siku zake. Alifanya hivyo pengine kwa sababu wengi wao walihudhuria hekalu yake au kusaidia mapambano yake ya kiunjilisti. Ibrahimu alikuwa amedanganywa na maongezi ya kidini yaliyokuwa na kinyume. Yesu alipofananisha dhambi za Sodoma na watu siku hizi, hakutazamia kutaja ushoga, uchawi, au kitu chochote cha kusisimua. Alisema tu kuwa shida ilikuwa ni umilikaji na mahitaji ya kijamii, hata kwa wale waliohudhuria mahekalu (ama "makanisa" yalivyoiytwa siku hizo.)

Ilikuwa katika hatua hii ambapo Rayford alipoteza haja.Alikuwa amedumisha amani katika ndoa yake na Irene kupitia kwa makubalino yasiyosemwa. Angevumilia kujihusisha kwake na Kanisa ikiwa Irene angevumilia kutojihusisha kwake Rayford. Baadhi ya wakati alikubali kuhudhuria kaanisa ndiposa apate mapendeleo fulani kutoka kwa Irene, lakini kile ambacho kundi la Jesani lilikuwa likipendekeza ni kuwa apate dini na amtenge Irene wakati huo huo. Hali gani ya kupoteza mara mbili!

Alikitumbukiza kitabu katika mkoba wake wa kusafiria na akaenda kulala. Saa kumi na moja asubuhi Rayford alirudi kwa uwanja wa ndege kusafiri kwa safari ya rehema huko Toronto. Masaa machache nje ya jiji la London aliingia katika bendi ya mawasiliano ya "Satphone".Kwa bahati mbaya mwingi wa ule wakati mzuri sana ulichukuliwa na mawasiliano rasmi ya kuelekeza ndege za Toronto.

Ilivyofanyika Rayford alikuwa ameorodhesha kwa ufupi yale aliyotaka kumwambia Irene, ndiposa angetumia bora zaidi sekunde chache zilizosalia kwa muda wa mawasiliano ya "Satphone",wakati shughuli rasmi ingekuwa imekamilika. Ingawa ilikuwa baada ya saa tisa asubuhi kule Illinois, Chloe alijibu kwa mlio wa pili. Hiyo ilikuwa bahati, Rayford alifikiria. Chloe alifikiri wazi kuliko Irene, na angefuata maagizo ya Rayford vyema.

 

"Chloe, huyu ni baba.Nina dakika moja tu, kwa hivyo sikiliza kwa makini. Je una kalamu ya mate na karatasi karibu?"

 

"Ndio baba, lakini"

 

"Vizuri,.Tafadhali zima simu kwa masaa arobaini na nane baada ya mimi kukata mawasiliano, hivi betri itakaa muda mrefu.Wanielewa?"

 

Chloe alikuwa tayari amewaza hivyo na alikuwa amezima simu kwa wakati mrefu siku iliyotangulia, alikuwa na uhakika kwamba babayake hajapiga simu kwa muda wa saa 18, hata ingawa kuna mengi aliyokuwa akitaka kujadili naye. "Ndio ninayo hayo. Lakini, Baba."

"Nitakuwa Toronto saa 8:30 saa ya kwenu, na nitahakikisha kwamba wale watu wa kuhudumia waliojeruhiwa wanakujua. Nitapiga simu ili nikupatie maelezo kamili nikielekea London siku chache zijazo."

"Baba!" Chloe aliita kwa sauti. "Mama ameondoka!"

"Ameondoka?" Rayford alidhani kwamba Irene alikuwa ameenda kutafuta bidhaa fulani, huku akisahau kwamba ilikuwa saa tisa za asubuhi katika saa za Prospectus.

"Sijui! Mahali kule Montana. Alienda kwa pamoja na Vernon na Elaine Billings jana. Wanafikiria kwamba Yesu ako huko. Raymie aliambatana nao. Nilijaribu kuwazuia, Baba. Nilijaribu!"

Ingawa kwa mshangao, ilichukua muda mfupi kwa Rayford kuamua kwamba kimsingi alifaa kumnusuru Chloe. Alibakia na sekunde chache.

"Haya. Tutaangalia hilo baadaye," alisema. "Lakini kwa sasa hali yako ni ipi kipenzi?"

Chloe kadhalika alikuwa na orodha ya mambo ya kusema akilini mwake. Hii ilikuwa fursa ya kutumia.

"Niko salama, Baba. Maji ndio kitu muhimu kwa sasa kuliko chakula, lakini hakuna haraka. Nniko mzima, lakini mwenye uchovu."

Alikuwa akisinzia. Hali yao ya mawasiliano ilikuwa ikididimia."

"Unaendelea vyema kipenzi! Nakupenda!" Rayford alisema kwa sauti, huku akishindwa kuelewa iwapo alimsikia.

Ghafla fikira zake zikamrejelea kuhusu Irene. Kukimbilia Montanna kumtafuta Yesu? Kwa hakika mkewe alikuwa timamu kuliko ilivyo! Alikuwa akifikiri nini? Ndiposa alikumbuka Reinhard akilalamikia kitendo cha Irene. Ilikuwaje kwa mgeni huyu kuelewa kwamba atafanya hivyo? Alimuuliza Rayford maelezo, lakini aliyakosa yalipotolewa. Jinsi gani yalivyo chukiza!

Ndege ilikuwa ikielekea vyema, Hivyo basi Rayford alimgeukia rubani mwenza. "Waweza kushika usukani kwa saa moja hivi, Chris?" aliuliza.

Rubani mwenza alimtazama kisha kuangalia mbele. "Roger," alijibu. "Hakuna shida"

Rayford alichomoa kitabu alichokuwa amepuuza hapo awali kutoka kwa mfuko wake.

Kwa wakati walipofika Canada alikuwa ameelewa kile walichosema Jesans.

Walikuwa wametabiri shambulizi la Urusi kule upembe wa Kaskazini. Halikadhalika walitabiri kwamba manusura wote wataokolewa kutoka Amerika, na kwamba nchi nzima itatowekwa kutokana na kiasi cha uharibifu.

Magonjwa yanayoongezeka, mitetemeko ya ardhi iliyozidi, na hatari kutokana na kuharibiwa kwa utando wa ozone yalikuwa yametabiriwa kwenye Bibilia.

Matukio mengine yaliyotabiriwa yalikuwa bado hayajaonekana na kumvutia Rayford. Alinakili kila moja kwenye akili. Na hasa mabadiliko yaliyokuwa ndani ya kitabu hicho kuhusu Umoja wa Mataifa. Kutokana na masimulizi ya mashirika ya habari, vita kati ya Amerika na Urusi vilifikia kikomo mara moja kama vilivyoanza. Urusi ilikuwa imejitoa kuwasaidia manusura na kuwanusuru. Katibu Mkuu Dangchao aliongoza mkutano wa waandishi wa habari muda mchache baada ya ripoti hiyo. Alijitweka jukumu la kuongoza shughuli ya kunusuru. Shambulizi hilo lilikuwa likichukuliwa kama mkasa wa kimaumbile na wala sio vita vya kulaumu Urusi.

Sio kwamba mataifa yote hayakukemea shambulizi. Lakini ukweli wa kuuma, nani aliyekuwa na jeshi lililojihami kukabili Urusi. kwani Amerika ilikuwa imeondoka? Kila mahali duniani watu walikuwa wapigwa butwa kutokana na kuharibiwa kwa U.S. hatukuwa na yeyote wa kugeukia.

Ilimshangaza Rayford kwani kijitabu cha Jesans kiliweza kutabiri hayo yote. Kilieleza kwamba tamaa ya Amerika ilikuwa imesababisha umasikini kote duniani. Kuhamia kwa wasomi hadi huko, biashara kuu ulimwenguni, ujuzi katika teknologia ya habari, kunyakua mazao ya mataifa yanayoendelea, kama vile chai, kahawa, sukari, pamba, tumbaku, viungo vya mchuzi na kuharibu kwa misitu katika mataifa yanayostawi. Hasara kubwa iliyotokea Amerika ilikuja kuadhiri dunia nzima. Hata msaada wa Amerika ulikuwa umekadiriwa kuendeleza nguvu za Amerika, kwa mikopo na misaada ya zana za kivita. Kwa uchache msaada ulikuwa kwa watu waliodhulumiwa na Amerika hadi kiwango cha kufa.

Rayford alitaka kuchambua yote aliyosoma., alikuwa akishuku maoni yake.

 

* * *

 

Ilikuwa yapata saa 24 tangu kombora la kwanza kulenga. Mamia ya wakimbizi tayari walikuwa wameanza kuingia Canada. Wachache kati ya wale waliowasili walikuwa wamejeruhiwa., lakini wengi walikuwa na uchovu kutokana na safari, na hata kupotewa kwa hamu ya chakula. Kwa wengi hali hii ingalisababisha kuadhiriwa kwa matumbo, ubongo na hata kifo. Hii ndio ilikuwa adhabu yakujitokeza mara tuu baada ya mlipuko.

Toronto nzima (kama miji mingine ya Canada) ilikuwa ikisukumwa kuwachukua majirani wa Kusini. Ilionekana kama mambo yamezidi mipaka., na msongamano ndio mwanzo ulikuwa umeanza. Katika muda wa miezi miwili ijayo, Toronto itakuwa imepokea zaidi ya watu milioni sita.

Siku mbili zilizofuatia, Rayford alizunguka huku na huku katika mashirika akitafuta usaidizi kwa Chloe. Ilihitaji apige simu kwanza, alipokutana na mtu wa kumpatia matumaini, angalichukua gari na kurudi, huku akitumai kukutana na ofisa fulani atakayempendelea endapo atakutana na mwanawe. Katika safari aliihiari kutoa damu, na kujishughulisha kujenga hema katika uwanja wa mpira upande wa kusini mwa mji. Dhamira yake haikuwa ya kibinafsi. Kwa hakika alitaka kusaidia.

Hatimaye alipeana maelezo kuhusu Chloe, Irene, Raymie na wale Billings katika orodha ndefu ya kimataifa, ambayo ingalitumiwa kutambua waadhiriwa, na kuwaunganisha manusura na jamii zao.

Utaratibu wa Pan Con ulihitaji Rayford kurejea London Ijumaa jioni. Ilikuwa kinyume na mkataba kwake kusafiri baada ya muda mchache; lakini kibinafsi angalifurahia kuondoka mapema. Katika juhudi za kumpata Chloe hakuwa na uwezo Toronto sawa na alivyokosa kule London. Lakini kila safari ya ndege ilimaanisha kumpigia simu chloe. hadi pale moto ulipungua kwenye simu ya rununu.

Hata ingawa Chloe, Raymie na Irene ndio waliokuwa kwenye fikira yake, Rayford kadhalika alifikiri kuhusu yale aliyosema Reinhard, na pia uhusiano wake na Mwenyezi Mungu. Daima alimuamini Mungu licha ya kunyamaza tu. Wakati wa ukiwa yeye huomba Mwenyezi Mungu. Mabishano yake kuhusu Makanisa yalikuwa tu tofauti za imani ya kiroho. Hata hivyo, aliamini kwamba imani ilikuwa zaidi ya yote aliyokuwa akiona kwenye Makanisa.

Sasa ilionekana kama kwamba amepata. Jaribio la Makanisa kumshawishi yalikuwa yamemkera; lakini uwepo wa Jesans ulimfanya kusadiki. Hapa kulikuwa na watu wenye bidhaa. Walikuwa na uwezo wa kutazama na kuchambua undani wa dhehebu--ikiwemo uingilisti wa Kiamerika--na kutoa heri kamili. Alisumbuliwa na yale aliyosikia, lakini wakati huo, alihitaji kujua mengi.

Hivyo basi, Ijumaa asubuhi, Rayford alipiga nambari ya rununu aliyopewa na Reinhard, kuona iwapo angalikutana na Jesans, punde tu atakapo wasili kule London.

"Tutakuwa tukigawa kule Hounslow Jumamosi, na kulala katika kituo cha huduma za Heston, kule M-4," Reinhard alisema kwa lahaja.

"Wewe hauna afisi?" Rayford aliuliza.

"La tuko na banda la kurekebisha magari la rafiki yetu," Reinhard alijibu.

"Lakini mnalala wapi?"

"Kwenye gari. Utaona kesho," Reinherd alihakikisha.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

Kuna aina mbalimbali ya watu wanaotabiri kwamba kutatokea shambulizi la ajabu huko Israeli "Kutokea Kaskazini". Wachambuzi wa Bibilia wameona kwamba Urusi ndio inayotarajia kusababaisha shambulizi hilo. Hata hivyo, wengi hawafahamu kwamba Amerika (U.S) ndio Israeli ya kisasa, na kwamba shambulizi la Urusi kutokea upembe wa Kaskazini mwa dunia, itakuwa ni shambulizi "kutokea Kaskazini."

Katika mwanzo wa kitabu cha Jeremia, Mungu anamuuliza mtume anachotazama usiku mmoja, na akasema anatazama chungu kinacho chemsha maji. Na kusema uso uliomo unaelekea Kaskazini." Mungu anaendelea na kumuonya kwamba chungu kinaashiria shida kutokea kaskazini. shida itakayopelekea watu wake kwenye "maji moto" kwa maongezi ya kuashiria. (Jeremia 1:13--14)

Ni hali ya kushangaza kwamba nyota kubwa ya upande wa Kaskazini mwa dunia ni Mdila Mkubwa (au `nyungu kubwa') na wahitaji tu kulainisha nyota mbili "usoni" ili kuona Nyota ya Kaskazini. Upande mwingine Nyota ya Kaskazini ni maarufu. Nyota hiyo hujulikana kwa Kilatini kama Ursa (au Urusi - Russia). yaani Bearl.

 

 

5.Njiani Kuelekea Montana

 

Ilikuwa ikikaribia saa tatu kamili saa za jioni siku moja Ijumaa ya Mei. Mahali palikuwa katika barabara moja kaskazini mwa Amerika ya Magharibi ya Kati. Katika historia, ilikuwa ni usiku wa kutafakari urembo wa maumbile. Lakini katikati ya uharibifu mkubwa kuwai kutokea, hayo hayakuwa katika fikira.

Irene Strait alitazama mzee aliyekuwa kando ya moto wa kambi. Alimuangalia kwa huruma lakini kwa kuchanganyikiwa. Kwa miaka mingi alimuheshimu-- na labda kumsujudu. Alitamani mumewa angalikuwa vivyo hivyo. Kwa sasa Vernon Billings alionyesha ujasiri na nguvu. Tamaa yake ya kutamani kufika Montana iliendelea, hata ingawa ilionekana kama atakufa kutokana na msimamo wake wa kishenzi.

Haikuwa bora kumuita Vernon Billings tapeli, iwapo ilikuwa sawa, basi alikuwa amejitapeli mwenyewe pia. Alikuwa amejitolea kulala sakafuni nje ya ukumbi wa Eau Claire, Minnesota, ili Raymie na wanawake wale waweze kulala vyema ndani ya gari. Lakini punde tuu mvua ilipoanza kunyesha na kulowa, ndipo alipokimbilia kujiunga nao ndani ya gari. Madhara ya bomu lililolipuka kule Minneapolis tayari yalikuwa yameonekana, na hasa kuonekana zaidi baada ya mvua.

Vernon alilala nje tena Alhamisi usiku, karibu na mpaka wa Dakota, kwenye barabara ya 94. Hali hii ilimfanya kuwa dhoofu kuliko wanahiji wenzake waliokuwa ndani karibu na mzunguko wa barabara ya 94, upande wa Magharibi na barabara ya 85 kuelekea Regina Kaskazini, Canada.

Lakini Irene hakuwa anafikiria kilichomfanya Vernon kulala nje siku hizo mbili, kama ulikuwa ujasiri au ujinga. Alikuwa akifikiria juu ya tabia yake siku hiyo.

Maji na chakula yalikuwa haba na ghali, lakini mafuta ya gari ndio yalikuwa katika fikira ya wasafiri wengi katika barabara kuu za taifa. Lori za kubeba mafuta hazikuonekana, Vituo vilivyouza kwa bei ya kawaida vilikuwa vimefungwa. Msongamano wa magari ulikuwepo, na magari yalisimama na kuenda, huku wakiyumbayumba kwa kutafuta sehemu bora ya kupitia au kuepuka magari yaliyokuwa yamekwama. Hali hii ilipelekea kutumia mafuta mengi.

Kufikia ijumaa asubuhi, vituo vilivyokuwa kuwa na mafuta viliweka bei waliyotaka. Hundi za pesa na kadi hazikuwa na manufaa na haingewezekana kupata fedha kutoka kwa benki. Wanahiji walikuwa na pesa chini ya $100 walipofikia kituo cha mafuta alasiri, na kuona tangazo la mafuta kuuzwa kwa $1,000 kwa tanki. Hali hii ilikuwa ya kutatanisha.

Vernon alisimamisha gari hilo kubwa la mji wa Lincoln karibu na matuta, kisha kuegemeza kichwa kwenye mduara wa usukani wa gari na kusema maombi. aliinua kichwa, kuegemea upande wa Elaine na kuchukua kiraka katika kisanduku, kisha kumgeukia Irene nyuma ya kiti. "Irene weka bomba la mafuta kwenye tanki na kuwachilia mafuta punde muhudumu wa kituo atakapoasha mashine?" Irene aliona Eleine akiwa ameshanga.

"La, Vern. Wacha." Elaine alianza.

"Nitawacha gari lingurume ili tusipoteze muda," Vernon alisema, bila kuzingatia fikira za Elaine alipoelekea kwenye chumba cha kituo cha mafuta. Alibaki humo huku Irene akiweka mafuta. Alipomaliza kuweka mafuta, Vernon aliingia kwenye kiti cha dereva na kulivuRomasha gari hadi kwenye njia.

Hakuna aliyesema chochote, ila walifahamu kwamba ametumia bunduki iliyokuwa ndani ya kile kiraka kupata mafuta.

"Sio kwamba nimeiba kwa mabavu," alisema, huku Elaine akimtazama kutoka nyuma. "nilimuachia pesa zote tulizokuwa nazo. Yeye ndiye aliyekuwa akitekeleza wizi. Ilikuwa kujikinga."

Hakuna la ziada lililonenwa siku yote, haata hivyo, Irene na Raymie waliangaliana kwa mshangao juu ya tukio hilo. Raymie angalitaka ufafanuzi zaidi; lakini Irene hakuwa na ufafanuzi.

Tanki la mafuta lilikuwa likikaribia kuisha walipoona kambi ya wanahiji waliokuwa wakimtafuta Masia Montana. Macho ya Vernon yalivutiwa na moto wa kambi. Hakuna yeyote katika kundi la Lincoln aliyebeba kiberiti, na kulikuwa na baridi kal. Magari mengine manne yalikuwa yameegemezwa karibu na moto, huku watu wakiongea na kujadili yale watakayoona kule Montana.

Wote walionyesha dalili ya kuchomwa kwa miali mikali. Baadhi yao, kama Vernon, walikuwa wakipoteza nywele zao, na kupata majipu kwenye ngozi yao. Lakini wote walisisitiza kwamba shida zao zitaisha wakati watakapofika Montana na kumuona Mwokozi wao

Irene alipomuangalia Vernon, alikumbuka yale Elaine alimueleza walipo lala siku ya pili kwenye gari, baada ya Raymie kulala.

"Ni kucheza na akili yangu" alisema. "Unajua sauti tuliyoongea juu yake kule Illinois? Ile iliyosema 'Kuja'."

Irene hangesema kwamba Elaine alikosea kuhusu "Ishara" kutoka kwa Mungu, au kwamba Vernon alifanya makosa kwa kulalamikia unyang'anyi wa mkuu wa kituo cha mafuta. Ilikuwa baadhi ya yale aliyokuwa akitafakari na kuanza kuona na kuelewa juu ya mambo mengi katika mwangaza mpya.

Katika kambi ya wanahiji ya cloverleaf, wanahiji wagonjwa, wanyonge na wachafu walikuwa wakiamuka kutoka kwa vitanda vilivyokuwa karibu na eneo la moto na kukusanyika kando ya gari moja la zamani. Dereva wa gari hilo alikuwa amepanda nyuma ili kuwaeleza kwamba alikuwa na galoni 44 za mafuta ya kuuza. Lakini hawakua mbali sana na mpaka wa Montana, na kiasi cha mafuta waliyokuwa nayo kingaliwafikisha huko.

Msongamano wa magari ulikuwa umepungua upande wa magharibi, kwa vile watu wengi kama dereva huyu walikuwa wakielekea Kaskazini. Mtu huyu alikuwa amechukua mafuta mengi kuliko kiwango cha kumfikisha Canada, na sasa alikuwa akiuza yale ya ziada ili kupata pesa.

Magari mengine yalisimamishwa katika cloverleaf. magari yaliyoelekea kaskazini mwa barabara ya 85. Watu walitoka sehemu za mbali kama Denver Kusini ili watoke nchini humo. Watu kutoka kambi zilizokuwa karibu walisongea kusikiza udalali huu.

Lakini wachache waliokuwa hapo hawakuwa na pesa kujiingiza katika udalali huo. Tulibakia na washindani watatu pale bei ilipofikia $1,000. Miongoni mwao walikuwa ni Tom na Betty White--wakongwe wawili waliokuwa na wajuku wawili

Irene alikuwa ameongea na Tom na Betty hapo awali jioni. Watoto hao walikuwa yatima. Betty alikuwa akiwatunza watoto hao pale wazazi wao walikuwa katika sherehe, na sehemu ya mjengo wa St. Paul ikashambuliwa.

Wakongwe hao walisikia kuhusu Masia wa Montana kutoka kwa jirani, na kujiunga na msafara. Tom alikuwa ametoa pesa za likizo siku moja kabla ya shambulio, hivyo basi alikuwa na pesa nyingi kuliko yeyote aliyeshiriki katika udalali. Alikuwa amemaliza mafuta yake kwa kukosa umakini yadi mia moja kutoka cloverleaf. Wote wawili walikuwa na udhaifu, na walishindwa kutembea. Uwezekano wa kuenda hadi kituo cha mafuta kisha kurudi haukuweko. Hata angalipata kituo cha mafuta, bei yake ingalikuwa juu zaidi.

Baada ya kuangalia tena katika kibindo chake huyo mzee alisema, "Elfu moja na mia mbili!" Wale washiriki wengine wawili walijiondoa kwenye king'ang'anyiro hicho. Yule mtu alitangaza kwamba Tom ampelekee pesa hizo. Betty aliruka kwa furaha.

Lakini Vernon Billings alienda karibu na gari hilo. Aliinua mkono wake wa kushoto ili dalali huyo auone, alimnong'onezea kwa kimya. Walisalimiana, wale wazee wawili waliambiwa waweke pesa zao. Walikuwa wameshindwa.

Tom na Betty walitoka hapo kwa huzuni wakilia. Walienda na kukaa karibu na wale watoto waliokuwa wakilala karibu na Irene. "Tafadhali, chukua watoto!" Betty aliomba, huku akilia. "Tutakupatia chochote tulichonacho iwapo utawachukua watoto."

Vernon alikuwa akiegemea upande wa Irene, na akasikia waliokuwa wakisema. Alitikisa kichwa la, akiashiria kwa mkono wake kwamba hakuna nafasi. Alimuashiria Irene kuwachana na mwanamke huyo.

"Bwana asfiwe!" alinong'oneza, kwa kuchochea alipomkaribia. "Alikubali Rolex yangu. Irene,waweza kusongesha gari hapa ili tujaze mafuta?"

"Twaweza kufinyilia watoto ndani," Irene aliomba. "Mimi na Raymie tutawatunza."

"Tutaweka wapi sanduku? au chupa za maji?" Jamii ya Billing ilikuwa imepakia kiti cha nyuma kwa vyakula, nguo na maji kabla ya kumchukua Irene karibu na Vilima vyaProspect. " Siwezi kukubali hayo," vernon alisema.

"Lakini ni nguo na chakula!" akashangaa Irene. "Twaongea kuhusu watoto wawili"

"Dada Mwenyezi Mungu anajua anachofanya. Mshukuru kwa yale ambayo ametutendea. Atawafungulia njia halikadhalika.Iwapo ni kwa mapenzi yake. Muamini Mungu dada. Ametuleta umbali huu."

Irene alitembea polepole hadi kwenye gari. Amini Mungu? alijiuliza . Walikuwa wamemuamini Mungu ili kuepuka janga; kwamba Yesu aliwaambia waende Montana. Na sasa alipaswa kuamini kwamba watoto wawili watatunzwa bila kujitolea kwa Vernon Billings. au, kwa upande wake.

Jee ni Mungu ndiye aliyeambiwa amuamini? Au Vernon Billings alikuwa kibadala cha Mungu? Aliwacha mtoto wake wa kike, kushiriki katika kuteka nyara, sasa kuwashinda wakongwe wawili na watoto wawili wadogo katika juhudi zao za kuishi, kwa sababu Vernon Billings alisema ni uwezo wa Mungu.

Irene alisukuma gari karibu na lile lililokuwa na mafuta. Wakati yule mtu wa galoni 44 alipoanza kuweka mafuta kwenyw gari la Vernon, alitamani kwamba Rayford angalikuwa hapo ili kumsaidia katika kutatua na kufanya uamuzi. Katika maisha yake alikuwa amefahamu Mwenyezi Mungu kupitia kwa watu wengine. Lakini sasa alipaswa kufanya uamuzi wa maana maishani mwake. Tayari alikuwa akishurutishwa kufanya uamuzi pasipokuegemea mtu. alijaribu kuomba, lakini alikosa imani.

Irene alingojea katika kiti cha dereva, huku yule dalali alipindua pipa ili kutoa mafuta ya mwisho. Alipomaliza, tayari alikuwa amefanya uamuzi. Alimuashiria kasisi Billings kuja.

"Vernon," alianza, kwa kumuita jina lake la kwanza kwa mara ya kwanza. "Nataka uwalete hapa wale wakongwe. Nataka kuongea nao." Kulikuwa na shtaka ndani ya sauti yake, jambo lililomshangaza Irene na vilevile Vernon Billings.

"Ni bora nisiseme kitu." Mtumishi wa Mungu alianza.

"Sitaki maoni yako. Nilisema uwalete hapa!" alisema. "Amsha Reymie na umlete vilevile". Vernon aligeuka kwa mshangao na kutii amri. Alikuwa na mshangao kutokana na uamuzi wake, na pia kutekeleza mbele ya mtu aliyemtolea uamuzi hapo awali. Ilikuwa inatisha lakini pia jambo la kusisimua.

Wakati Vernon alirejea, alikuwa pamoja na mkewe. "Ingia ndani ya gari, Reymie," Irene alisema. Raymie alipanda nyuma, huku wengine wakijikusanya kando ya mlango wa dereva. Aliongea ili wote wamsikize, lakini sio kwa sauti ambayo wanahiji wengine wangalisikia.

"Kuna mabadiliko ya mpango. Tunaelekea Kaskazini", alisema. "Hatuendi Montana. Iwapo utahitaji kuelekea Canada basi jiunge nasi."

"Hapana, usiseme hayo dada Strait," Mchungaji billings aliteta huku akisonga karibu na gari. "Karibu tunakaribia sehemu hiyo. Twaweza kuwachukua watoto iwapo utataka."

Punde tuu aliona mtutu wa bastola yake ukimuelekea kutoka dirishani.

"Dada Strait! Unafanya nini? Weka hiyo chini!"

Bang! Risasi lilifiatuka. Lilipitia juu ya kichwa cha Vernon. Wanahiji wengine waligeuka na kuangalia, huku wakifikiria kwamba gari limeungua.

"Nimekuonya kwa uzito, Vernon!" Irene alisema. "Nina jamii huko illinois, nahitaji kuwatafuta. Amerika imearibiwa, kwa yoyote sitaki kujua. Lakini siwezi kubadili kwa kufikiria hivi.

"Sasa nitauliza mara ya mwisho: Nani anayetaka tuende Canada pamoja?" Tom na Betty walitazamana. Kuangalia kwao kulidhihirisha kwamba imani yao kuelekea Montana ilikuwa imedidimia. Walitazama nyuma upande wa Irene na kuinua mikono yao.

"Leteni watoto," Irene alisema. Tutajazana lakini tutasaidiana. Je, wewe Vernon? waweza kutufuata kama utapenda."

Vernon Billings alikuwa na maumivu ya mwili na roho. kijasho kilimtoka na huku homa ikimpata. Alikuwa amesafiri kwa muda mrefu. Fahari yake na imani ya dini haingebadilisha uamuzi wake. Kweli au si kweli, alikuwa tayari kufa ili kutetea uamuzi wake. Alitikisa kichwa chake kisha kuenda kando.

Irene alimtazama Elaine, "Na wewe?"

"Uamuzi wangu ni sawa na ule wa Vern," alisema, akisonga karibu na mumewe ili kumliwaza na kumtuliza.

"Ninaelewa," Irene alisema, huku akijituliza kwa muda. "Ninawapenda nyinyi. wote".

Bibi wa mchungaji alirudisha ujumbe aliotoa Irene kuhusu upendo, kisha Tom White akapata ruhusa kutoka kwa Irene kabla ya kuwafikia Vernon na Elaine.

Aliwapatia funguo za gari lake na pesa huku Betty akiwapandisha watoto kwenye gari.

"Gari langu liko pale" Tom alisema huku akionyesha upande kulipokuwa na gari aina ya Ford la rangi ya kijani. "Garihilo halina chochote, lakini mwaweza kutoka hapa na hii." Alidhamiria kitita cha pesa.

Tom aliporejelea Irene na kujiunga na Raymie na mtoto mmoja katika kiti cha nyuma. Betty alimshikilia mtoto mmoja kwenye kiti cha mbele pamoja na Irene. Katika kiti cha nyuma kulikuweko pia visanduku viwili na kufanya msongamano.

Irene alianzisha gari na kuwapungia mchungaji na mkewe, na kisha kuingia kwa kasi kwenye barabara kuu.

"Mama, tumefinyana hapa nyuma," Raymie alilalamika.

Irene aliitikia kwa upole huku akiendesha gari, huku akisikiliza kwa makini. "Nitasema mara moja tuu, Reymie. Iwapo mmoja kati yenu haridhishwi na hali hii, uliza tuu na nitakushukisha. Samahani sana Raymie sijawai kukufundisha adabu njema. Hizi ni nyakati za dhiki, jaribu kuerevuka na kuelewa mara moja. Ni wakati uwache kulalamika na kumshukuru Mungu kwamba ungali hai, na vilevile tumepata uwezo wa kuondoka mahali hapo. Je, wanielewa?"

"Ndio, mama," Raymie alisema. Tom na Betty pia walinong'onea kukiri masharti hayo.

Walienda kwa kimya Walipokuwa wakienda kila mmoja wao aliomba maombi kwa njia ya kipekee.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Kitu muhimu ambacho Wakristo wapasa kuelewa ili kuepuka majaribio na kujitayarisha kuyakabili, ni jinsi ya kutii na kufuata Sauti ya mwenyezi mungu. Inaanzia na kufikiria na kujali ndani ya roho yako. Ulimwengu wa sasa umekaidi haya, hivyo basi kukosa kutii maadili ya Mwenyezi Mungu.

Utiifu kwa Mwenyezi Mungu umegeuka kuwa kuabudu na kutii binadamu wenzao.watu walio kwenye mamlaka, wazazi askari, waalimu na askari. Shida ya Irene sio kwamba alimtii Vernon Billings, au yale aliyofanya Vernon hayakuwa mema. (Hata hivyo Irene alitumia bunduki hatimaye!) Shida yake ni kwamba alikosa kuuliza Mwenyezi Mungu jambo la kufanya, au alidhania kwamba mapenzi ya Mungu sharti yadhihirike kupitia kwa mchungaji wake. lazima awachane na mchungaji wake ili aweze kukua kiroho.

Jamii ya dini na madhehebu hufundisha kuhusu kutii dini au dhehebu ni hakikisho la uokovu, dhana hii ni kinyume cha ukweli. Wokovu ni pale tunapopata na kuamini Mwenyezi Mungu pasipo kusujudu dini au madhehebu.

Soma Luka 17:31-37. Wanafunzi walitaka kujua mahali pa kuenda siku ya kiama, Yesu aliwajibu kwa mafumbo yaliyoeleza kwamba lazima tuwe kama ndege, tayari kufuata maagizo ya Roho mtakatifu ili kutuongoza kila dakika wapi tunapoelekea na lini.

 

 

6. Kuhesabu Gharama

 

Rayford aliangalia juu ya gari la Leyland Dal. Lilikuwa limejaa, Watu wanne kwenye sebule, lakini sio msongamano kama alivyotarajia. Daftari ilijumuisha vifaa vya mbao. Kulikuwa na mahali pa kila mmoja kulala na pia kuketi. Kila kitu kilikuwa kimewekwa vyema. Kusonga au kupita katika sehemu moja hadi nyingine ndani ya gari hilo haikuwa rahisi, hasa iwapo mmoja alikuwa akipika au kuosha vyombo katika eneo ndogo la jikoni.

Karibu na Rayford, upande wa nyuma wa gari hili, alikuwa ameketi kijana mwenye umri wa chini kwenye kundi hilo aliye na miaka 24 kwa jina la Martin. Jamii ya Martin ilitoka nchi ya Czech. Upande mwingine kinyume na Rayford, kulikuwepo Reinhard na Francisco. Reinhard alikuwa na miaka 32, ilihali Fransisco alikuwa na umri wa miaka 28. Mama ya Frans alitoka Argentina. Wote watatu hawakuwa wamefuzu taaluma yoyote licha ya kuelewa lugha nyingi lwa ufasaha. Kwa pamoja walikuwa wametafsiri Kuangamia kwa amerika kwa lugha ya Kifaransa, Kijerumani, Kiispania, Czech, Kirusi na hata Kipolishi.

"Je, kwa wiki moja mnapata vingapi," Rayford aliuliza, huku ameshika nakala moja ya kitabu kilichomvutia.

"Maelfu katika wiki nzuri", Martin alijibu. Martin alikuwa mkuu wa takrimu. Yeye ndiye aliyetayarisha makadirio ya kifedha kwaniaba ya kundi hilo.

"Hiyo ni 1000,000 kwa mwaka," Rayford alisema.

"Mwaka bora," Martin alimjulisha.

"Chochote. Jambo ni hata mwaka mbaya, mtapata wanachama wengine. mbona nyinyi ni watatu?"

"Sababu mbili," Fransisco alijibu, aliyeonekana mwenye uwezo na mali kuliko wale mamishionari wengine wawili. Mikono yake ilichezacheza, na kutingisha kichwa kana kwamba kichwa kilivuta kamba mkononi. Kutikisa kwa kichwa ilikuwa ishara ya kutoka kwa wazo fulani hadi lingine.

"Tunayo hubiri.hasa, watu hawasikii. Wajua, wanataka wahubiri kuwabembeeeleza." Alikariri na kulivuta neno kuwabembeleza. "Tunaongea juu ya kifo hapa. kutuandama sote. Namaanisha kutoa kila kitu kwa Mungu! Nani anataka kusikia hayo?"

"Sababu gani nyingine inayowafanya watu wasijiunge nanyi?" Rayford aliuliza.

Reinhard alijibu. "Twatumai kwamba Mungu amatuficha chini ya waumini wa hakika. Hao pia wanajificha tusiwaone. Siku moja tutakuja pamoja. Kwa sasa, tunajaribiwa kuona kama tutadanganya au kubadili ujumbe wetu."

"Mmoja akipanda mmea, mwingine hunyunyiza." Fransisco alirudia. "Mavuno yatawadia. Hakuna wasiwasi. Kwa sasa wanasoma. Wanafikiria. Na lo, wanazungumza juu ya hayo. Watu hutueleza.kil siku!"

Rayford alitamani mawazo ya watatu hawa; lakini hakuamini kwamba wengine hawakujiunga nao licha ya utabiri wao kuhusu Amerika kuonekana na kutimia. Na akasema hivyo.

"Kwa haraka watu husahau," Reinhard alieleza. Wanapuuza pia. Ikiwa wanasema kwamba kitabu chetu kiliandikwa baada ya shambulio."

"Lakini ndani ya mioyo yao wanajua!" Fransisco alieleza. "Wanajua basi! Ukweli umo kwenye vitabu, kupita kama bomu lililotunguliwa. Siku moja uwazi utajitokeza.Na kisha. Ka-PWA!" Alipiga makofi kutoa hiyo sauti na kisha kubeba mkono juu ya hewa kama roketi. Nyuso zote tatu ziliangalia kwa kukubali yale aliyoyasema Fransisco.

"Hatuongezeki kwa idadi; lakini ukweli unadhihirika," Kufanikiwa mbele ya Mungu ni bora kuliko kufanikiwa tu."

"Lazima uelewe," aliendelea Reinhard, "Sisi huamini tunapozungumzia juu ya mbingu na Mungu, na kuhusu kurudi kwa Yesu. Imani hii hubadili fikira zetu kuhusu vitu vingine. Tunaishi katika ulimwengu mpya. milele. Imani yetu sio ile imani ya kanisa."

Hayo ni mawazo makuu! Rayford hakuamini kwamba watu wa ajabu watatu wanaoishi kwa umasikini wangali mshawishi. Ili hali walikuwa wakifanya hivyo. Ukweli ni kwamba hangaliwapatia nafasi ya pili pasipo shambulio la Amerika. Gharama gani hii juu ya Mwenyezi Mungu kwake kusikiza kwa makini! Watu wengi kote ulimwenguni walikuwa wakitafakari kuhusu uchumi na wala sio hali ya kiroho inavyozidi kudidimia nchini Amerika.

Rayford alibakia akiongea kwa muda. Aliwatumbuiza kwa chakula moto ndani ya mkahawa wa kituo cha Heston. Kwa wakati huo alifahamu kwamba watatu hao waliegeza gari lao usiku katika vituo vya kurekebisha magari, kutokana na hali isiyo ya wasiwasi au hata kushukiwa hata kwa saa 24 kuliko kuegesha kando ya barabara. Kuegesha katika sehemu kama hizi ilikuwa ni hakikisho la kupata vyumba. Wakati wa mchana waliuza makala yao kwenye vituo vya biashara, kama walivyofanya katika barabara ya Hounslow hapo awali.

"Hatuishi mahali pamoja kwa siku mbili mfululizo," Martin alieleza. "Sio rahisi kugundua kwamba tuko hapo."

Siku iliyofuatia, Jumapili, Jesans walikutana na Rayford katika ukumbi wa Ruislip, siku yao ya kupumzika. Rayford alijuunga nao kisha kutoa mafundisho ya Bibilia na maankuli ya mchana yaliyotayarishwa na Francisco.

"Niwache kazi yangu ili niwe mkristo kamili?" aliuliza walipokuwa wanakula.

"Unachotakiwa kufanya ni kumuamini Yesu," Reinhard alisema.

"Lakini uliniambia kwamba ni kutoa yote uliyonayo, na kumtumikia muda wote!" Rayford alikuwa akirejelea mafundisho ya mlango wa kumi nanne katika kitabu cha Luka.

"Kwa hivyo fanya alivyosema," Reinhard alijibu. "Lakini usifanye tu kwasababu alisema."

"Lakini nini kuhusu familia yangu?"

"Nini kuwahusu?" Reinhard aliuliza kwa upole akikodoa macho kuonyesha hali ya kusisitiza.

"Siwezi kuwaacha"

"Kwa hivyo kuja pamoja nao."

"Unajua siwezi kufanya hivyo. Chloe ameshikwa kule Chicago, na sijui mahali alipo Irene na Raymie. Wanaweza kuwa wameuawa." Reinhard hakupinga hayo, kwani jesans walimpa muda na kumsikiza Rayford na vilevile kumhadithia kuwahusu. lakini alitaka kumuonyesha Rayford jinsi asivyo na uwezo.

Kwa mara nyingine Furaha ya Fransisco ilizidi ile ya Reinhard. Ona? unashikilia kitu usicho nacho!" alisema. "Wachilia! ukiwachilia Mungu atakuonyesha cha kufanya. Lakini huwezi kufikiria hayo kabla ya kuwachilia kwanza".

Reinhard kwa siri alimuashiria Fransisco kuondoka, na kuwacha kundi katika hali mbaya ya kimya kwa muda. Walikula bila kuongea huku Rayford akiwaza sana ndani ya akili yake. Fikira zake hazikuhusu wageni hawa. Fikira yake ilikuwa kuhusu Muumba wake.

Iwapo Mungu wetu ni Mwaminifu, aliwaza, basi Mungu anahaki ya kuwaamuru watu kuwacha familia zao, kazi, utajiri wao ili kudhihirisha imani yao kwake. Lazima ilikuwa imani kama hiyo iliyotoa uhuru kwa Reinhard, Fransisco na Martin kufanya yale waliyokuwa wakifanya. Idadi yao haitawai kuongezeka iwapo wenzake hawangali fanya uamuzi kama wake. Rayford aliona kwamba mazungumzo ya imani kuhusu Yesu yaliyopuuzwa na wafaasi sio imani tena. Lakini angalifanya nini kuhusu jambo hilo?

Tukio la hali lilikuwa limechukua nyumba na jamii yake. Kilichobaki ni kazi yake. Hata ingawa kazi ilikuwa kwa minajili ya jamii yake, na wazo la kujipatia nyumba mpya siku moja.

"Ewe Mwenyezi Mungu," aliomba. "Siwezi kumuacha Chloe. Yeye ananitegemea."

"Mungu anajua kilicho na muhimu kwako," Reinhard alisema kwa lahaja yake, kama kwamba alikuwa akisoma akili ya Rayford. "Ni bora kumchukulia kwa fikira nzito badala ya kupuuza maneno yake."

Jasho lilimtiririka Rayford. Alikuwa amesimama kando ya ukingo wa jukwa la maamuzi ya mwenyezi Mungu kama alivyofahamu. Aliendelea kuomba kwa kisiri. "Ewe Mwenyezi Mungu nisaidie. Sitaki kufanya jambo la kishenzi. Kuna mengi mbele yangu. Na je, kuhusu Chloe?"

Reinhard alinena tena kama kwamba anasoma fikira zake. "Hatuna uwezo lakini tunafikiria tunao," alisema. "Kwa dakika Mungu anaweza kuchukua. Na kwa dakika anaweza kupeana. Iwapo unatumai mema basi wachilia! Wachia Mwenyezi Mungu atoeuamuzi kuhusu yaliyo bora kwako na kwa watu uwapendao."

Akili nyepesi ya Rayford Strait iliweza kukadiri ukweli wa yale yaliyosemwa na Reinhard. Alikuwa ameeleza utawala wa Canada yale aliyofahamu kuhusu familia yake. Licha ya hayo hakuwa na uwezo. Mambo muhimu yalikuwa madaraka, heshima na pesa pamoja na uhuru wa kuenda Uingereza na Canada kwa ajili ya kazi yake. Mengi ya kuacha, hata hivyo ni bure ikiwa ni mipango ya Maulana. Matukio ya siku chache zilizopita yalikuwa yamemshtua. kumuezesha kuona jinsi maisha yalivyo ya kutisha na vile ndoto zilivyo tamu. Iwapo angali sema laa kwa Maulana, ni sawa na kusema hapana kwa maisha ya milele. Rayford alikuwa ameonyeshwa ukweli wa kiroho na watu hawa, kwa hali ambayo alikuwa hajapata kuona. lilikuwa jukumu lake kutekeleza.

Hata ingawa yote hayo yalitokea baada ya shambulizi la mabomu, Rayford hakuwa amelia mara moja. Labda ilikuwa kujinyima, au kujihusisha kwa uangalifu na matukio yaliyokuwa yakitukia. Lakini machozi yalimlengalenga, ukweli wa Mungu katika maisha yake ulipomjia. Alijikaza kufuata na kutekeleza aliyofikiria kwenye akili.

Fikira na mawazo yalimpelekea kukata tamaa ya kuwacha kazi. Je atoe ilani? Akose tu kufika kazini? Aligundua kwamba alikuwa ametoaa uamuzi kufanya. Yote ili kumfuata Mwenyezi Mungu. Swali kuu ni vipi. na lini.

Rayford aliinua kichwa chake na kutabasamu, huku machozi ya furaha yakimtoka. Wenzake walielewa maana ya machozi hayo, na hasa tabasamu iliyofuatia. Fransisco aliyeketi ule upande mwingine wa Rayford, aliruka na kumsalimia. Salamu hizo zilipelekea kukumbatiana. Martin na Rainhard walingojea zamu yao kwa furaha na machozi.

Rayford alipiga simu kazini siku ya Jumatatu ili kuwaarifu. Alijulishwa kwamba Jeshi la Uingereza halingalimruhusu kuwacha kazi. Ni miezi mingi kabla ya mashirika ya ndege kurejelea safari zao, kwa sasa kila rubani na ndege walitumiwa kwa kikamilifu katika juhudi za kunusuru.

Wote wanne walijadili swala hilo na kuamua kwamba hali ya Rayford ilikuwa sawa na utumwa. hasa kwa wakati. Alikuwa ameapa kujiuzulu kwa ajili ya kazi ya Mungu, na huku hali ya wakati imemrejeshea kazi. Angalingojea hadi pale anaporuhusiwa kujiuzulu, kwa sasa angetumia uwezo wake kuomba msaada kwa ajili ya jamii yake. Akiwa London ataishi na ndugu zake wa kikristo na kuwasaidia kueneza injili kwa kuuza majarida kando ya njia.

Majuma machache yajayo, katikati ya fikira zao kuhusushida ya Amerika, Wahudumu wa Pan-Con waliona ubadilifu wa Rayford Strait. Rayford Strait alikuwa ameokoka na kujiunga na wafaasi wa Kristo. Kujitolea mhanga katikaToronto kulikuwa kwa haki, lakini London angalikutana na wanaume walio kwenye gari aina ya Daf katika uwanja wa ndege, na kurudi kwa wakati kuchukua ndege. Hali yake ya kawaida ilikuwa imempotea, na kwamba uvumi ulienea kwamba yeye anarandaranda mitaani huku akiomba.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

G.K Chesterton aliwai sema, "Sio kwamba Ukristo umejaribiwa na kupatikana umeshindika. Ni ile tuu watu walijua sio rahisi na kutojaribu."

Shida katika Kanisa la kisasa ni kwamba watu wachache wamekuwa wakijaribu (lakini changamoto kwa wengi) kufuata sheria za Kristo kwa wafuasi wake. Kuna wahubiri wengi walio tayari kutueleza yale tunayotaka kusikia, yale tusiyochukua muda kusikiza kutoka kwa Bwana wetu. Iwapo maana ya Ukristo ni kumfuata Kristo, basi hatuwezi kufurahi kusema kwamba Kanisa ni la kikristo, licha ya kujihusisha na mengi kuhusu dini au dhehebu hili.

Chukua muda kupitia katika sura ya kumi na nne ya kitabu cha Luka mstari wa 25 hadi 35. Labda Yesu hakutaka tuelewe sura hiyo kwa juu tu. na labda pia alinuia hivyo. Mengi yako juu yetu lazima tuombe kwa wingi na kwa kujitolea kabla ya kutupilia mbali sura hizi.

Tunapowadia katika kutambua miujiza ya maisha yamilele na yale maisha yanayowakilishwa, utapata hakikisho kwamba tutadanganya kuhusu maagizo hayo na pia kupata kuyajua.

Siku moja Mwenyezi Mungu atakuuliza kulaza maisha yako kwake. Je, ni gharama kwako kutoa familia yako kwake, kazi, na utajiri iwapo anauliza hayo sasa?

 

 

7. Wakimbizi

 

Licha ya uchovu na kisunzi na shida nyingine za safari, Irene Straight aliweza kuendesha kwa muda bora kuelekea kaskazini alipokuwa amewacha wanakambi wengine Kaskazini mwa Dakota. Aliendesha mbio usiku kucha na kuwasili mchana siku ya Jumamosi.

Mamlaka ya nchi ya Canada ilikuwa ikichukua maelezo kutoka kwa wakimbizi waliokuwa wakija na kuwaelekeza kwenye kambi. Tom na Betty na wajukuu walidhibitishwa kuhitaji matibabu ya dharura kuliko Irene na Reymie, hivyo basi waliingia kwenye basi na kuelekea Regina ili kupata kutunzwa vyema.

Usafiri ndani ya nchi uliwekewa vikwazo kote nchini Canada. Irene hakuwa na fedha, ombi lake kuenda Toronto lilikataliwa. Kulingana na mamlaka, Toronto ilikuwa imepata wakimbizi wengi kupita kiasi. Irene na Reymie walielekezwa katika kampi iliyokuwa katika barabara kuu ya kuelekeaRegina na Winnipeg. (Waliweza kuwacha Lincoln kwenye mpaka). Kampi hii ilikuwa kati ya zile nyingi zilizokuwa zikitengwa kutoka kwa mashamba kila mahali kusini mwa Canada.

Irene na Reymie walipaswa kungojea hapo hadi tuwe na utulivu Toronto, au hadi watakapochukuliwa kwa ndege nje ya Saskatchewan. Wote walikuwa wakipoteza nywele na kukosa maji kutokana na kutapika, lakini hawakua wagonjwa kama watu wengi kwenye kambi. Kambi ya wakimbizi ilikuwa na maelfu ya mahema ya futi kumi na mbili mraba, kila hema likiwa na watu wanane. Kila baada ya mahema manne kulikuwa na chumba cha kuogea. Ndoo kwenye vyumba ilitumiwa kama choo wakati vyumba hivyo vilikuwa vikitumiwa kwa wingi au wakati wa hali mbaya ya hewa. Eneo la shamba palikuwa mahali pa kuchukiza kutokana kiasi kikubwa cha mvua ya hapo awali na pia kutokana na msongamano wa watu wanaotembea kupitia hapo.

Wakimbizi walishahuriwa kubaki ndani ya kambi kuzuia maafa. Wahudumu wasio na ujuzi walileta madawa mara mbili kwa siku. Dawa hizo zilikuwa pamoja na zile za kisunzi, kuendesha. Halikadhalika maji na chakula. Visa vya dharura vya magonjwa ndivyo vilivyoripotiwa kwa wauguzi waliohitimu. Katika eneo lililotumiwa kama zahanati, tulikuwa na madaktari wawili na wauguzi wachache. Maisha yalikuwa magumu kwenye kambi hiyo licha ya uvumi kwamba hiyo ndiyo ilikuwa kambi nzuri kushinda nyingine yeyote.

Shirika la ndege la Pan-continental lilijulishwa kuhusu hali ya Reymie na Irene na Pan-con kupitisha ujumbe kupitia kwa Rayford. Jamii hiyo haikuwa na la kufanya ila kungojearuhusa ya kwenda kuungana na jamii.

Kwa sasa Irene na Reymie walisadiki kwamba wanapata chakula bora na maji safi, na pia kambi bora iliyo na mahali pa kupumzikia, kulala na kuwa na matumaini. Hapakuwepo na uwezekano waRayford kuwasiliana nao moja kwa moja, na kwamba simu za dharura za kuenda nje ndizo zilizokubaliwa ndani ya kambi.

Kwa wakati fulani, Reymie alikuwa akifikiri kuhusu hali ya maisha. Maisha yalikuwa mabaya hata kushinda gereza au korokoro mbovu Kaskazini mwa Amerika. Lakini kwwa muda wa wiki mbili alikuwa mgonjwa kufanya lolote ila kuguna kwa maumivu. Hadi tu alipopata nguvu ndipo alipoanza kulalamika. Irene alikimia na kunyamaza kuhusu shida zake, huku akimjulisha mara kwa mara jinsi walivyonusurika. Lakini Reymie alikuwa akijaribu kuvunja tabia za kitambo. Ilikuwa kama kwamba roho yake ilikuwa ikingoja Irene kupata nguvu na busara ya kuimiliki. Ni wazi kwamba katika ulimwengu yale yanayopuuzwa ndio husababisha maafa. Kwa jumla, Raymie alilazimishwa kukua katika muda mfupi, na kwa haraka alikuwa akijaribu kuishi katika hali hiyo mpya ya kuwa mtu mzima mwenye utu-bora.

Jamii ya watu wanane katika kila hema waliongea na kufanya kazi ndogondogo kwa wale waliokuwa na nguvu. Mengi ya mazungumzo yalikuwa kuhusu kile walichofikiria juu ya yale yaliyotokea, na muelekeo na madhara kwa jamii zao. Kila mmoja alikuwa na huzuni na maombolezi kwa kupoteza rafiki mpendwa au jamaa yake, hata hivyo wengi walidhani kwamba baadhi ya jamaa zao walinusurika shambulizi

Mtandao wa habari na mawasiliano katika U.S. ulikuwa umeharibiwa muda mfupi baada ya shambulizi.

Licha ya kukosa magazeti katika kambi, wahudumu fulani walipata habari au ujumbe kutoka nyumbani, na kuwaarifu wakimbizi waliporejea kwenye kambi. Kutoka hapo ujumbe wa mdomo ulienea kwa haraka.

Wakaazi walijua kwamba Umoja wa Mataifa ulikuwa umeanda jinsi ya kutunza misaada. Katika majuma machache yajayo, manusura wa Amerika wataanza kusambazwa kote ulimwenguni kutoka kambi za Canada na Mexico na sehemu za Amerika. mahali pa kuchukuliwa kwa ndege katika sehemu zilizo na uwezo wa ndege kutua.

Hali ya anga ilikuwa shuari, kwa upepo wenye utaratibu uliopita juu ya Atlantic. Upepo ulisukumwa kusini mwa nje ya Canada baada ya shambulizi. Hata hivyo viwango vya miali ya jua vilikuwa juu hasa kusini mwa Canada, juu kuliko ilivyotarajiwa. watu wa Canada walihimizwa kubakia nyumbani. Ulimwengu kwa jumla na visiwa vya Caribbean na sehemu za Mexico hazikuadhiriwa kwa miali hiyo.

Nchi ya Urusi ilichukulia hali ya vita hivi kama kwamba havikutokea. Baada ya wanamgambo wake kulipua makombora kwenye kambi za kijeshi na sehemu nyingine muhimu za umeme na mawasiliano, walirudi kwenye maskani yao. Kutokea hapo Russia ilitoa misaada kwa manusura kama taifa lengine lolote.

US. na Uingereza walikuwa wametimuliwa kutoka kwa umoja wa mataifa siku chache baada ya shambulizi. Amerika ilitimuliwa kwa kuangamizwa ilihali maelezo kuhusu Uingereza kutimuliwa hayakutolewa. Licha ya malalamishi kutoka Uingereza, hatukuwa na pingamizi kutoka kwa jamii nyingine za umoja huu. Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Xu Dangchao, kwa kuungwa mkono na Russia na China katibu huyu aliweza kusuluhisha kwa wepesi. Kutimuliwa kutoka kwa uanachama haukufuata na kuwekewa vikwazo. Hata hivyo watu wa Uingereza walipuuza na kuendelea kusaidia Amerka. Uingereza haikutaka kubishana kutokana na tofauti ya mawazo.

Kupotea kwa nafasi ya kibiashara na Amerika ilikuwa tisho kwa mataifa mengi maskini, lakini Umoja wa Mataifa ulianzisha juhudi za kutaka kuchukua sehemu zilizomilikiwa na Amerika na kuanza kutayarisha mashamba ili kukidhi uhaba wa chakula. Katibu wa Umaja wa Mataifa bwana Dangchao aliahidi kwamba atasaidia mataifa yanayostawi, na ajabu ni kwamba Banki kuu duniani iliunga mkono azimio hilo.

Mkutano mkuu ulipangiwa kufanyika kuhusu hali ya uchumi wa dunia. Mojawapo ya maswala ya kujadiliwa ilikuwa ni matumizi ya sarafu moja.

Jambo moja au mradi wa umoja wa mataifa ambalo halikushughulikiwa kama mambo ya fedha na siasa ilikuwa jumuia ya madhehebu. Dunia nzima watu walitaka hakikisho kwamba janga la USA lisirudiwe tena. Wakuu wa madhehebu walishanga kuona tofauti zilizowagawanya hapo awali zikitokea. Hao pia walitaka kujumuishwa katika kuleta amani duniani na umoja.Umoja baina yao na pia umoja wa kitaifa. Wakati wa dhiki au shida, watu wengi hukimbilia vituo vya dini kwa msaada: hivyo basi ni muhimu kwa serikali, kanisa, sinagoji na misikiti kutoa ishara ya umoja na matumai.

Hatukua na ujumbe au risala kutoka kwa rais Fitzhug, ambaye kwamba yeye na familia yake pamoja na wasaidizi wake walikuwa wametekwa nyara ndani ya Ikulu ya White House kutokana na shambulio. Matumaini yao kama manusura yalizidi kudidimia, licha ya kuwepo vyumba na njia za kuepukia mikasa. Tulikuwa na njia ya kuapisha rais mwengine. Hata hivyo wale ambao walihitimu kama vile makamu wa rais na wagombeaji wengine walikuwa wametoweka au kufa, na pia na idadi kubwa ya maseneta na wajumbe wa bunge la chini. Wachache waliokuwa hai walikuwa wakimbizi. Kwa hakika, Amerika ilikuwa imeangamizwa kama taifa huru.

Taifa hili lilikuwa imara kutokana na kuunga mkono Israeli. Taifa hilo ndogo la Israeli lililozungukwa na mataifa ya kiarabu lilikuwa na wasiwasi kutokana na tukio hili. Lakini Dangchao alishangaza ulimwengu na kupata sifa na heshima kwa kuendesha mazungumzo ya amani kati ya Israeli na nchi za Kiarabu. Iliaminika kwamba uwezo wa wayahudi katika Banki ya Dunia ndio chanzo cha kufaulu kwa Dangchao. Alipata mabilioni ya dola kutoka kwa Banki ya dunia ili kusaidia mataifa maskini.

Jambo la kutisha kwa mamilioni ya Waamerika walikuwa wakijaribu kuepuka kifo na janga lililokumba taifa hili. Maelfu ya watu waliendelea kufa kila siku kutokana na yale majeraha na shida nyinginezo kutokana na mlipuko. Wengi walikufa kwa kukosa madawa, aidha waliwachwa mahali hadi pale watakapo kata roho. Wale manusura waliobebwa kwa gari walikufa wangali njiani au hata kwa kufikishwa hospitalini au kwenye kambi. Mazishi halikuwa jambo la kawaida. Kuchoma maiti ilikuwa rahisi na haraka, na kwa kiasi kikubwa maiti iliwachwa kuoza, na magonjwa kusambaa.

Kwa watu kama Chloe, waliokuwa wakingoja msaada kuwafikia, hatari ya kupata kipindupindu iliongezeka.

 

 

Zion Ben-Jonah aandika

 

Alama mbili zatumiwa kuashiria Amerika katika unabii wa Bibilia. Kahaba aliyejulikana kama Babeli, na mabawa ya mwewe na kiwiliwili cha simba (Simba akiwa ni Uingereza.) (Tazama maelezo baada ya sura ya 2)

Kitabu cha Danieli 7:, mabawa ya mwewe yamenyanyuliwa, na simba (yaani Uingereza) sio "jitu" (au babe la dunia) hatimaye. Katika Ufunuo wa Yohana 17:16-18, na Ufunuo wa Yohana 18 kwa jumla, tunasoma juu ya kuanguka kwa Babeli na jinsi kulivyoadhiri wafalme, mabepari na manuari duniani.

Kumbuka kwamba neno "Babeli" halimaanishi tu Amerika. Ni ishara ya utawala wote wa binadamu. Hivyo basi jina litapitishwa kwa taifa lenye uwezo mkubwa wa kifedha katika mpangilio mpya.

Kuibuka kwa dini au dhehebu moja duniani hakuwezi kusaidiwa na Umoja wa Mataifa. mazungumuzo kuhusu dhehebu la dunia yamekuwa yakiendelea; lakini shida na majanga hufanya watu kufikiria juu ya jambo hili.

Ubeberu na ubabe wa Amerika pamoja na Israeli huelezwa kwa wingi (hata kwenye kanisa), kwa kufahamu kwamba ni wateule wa mungu (Licha ya kukata na kumkana Mtume wa Mungu Yesu Kristo!). Hata hivyo, kivutia cha Israeli katika viwango vya serikali ni kupata uwezo wa kumiliki banki kuu ya dunia.

 

 

8. Kuungana

 

Chloe alifanya bidii kuhakikisha kwamba maisha yake katika vilima vya Prospect Height yalikuwa tulivu na salama. Alifungua simu kwa saa chache tu kila wiki--wakati ambao baba yake alitarajia kumpigia simu. Aliongeza kiasi cha maji yaliyomfikia kwa kugeuza mkondo wa mfereji wa choo katika vyumba vya juu. Iwapo yaliisha, basi ilimbidi atafute, ili apate maji na chakula kutoka kwa nyumba zilizokuwa karibu na zilizowachwa punde tu baada ya shambulizi. Alisonga kutoka kutoka kule chini hadi kwenye vyumba vya gorofa ya kwanza. Lakini alitumia choo katika chumba cha chini. Kwasababu hatukuwa na vifo katika mazingira yake, aliepuka janga la maambukizo ya magonjwa. Kwa jumla wiki yake ya mwisho katika eneo hilo ilikuwa ni raha.

Baada ya majuma matatu ya kutokea shambulizi, basi la kuokoa majeruhi lilikuja mbele ya nyumba hiyo na kumuomba Chloe iwapo ilikuwa bora kumsafirisha hadi kwenye feri itakayomchukua yeye pamoja na mamia ya manusura wengine hadi ziwa la Michigan kuelekea ukanda wa Elgin, magharibi mwa ziwa la Huron. Kutoka hapo walipelekwa kwa basi hadi Toronto.

Chloe alikuwa kwenye kambi kwa siku mbili kabla ya kupelekwa uwanja wa ndege. Alikuwa hajawasiliana na babake kwa siku tano, hatahivyo hakushtuka kwa kupata tiketi ya kuenda hadiLondon. Hakushanga vilevile kuona babake akimngojea kumlaki baada ya kupita mlango wa walinda usalama . hata hivyo alikuwa na hamaki kuu. Walisalimiana kwa furaha, na kusonga hatua ili kumuangalia kila mmoja kabla ya kukumbatiana tena. Shida na uchovu wa wiki zilizopita yalimfanya Chloe kutiririka na machozi. Lakini aliona babake akishikilia kitu.

"Jambo lolote kuhusu mama na Reymie?" aliuliza. "Wako salama," Rayford alisema. "Wangali Regina, lakini sio kwa muda mrefu. Nimewasilisha hati za usafiri ili wafike hapa Uingereza watakapowachiliwa."

"Mawazo ya Rayford yalikuwa mbali. "Chloe waweza kukaa chumba cha rubani nami leo?" aliuliza.

"Hiyo ni kejeli? Hakuna anayeweza kunizuia!" alisema kwa furaha.

Rayford aliongeza, "Nimetoa uamuzi fulani wa maana kuhusu kumtumikia Mungu. Tutajadili kuhusu hilo."

Chloe alikuwa ameomba kivyake, kwa hivyo angalikubali yote hayo kutoka kwa babake kuhusu kuenda kanisani. "Ninaelewa," alisema kwa kutabasamu wakielekea kwenye ndege.

"Kuna mengi juu yake zaidi ya vile unavyofikiria," alisema "Tutaongea juu ya hayo baada ya kupaa."

Ndani ya ndege Rayford aliangalia na kuchunguza kwa makini kuhusu vifaa vya usalama, mawasiliano (kutoka kwa waelekezi na abiria), na ndege zilizokuwa angani Lakini walipokuwa katika eneo la kupaa kwa kikamilifu na ishara ya mshipi wa kiti kuzimwa, Rayford alitoa usukani kwa msaidizi wake na kuelekea kiti cha muongozaji, mahali ambapo wangezungumuza na Chloe.

"Kuna mengi ninayotaka kusimulia," alianza.

"Jambo la kwanza, fahamu kwamba sina nyumba au chumba chochote kule London."

"Tutajaribu. Nitapata kazi," Chloe aliahidi.

Rayford alijaribu kumueleza kwa undani kuhusu azimio hilo.

"Hatuhitaji kazi," alisema "Hata nitawacha kazi hii ninayofanya hivi karibuni.ili kumtumikia Mwenyezi Mungu."

Chloe alikodoa macho. Kitu cha ajabu kitatukia.

"Uwache kazi?" aliuliza kwa mshangao. "Tutaishi jinsi gani? Haujapata mafunzo yoyote kama mhubiri." alilisema neno "mhubiri" kwa ushangao.

"Kwa sasa mimi ni mhubiri," Rayford alijibu

"Wapi? katika Kanisa gani?"

"Hakuna kanisa. Ninaongea tu na watu kuhusu Neno la Mungu. mitaani."

"Nini? wewe ni mhubiri wa mitaani?" Mambo haya yalionekana ya ajabu.

"La, mimi hugawa majarida kwa watu, na wakati mwingine maswali huzuka na kusababisha mazungumuzo."

Chloe aliona hayo kama haya na kejeli. Babake ---rubani aliyeheshimiwa--- kuonekana mitaani. Aliwaza na kufikiri jinsi atakavyo kuwa na umati mkubwa, na Bibilia mkononi. Lakini alificha mawazo yake.

"Haufai kuwacha kazi yako," alisema.

Na mshahara unaopata waweza kuajiri mtu wa kukufanyia kazi hiyo, na tutaweza kuunganisha jamii yetu tena."

"Chloe kipenzi," Rayford alianza. "Nipatie fursa nikueeze? Ni muhimu sana kwangu uelewe hasa kinachoendelea."

Chloe alitaka sana kupata maelezo. "Hasa," alisema kwa huruma. "Endelea mbele" aliketi ili kusikiza kwa makini

Rayford alianza kusimulia juu ya mazungumzo yake na Reinhard katika uwanja wa ndege, muda mfupi baada ya shambulizi. Alieleza jinsi alivyofikiria kwamba mafundisho ya dini kanisani hayakutosheleza na yalikuwa duni. Alikiri kwamba pia yeye aliepuka na kutoa muda usiotosha kwa kazi ya Mwenyezi Mungu.

"Wale jamaa katika gari lile walifanya nifahamu na kusoma yale aliyofundisha Yesu," alisema.

Chloe alikuwa alikuwa hajatilia maanani maelezo na mafunzo ya dini aliyofundishwa na mamake, hivyo basi Rayford alijua hangebishana naye au kuwaza kama angalifanya na Irene. Alipaswa kuanzia na maelezo ya kimsingi.

"Haiwezekani kwamba mambo uliyoyapitia wiki tatu zilizopita hayawezi kukufanya kufikiri juu ya Mungu," alisema kwa tabasamu.

Chloe alitingisha kichwa. Aliomba kila mara, hasa siku zile za kwanza katika chumba cha chini. Lakini maombi yalikuwa jambo la mwisho baada ya mengine yote kushindwa. Sio bora kumulimbikizia Mwenyezi Mungu mambo unayoweza kufanya mwenyewe.

"Ndio, hasa nimekuja kuona kwamba maisha yetu ni kati ya mpango. kama jaribio. ambapo Mwenyezi Mungu anatazama iwapo tutasisitiza kufanya kazi zetu wenyewe."

Rayford alionekana kama anayebadili kauli kwa muda. "Maombi yote katika dunia hayatatuzuia kuaga dunia. Ilihali mengi ya maombi huombwa hivyo. maombi ili tusiumie, tusife, au kusumbuka tu." Rayford alijiona kama asiyejieleza kwa kikamilifu.

"Ninalosema ni kwamba, iwapotutaomba, lazima tuombe kitu kingine isipokuwa ubinafsi."

Kulikuwa na kusitasha mazungumzo hayo mhudumu wa ndege alipokuja na kahawa. Chloe alikubali kuchukua kikombe na kuongeza sukari, lakini alisumbuka kwenye akili kilichokuwa kimetendeka ndani ya roho ya babake. Hangepata taswira hiyo kumuondokea kwamba Rayford anatembea mitaani akipaaza sauti kwa umati. Mbona alifikiria kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa njia kama hiyo? Hakuna anayewasikiza wahubiri wa mitaani! Iwapo babake alitaka kuhubiri, basi afanye hivyo kanisani. Alikuwa mtu hodari sana kuonekana akitenda mambo kama hayo mitaani. Je aliwacha kazi kwa kuchoshwa na mambo ya vita?

Chloe alitoka kwenye lindi la mawazo rayford alipoanza kuongea.

"Mpenzi, nitatoa chochote ili uweze kuona yale niliyoyaona. Lakini kwa usaidizi wako au bila, lazima nipitie katika mambo ninayoona na kuamini kwamba Mungu anataka ni fanye." hakuna jibu. Hivyo basi Rayford aliendelea.

"Hatukuumbwa kutafuta pesa. Tuliwekwa hapa duniani kumhudumia Mwenyezi Mungu. Unapokubali haya, utafahamu kwamba shida zote duniani zatokana na tamaa. Wiki mbili zilizopita sijafanya chochote, na ninajisikia mzima na bora kuliko wakati mwingine wowote."

 

"Hiyo ni rahisi kusema unapolipiwa ada ya hoteli na Pan-Con," Chloe aliteta. "Nani anayepokea malipo yako? Huyu mtu Reinhard? hiyo ni kejeli tupu."

"Reinhard anashikilia pesa, lakini hatumii kwa tamaa. Sija kaa kwenye hoteli mjini london. Pan-Can hata hanilishi mimi ninapoenda Uingereza."

Rayford alijaribu sana kumfanya Chloe aelewe umuhimu wa kiroho na yale aliyogundua, lakini hangevutwa kutoka kwa mawazo ya vitu vya kilimwengu, na hakutaka kuwekwa upande wa utetezi kuhusu mambo ya imani.

Tuna chumba kwako, mama na Reymie na rafiki wa Guildford," alisema. "Utatumia kwa pamoja na mom na Raymie watakapofika. Ni vigumu kupata madanguro au vyumba vya bei nafuu."

"Na utaishi wapi?" Chloe aliuliza. Hali yake ilibadilika kutoka kwa mshangao hadi hasira, kila baada ya ile hali ya babake kujitolea ilimpita kwenye akili.

"Nitakuwa nikiishi kwenye gari na marafiki wangu fulani," alisema. "Hayo ni kati ya yale ambayo nimekuwa nikijaribu kukueleza."

"Huyu ni Mungu wa aina gani?" Chloe alisema kwa sauti ya juu. Uso wake ulijaa hasira. "Hatakuambia uwache jamii yako. sio sasa, tunapokuhitaji sana" Machozi yalianza kumtoka.

Moyo wa Rayford ulikuwa unapasuka. Alikuwa karibu sana na Chloe, na kudhani kwamba ataelewa hasa jambo muhimu linalomuhusu. Aliamua kumuacha kuwazia juu ya mambo hayo, huku akirejelea jukumu lake kwenye kiti cha rubani kwa muda wa saa.

Aliporudi kwenye kiti kilichokuwa karibu na Chloe, alikuwa ametulia. Alikuwa amepanguza machozi yake.

"Haya", alianza alipo keti. "Wacha tuseme kwamba Mungu anataka ufanye hivyo. Unafikiri atataka mimi na mama pamoja na Reymie tufanye?"

Huyo ndiye Chloe ambaye Rayford alimkumbuka. Kichwa chake kilikuwa kikimuongoza na wala sio roho yake. Lazima aliona mahali fikira zake za kukana zilipokuwa zikimuelekeza na kuchukua muelekeo bora. Heshima na utu aliokuwa nayo Chloe kuhusu babake yalimsaidia katika kuelewa fikira na uamuzi kwamba yale aliyoyataka yatafaa maishani mwake.

"Kipenzi, ningependa kufikiri kwamba Mungu anataka ujiunge nami. Lakini tafakari juu ya hayo wewe mwenyewe."

Chloe aliwaza na kufikiri sana jinsi Rayford alifikia uamuzi wa ajabu kama ule. Lakini kwa wakti huu alijaribu kusikiza, na kuwaza jinsi babake alikuwa akifikiri. Kila kitu kilionekana kuwa shuari alipofanya hivyo.

Rayford alieleza kuhusu kupotea kwa maisha ya watu wengi (wakiwemo marafiki na jamaa yake) kule Amerika, na uwezekano wa kumpoteza mkewe na watoto, yalimfanya kujiuliza maswali mengi.

"Pesa zote duniani haziwezi kuwa hakikisho kwamba nitabaki nanyi, mama na Raymie, alisema. "Na haitakuwa na dhamani yoyote nitakapo simama mbele ya Mwenyezi Mungu. Naelewa kwamba yale ninayofanya yataonekana kuwa upuzi na ushenzi mbele ya watu wengi; Lakini jambo la upuzi na ushenzi ni pale tunapo sahau mambo ya milele, kama vile tunavyofanya.

"Mungu hahitaji pesa," aliendelea. "Aliumba ulimwengu bila pesa, na anaweza kufanya mambo mengi bila hizo fedha. Tazama, Yesu aliongea kuhusu Dunia ya Mwenyezi Mungu, au Ufalme wa Mungu, mahali watu hufanya kazi kwa mapenzi na wala sio fedha. Ni kama kurudi shamba la Edeni. Mipango ya awali ya Mungu kwa binadamu."

Rayford aliangalia machoni mwa mwanawe. Moyo wake ulikuwa umejaa furaha. Alikuwa akisikiza!

"Naona sasa unayaelewa baadhi ya yale ninayosimulia," alisema kwa upole na utaratibu. "Lakini ukianza kuishi vile nimekuwa nikiishi yapata wiki kadha zilizopita, takuwa na maana mara kumi zaidi."

Chloe alifikiri sana. "Ndio, laiti tungalikuja pamoja nawe. Tungaliishi wapi? Ni nafasi kiasi gani iliyo kwenye gari lako?"

Rayford alicheka huku akijibu, kusikia fikira ya kuja pamoja naye ni jambo la kufurahia, hata kuliko swali nzima. Alijaribu kuona kwamba siri zake zisifike kwenye fikira yake. "Hakuna! hatuwezi kutosha kwenye gari," alicheka. "Gari limeja kama unavyofikiri. Lakini Mungu atatuwezesha kufika."

"Sisemi kwamba umenishawishi," Chloe alionya. "Lakini sitaki kukupoteza." Ukweli ni kwamba alidhani kwamba amemezwa na dhehebu fulani; lakini hakutaka malumbano. Iwapo angalitazama na kutafakari mwenyewe ingalikuwa bora.

"Kwa sasa waweza kuenda Guidford pamoja na Neville na Maria," Rayford alisema. "Hawa ni watu waliokomaa na kusaidia kundi hilo kwa miaka kadhaa. Wako na chumba cha ziada wanachotuwachia tunapoenda kule. Tutakuwa na wakati bora kukutembelea na halikadhalika wewe kututembelea."

Ndege ilipotua kule London, wale jama kama kawaida walimlaki Rayford. Fran alichukua mzigo wa Chloe na kusimama huku wakiongea kwa muda huku Rayford akienda kuleta gari. "Ni ghali sana kuegesha gari katika uwanja wa ndege, lakini tunajua sehemu fulani karibu na hapa tunapoegesha magari bure,"

Chloe alishanga sana na babake kukosa kulipa pesa kidogo kama za kuegesha gari kwenye uwanja wa ndege na kutaka mahali pa kuegesha bure. Lakini wiki chache zijazo ataona jinsi watu hawa wanaishi bila kutumia pesa katika nchi ambayo watu wanafurahia kutumia pesa nyingi. Waliita hilo "Umasikini wa roho"

Gari lilikuwa ndogo kuliko alivyotarajia, lakini wale 'jama' wa babake walikuwa watulivu na wazuri kuliko alivyotarajia. Vyumba katika nyumba ya Neville na Maria vilikuwa vya nafasi kubwa na kutosha--- hasa alipolinganisha na jinsi alivyoishi katika chumba cha chini kule Prospect Heights. Chakula kilikuwa cha kutosha na maji masafi pamoja na nguo safi. Kwa lolote lile alikuwa amejifunza na kukubali vitu vidogo hasa wiki tatu zilizopita.

Wakati wa siku nne kabla ya Rayford kusafiri tena, wale Jesans walitayarisha na kumpatia Chloe nafasi ya kutosha kadri alivyotaka. Alifurahi kuhusu jinsi walivyojali maslahi yake. Aligundua kwamba Reinhard alikuwa amehifadhi malipo ya Reyford kutoka kwa PanoCon, na alikuwa na pesa za kutosha kukodi nyumba nyingine punde tu Irene na Raymie watawasili. Watu hawa walitaka kuwashahuri mamake na nduguye Chloe kabla ya kufanya uamuzi wowote mahali familia hiyo itaishi.

Ilikuwa wiki tatu zaidi kabla ya mama na kijana kuwachiliwa huru kutoka kambi walimokuwa. Kwa muda huo Chloe alizoea wale jama wa babake.

"Ni ajabu, au sio? alimuambia Reyford jioni moja walipokuwa wanaburidika karibu na kituo cha Guildford, baada ya shuguli nyingi za siku. "Maisha yetu yote tunaishi kwa kuogopa umaskini; lakini umaskini sio jambo mbaya, au sio?"

"Sio iwapo huu ndio umaskini," babake alisema kutoka ule upande mwingine wa meza. Alikumbata njugu zilizokuwa kwenye sahani. "Pesa zote duniani hazifanyi lolote ila kuwalisha watu, kuwapatia mavazi na kujenga nyumba. Tayari yote hayo tunayo."

 

* * *

 

Irene na Raymie walikuwa wameenda kwa basi kule Toronto; lakini walikosa ndege ya asubuhi ya Pan-Con kuelekea London kwa saa moja. Hivyo basi waliabiri ndege ya shirika la ndege la Uingereza baadaye jioni hiyo. Walipowasili asubuhi na mapema siku iliyofuata, wale wanahiji wengine hawakuonekana, huku Rayford na Chloe wakingojea kumlaki Irene na Raymie. Mama na mwanawe walikuwa wamepoteza uzani, na nywele zao ndio mwanzo ilikuwa inaota. Irene alifunika kichwa kwa kitambaa, lakini Raymie alifurahia upara wa kichwa chake.

Walikuwa na uchovu mwingi kutokana na safari. Hivyo basi Rayford hakutaka kujadili kuhusu mipango yao kuelekea Neville. Punde tu walipofika Guildford, Irene na Raymie walishikwa na usingizi.

Ilikuwa adhuhuri Irene alipoamuka na kuelekea kwenye sebule ya Neville. Rayford, Chloe, Neville, Maria na wale Jesans walikuwa hapo. Rayford alimjulisha Irene na kuwaeleza machache kuhusu yale yeye pamoja na Raymie walikuwa wamepitia tangu kuondoka maeneo ya vilima vya Prospect Heights.

Rayford alikuwa akitaka kuongea na Irene kwa faraga na kisiri kuhusu mipango yake, lakini wazo hilo lilizuka alipokuwa akiwajulisha wale Jesan.

Rayford alikuwa na uhakika kuhusu kujitolea kwa Chloe, na kuwa pia na uhakika kuhusu kujitoa hapo mbeleni kwa Irene kuishi kama mkristo. Jambo la kumfurahisha muno lilikuwa kule kubadili kwa Irene kutoka Clover leaf kule Dakota Kaskazini. Yote hayo yalikuwa kielelezo kuhusu tamaduni na fikira aliyokuwa nayo Vernon Billings juu ya hali yake ya ukristo. Hivi sasa mumewe alikuwa akimpatia jukumu jipya maishani. Juu ya hayo alikuwa akimpatia kitu kilichokuwa cha ukristo wa kweli. Alisikiza kwa makini bila uoga yale Rayford alikuwa akisema.

Baada ya wiki chache, Irene, Chloe na Raymie walibadili hali ya kushirikiana na Rayford na kumpatia heshima kuu, na vilevile kuiga imani yake. Yote haya yalitendeka kila walipokuwa wakijadili, kujifunza au kufikiri juu ya mafundisho ya Yesu na imani yao ikaendelea kukua. Walikubali kwa kauli moja kujiunga na wale jesans.

Mwezi mmoja baada ya Irene kurudi, Rayford aliwachiliwa kutoka mahali alipokuwa akiishi na Pan-Con. Kundi liliazimia kwamba zile fedha walizoweka katika hakiba ya kununua jumba lingine zitumiwe kununua gari lengine la Chloe na Raymie. Gari hilo litumiwe katika shughuli za kugawa katika idara ya ugawaji katika kundi la Jesans.

Neville na Maria walifurahi kuwa pamoja na Rayford na Irene, na kuamua kwamba wawili hao wachukue chumba kimoja.

Kuanzia hapo maisha ya wanajesans yalichukua mwelekeo mpya

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

Kila aina ya mtindo au mbinu inayotumiwa kuleta wokovu, huwacha kiungo fulani muhimu, kiungo hicho ni mafundisho ya Yesu . Katika sura hii, kuna watu wanaosikiza na kupokea mafundisho ya Yesu, na matokeo i msisimuko wa ajabu unaopelekea kubadilika ka maisha yao.

Yesu alisema kwamba wajenzi wa kiroho watawacha nguzo kuu katika mafundisho yake, na kwamba matokeo yake yatakuwa jinsi yule mjinga aliivyojenga nyumba kwenye mchanga. Chochote kile wanachojaribu kujenga kitaanguka. Na kuongeza kwamba yoyote yule atakaye sikiza mafundisho yake na kufuata njia zake, atakuwa kama yule tu mwerevu aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba. mafuriko na kimbunga cha maisha ya sasa na baadaye hayatamuadhiri.

Huu ndio ujumbe wa uponyaji aliotoa Bwana Yesu na kufunndisha. Huu ndio ujumbe tunaopaswa kufundisha hivi leo.

Yesu alisema kwamba iwapo tuna imani katika kushirikiana na kusaidiana katika kueneza mafundisho yake, basi yeyote yule atakaye fuata mafundisho na yale tunayossema, atakuwa akimsikiza na kufuata mafundisho yake. (Matayo 10:40) Katika sura hii, Chloe, Irene na Raymie walipaswa kuanza kukubali mafundisho ya Rayford (kisha Reinhard na wale wengine) katika kutunza na kulinda mafundisho ya Yesu. Walivyofanya walikuwa "wamezaliwa upya" katika "Neno la Mungu", ambalo hasa ni jina la Yesu katika Bibilia. (Tazama Ufunuo wa Yohana 19:13-16.)

 

 

 

KITABU CHA PILI

9.Kuanza kuhesabu

 

"Lingine tena!" Rayford alijiongelesha alipokuwa ameketi kwenye dawati lake usiku mmoja Januari.

Ilikuwa yapata miezi kumi na minane tangu Straits kujiunga na Jesans. Hali ya Rayford kuwa makini katika utabiri wa Bibilia, na mori yake katika kufundisha, ilipelekea kupanda daraja na kuwa kiongozi katika jamii. Alijiuliza iwapo angalikuwa na furaha jinsi hii angaliendelea kuwa rubani. Maisha yalikuwa matamu na ya kupendeza tangu alipochukua uamuzi na kumpatia Mwenyezi Mungu chochote alichokuwa nacho.

Cheo cha Rayford katika jamii kilipelekea kujitoa mhanga kwa Neville, aliyefurahia kufanya kazi pamoja na Rayford kwa kutumia kifaa alichopenda.tarakilishi. Neville alionekana kama kijana barubaru, na Maria asiye na uzoefu wa kusema mengi, alifurahi kuona mumewe akibadilika hivo.

Wote wawili walikuwa wamefanya kazi kwa pamoja zaidi ya mwaka mmoja, huku Rayford akiandika makala kuhusu mambo ya kila aina (na hasa kuhusu jinsi kila aina ya makala yalivyolingana na matukio ya wakati fulani duniani), na Neville kuanda mtandao kwenye tuvuti ili watu waweze kupata yale makala aliyoanda Rayford. Kwa wakati fulani Rayford angalitayarisha majarida manne au matano kwa siku moja. Kichochezi kilitokana na kule kujihusisha moja kwa moja na Jesans, na kutoka kwa fikira au mazungumzo waliyokuwa nayo mitaani.

Neville alianda kitabu cha wageni, msukumo wa mtandao na kifuatilizi katika ukurasa wao kwenye tuvuti. Halikadhalika aliweka utaratibu wa mafunzo, ambao ulinuiwa kuwataini wasomaji moja kwa moja kutoka kwa jarida moja hadi lingine. Neville alihakikisha kwamba ukurasa wao ulipata uwakilishi katika pembe zote za dunia na mitambo yote ya kupeperusha ujumbe wa tuvuti, na pia kukusanya anwani nyingi za barua pepe kutoka kwa jarida la mtandao ambalo lilichapishwa kila mwezi na Chloe pamoja na Reinhard. Dhamira ya jarida hilo lilikuwa kuwachochea wasomaji wengi kuutembelea ukurasa wao kwenye mtandao.

"Tazama hili" Rayford alisema baada ya kumaliza kusoma jarida lililokuwa mkononi mwake. Alipinduka kwenye kiti na kupitishia Irene. "Barua sita katika anuani, na wote kuonekana kuwa na uaminifu. Je itakuwa furaha kupata angalau mshiriki mmoja kutoka kwa hawa wote?"

Rayford alianza kutaambua ukweli wa dhana ya kundi hilo kwamba Mungu alikuwa anakusudia kupinga watu kujiunga nao. Walikuwa hawajapata mfuasi tangu ajiunge nao, na alijaribu kila awezalo kutambua shida. Angalau mara moja kwa mwezi walipata barua kutoka kwa mtu aliyesoma majarida yao au kutembelea ukurasa wao kwenye tuvuti. Lakini hawakupata kusikia lolote kutoka kwa watu hawa tena. Kupata watu sita kwa siku moja wakitaka maelezo zaidi lilikuwa tukio lisilo la kawaida.

Irene alisoma barua hizo na kisha kuongea. "Yaonekana kuwa mambo makuu, au sivyo? kuna mpango upi kuhusu barua hizi?"

"Neville na maria wataondoka wiki ijayo. Nitajaribu kuwaleta wote sita hapa Jumatatu. Kisha sitajibu swali hilo mara kwa mara."

"Wafikiri ni bora kuwaleta hapa?" Irene aliuliza. Azimio la kundi halikuwa kutoa anwani ya Neville kabla ya kumuarifu.

"Nina wazo kuhusu hili," Rayford alisema. Natumai kuna ulinganifu na mazungumzo ya Yerusalemi."

Rayford alikuwa akiongea juu ya mpango wa Umoja wa mataifa kujenga hekalu kwa wayahudi kule Yerusalemi. Dunia ilikuwa imeanza kujiendeleza baada ya kuangamia kwa Amerika, na sasa ulikuwa wakati wa watu kutafakari na kufikiri juu ya mambo mengine. Mazungumzo yalikuwa yakiendelea kule Israel yapata wiki mbili au tatu zilizopita. Katibu mkuu Dangchao alikuwa huko kwa siku tatu zilizopita, na hata Baba mtakatifu alihudhuria.

Waarabu walikaidi na kusema kwamba kutazuka vita iwapo mtu angaligusa mnara wa mwamba, hekalu lao la msikiti. Lilikuwa limejengwa yapata karne nyingi zilizopita, hasa katika eneo la hekalu la Solomon, mahali ambapo tangu jadi wayahudi walimtolea Mungu dhabihu. Lakini Dangchao alikuwa na mbinu ya kuwabembeleza. Mbinu hiyo ilijumuisha ujenzi wa hekalu la kiyahudi upande mmoja wa mnara wa mwamba na ule upande wa pili kujenge hekalu la Kikristo. Msikiti uliopewa heshima hizo hautashikwa. Baba mtakatifu mteule Pope Pius XIII, alikuwa amedokeza kwamba angalitoka Vatican na kuchukua nafasi ya makao mapya kule Yerusalemi, eneo lisilo mbali na hekalu mpya, na pia kama ishara ya kuonyesha hali ya kujitoa kwa Vatican kwenye kumbukumbu ya ushirikiano wa kidini.

Waislamu hawakufurahia uamuzi huo, Lakini kulikuwa na kitu ndani ya Dangchao kwamba hatakubali La kama jawabu.

Iwapo watu walidhani kwamba Amerika ilikuwa na upendeleo kwa wayahudi, Waamerika walionekana kuwa na matumaini kulingana na Dangchao. Idadi ya walinzi kutoka Umoja wa Mataifa ilikuwa imeongezeka katika mji mtakatifu. Na Waislamu walifahamu jambo hili kama onyo kuhusu yale Dangchao angalifanya endapo hawangekubali "mtaji" wa hekalu.

"Mazungumzo Yerusalemi? Sikumbuki ni lini tumekosa kusikia kwamba aina fulani ya mazungumzo yanaendelea kule Mashariki ya Kati. Sasa katika miaka hii yote tulitazamia kuona ukweli halisi wa mambo. Iwapo Dangchao angaliwachilia, hilo litakuwa dhibitisho kwamba kuhusu yale niliyokuwa nikifikiri

Rayford alikuwa akifikiri ya kwamba Dangchao alikuwa kama ilivyotabiriwa kuwa mtu asiyependa Kristo. Jambo kama hilo halikuwa kwenye fikira ya uma, kwasababu lolote alilofanya Dangchao lilikuwa kwa maslahi ya binadamu. Ilikuwa tu ni ufahamu wa Bibilia kulingana na Rayford, ndiposa akahisi kuna tukio lisilo la kawaida kutokana na ujasiri wa Dangchao. Shida moja ilikuwa jina lake. Kulingana na utabiri wa Bibilia (Ufunuo wa Yohana 13:17-18), suluhisho la idadi ya herufi za jina la mtawala wa mwisho duniani litakuwa jumla 666. Haijulikani mbinu au mtindo aliotumia Rayford (Kigriki, kihibrania, Kilatino au hata Kichina iliyo lugha ya Dangchao) idadi ya herufi zote kwa pamoja zilipungua.

Herufi za kiRoma zilikuwa X, D na C, kwa jumla zikiwa 610. Herufi I, V na L zilihitajika kuongeza 56* iliyokuwa imekosea. Katika Kigriki na Kihibrania aidha idadi ya herufi hizo ilikuwa chache. Rayford hakuwa na la kufanya kuyahusu hayo. Hata hivyo kulikuwa na mambo mengine mengi yaliyoashiria kwamba Xu Dangchao alikuwa miongoni mwa wale waliotabiriwa kuwa wakaidi wa Ukristo, na walio mkana Yesu.

Uwezo na kufaulu kwa Dangchao kuuteka ulimwengu kupitia Umoja wa Mataifa, kilikuwa ni kidokezo cha nguvu alizokuwa nazo, lakini Rayford alipaswa kukiri kwamba Umoja wa Mataifa haukuwa utawala rasmi wa dunia. Kila Taifa lilijitawala kulingana na maadili yao.

Lakini Dangchao alikuwa amebuni jeshi la umoja wa mataifa lililosambazwa pembe nyingi za dunia kwa kisingizio cha kudumisha amani. Kutokana na kuwepo kwa jeshi hilo, dunia nzima ilipata amani, au hata umoja, yapata mwaka mmoja na nusu tangu kuanguka kwa Amerika.

 

---------------------------------------------------------------------------------------------

*Herufi I, V, X, L, C na D (Herufi za kiRoma zinazowakilisha 1, 5, 10, 50, 100, na 500) lazima zionekane mara moja (na iwe mara moja), na herufi M (1,000) haipaswi kuonekana katika jina lolote linalotarajiwa kufikia 666 katika kiRoma.

Fahamu: Majina yote yaliyotumiwa katika riwaya hii sio ya kweli. Kuna uwezekano kwamba mtawala asiyetambua Yesu atakuwa na jina lililo na idadi ya 666 katika herufi za Kilatino, Kigriki na Kihebrania.

 

Iwapo Katibu Mkuu Dangchao angalifaulu kupata hekalu kwaniaba ya Wayahudi, Rayford hangalishawishika tu kwamba huyu ni mpiga Kristo vita, bali angaliweza kuhesabu siku zilizosalia kabla ya kurudi kwa Yesu Kristo.

Rayford hakulala mapema siku hiyo, huku akisoma zile barua sita na kufikiri juu ya ule mkutano wa Jumatatu. Alikataa kula siku ya Jumamosi na Jumapili, na kukaa pekee yake chumbani mwake au kuzunguka nje. Alimuambia Irene machache kumuarifu kwamba mambo sio mabaya, kati yao wawili au kati ya Rayford na Mungu. Hali yake hiyo ya unyenyekevu ilikuwa katika ile hatua ya kusubiri au kutarajia mipango ya Mungu.

Alipowapigia simu wale watu waliotaka maelezo kamili, aliwapata kama waliotayari kupokea na kujitolea. Yohana Doorman na Dada Maria Teresa walikuwa na kazi zilizowawezesha kupata fursa ya kuhudhuria. Matayo Baker na Sheila Armitage hawakuwa na ujira. Wale wengine wawili walisema kwamba wataomba ruhusa ili waweze kuhudhuria mkutano huo Jumatatu.

Yohana Doorman aliyekuwa na umri wa miaka 42 alikuwa mfuasi wa Mashahidi wa Yehova, na alipata uguso kutokana na mafundisho na utabiri wa wale Jesans, hivyo basi kuvutiwa. Jesans walihubbiri kwamba serikali zote zina ukaidi, na kwamba Mwenyezi Mungu anatafuta watu wanaotii na kulitimiza neno lake na wala sio siasa. Doorman alikuwa Mpasifisti. Alikuwa amehudumu kama mmishonari katoka bara lake la Afrika na kwa wakati fulani kutiwa mbaroni kwasababu ya imani yake. Alikuwa hajaoa na wakati mwingi alifanya kazi za mkono ili kupata fursa zaidi kutumikia kanisa.

Dada Maria Teresa alikuwa na umri wa miaka 56, mtawa wa kikatoliki na mshiriki wa Wanadada katika Yesu. Aliishi na kufanya kazi ya jamii na wahamiaji katika vitongoji vya mji wa London. Alivutiwa na maisha ya kujitolea ya Jesans, na dhamira ya kujenga jamii iliyojumuisha waliooa na wale ambao hawajaoa.

Matayo Baker alikuwa mbatizaji wa umri wa miaka 40, aliyejishughulisha kwa kutembelea Hospitali magereza na miji. Alifurahishwa na msimamo wa Jesans kuhusu maisha na hasa kuhusu ndoa na talaka. Bibi yake alimtalaki baada ya miaka miwili ya kuoana, kutokana na tofauti za kidini.

Sheila Armitage alikuwa mfuasi wa dhehebu la marafiki na mwenye umri wa miaka 70 na halikadhalika msagaji, na aliyevutiwa sana na Jesans kutokana na moyo wao wa heshima na kushirikiana na imani tofauti za watu, na hasa kuwa muaminifu kwa Mwenyezi Mungu sio sawa na kuwa mwaminifu kwa dhehebu fulani.

Mike Anastopoulos alikuwa mwanagenzi wa umri wa miaka 36 kutoka Uturuki, aliyekuwa akisomea shahada ya uzamili katika Chuo kikuu katika taaluma ya mambo ya kale. Yeye hakuwa mfuasi wa dhehebu au dini yoyote na alijiita Mbinadamu. Mike alivvutiwa na ushirika wa Jesans hasa kuhusu msimamo wao juu ya uchumi, na hasa maisha nje ya uchumi na kisiasa.

Hatimaye tulikuwa na Luis Rafael, mwenye umri wa miaka 29 Mpentekosti kutoka Brazil. Hapo awali alikuwa amejiunga na ushirika fulani wa kipentekosti ulio kuwa na mafundisho ya kutatanisha kuhusu jinzia. Luis alifurahia mafundisho ya jamii kuhusu Bibilia na imani, lakini alichukizwa na baadhi ya mafundisho yao. Alivutiwa na Jesans kutokana na jinsi walivyotafsiri mafundisho ya Yesu Kristo, na jinsi walivyochukulia maadili hayo kama njia ya kukadiri mafundisho mengine.

Rayford alisoma barua hizo zote, na kurudia mara kadhaa Ijumaa usiku, na kujadili mambo fulani yaliyomvutia kuhusu kila mmoja kupitia kwa simu alizowapigia Jumamosi. Wote sita walionekana kama waliokuwa na kiu cha kutaka kufahamu mengi zaidi, hata hivyo kulikuwa na hali ya kuasi miongoni mwa wote hao. Alimuomba Mwenyezi Mungu kumpatia hekima na ujasiri kukumbana na hali yeyote ya uasi atakapo kutana nao Jumatatu.

 

 

* * *

 

Luis Rafael ndiye aliyekuwa wa kwanza kuwasili siku ya Jumatatu asubuhi. Rayford ndio mwanzo tu alikuwa akimjulisha kwa Irene, ndiposa kengele ililia mara nyingine.na mara nyingine. Saa nne kamili, watu hao sita walikuwa wameketi kwenye sebule ya neville.

"Wacha tuone.Tutanzia wapi?" Rayford alisema. "Na iwapo wewe utaanza, kwa kuuliza swali ulilo nalo, nasi tujaribu tuwezavyo kujibu." Alimtazama Irene kana kwamba anatafuta uungaji mkono.

Mike Anastopoulus, mkufunzi wa mambo ya kale, alitazama na kufahamu kwamba wenzake wote kwa kiwango fulani walikuwa wafuasi wa madhehebu fulani. Yeye ndiye aliyeongea kwanza. "Ni lazima tuamini kwamba Mungu yu pamoja nasi katika kikao hiki?"

"Itategemea na vile unavyomaanisha kumuamini Mungu," Rayford alijibu. Hapo aliona Matayo na Luis wakiingilia mara moja, wawili hao walikuwa waingilisti wa kikristo kwenye chumba hicho. Walisonga na kusikiza kwa makini yale Rayford alitaka kusema.

"Mafunzo ya kidini hayatatuponya." "Imani ndiyo itatuponya kwa kuamini Mwenyezi Mungu tunayemtambua. Ukimuita wa upendo au wa kweli, lolote utakalo, lakini ni Mungu."

Mike alionekana kufurahia jawabu hilo, lakini Matayo na Luis walitazamana kwa shaka kabla Luis kuinua mkono ili aongee.

"Sikubali," alisema. "Iwapo mtu ni mnyoofu na muaminifu, basi lazima aweze kumuamini Mungu."

Yohana Doorman alifikia kibeti chake na kuchomoa toleo la gazeti, na kumpatia Mike. "Yahova Mungu anataka kila mtu kumtambua kwa jina lake," alisema. "Kuna makala fulani katika jarida hili ambayo yatakusaidia."

"Je, hilo ni jarida la Amkeni?" Matayo aliuliza. "Je, wewe ni mfuasi wa Mashahidi wa Yehova?"

"Uh-oh," alidhani Rayford. Hili ndilo jambo ambalo alitaka kuepuka. Mashahidi wa Yehova wamekatiliwa kote ulimwenguni na madhehebu yote ya Kikristo. Msisimuko uliokuwa kwenye chumba kile ungewezesha mambo makuu ya Mwenyezi Mungu kujitokeza, bora tu kutakuwepo na masikizano. Kwa sasa mwelekeo uliokuwa unaanza kuchukuliwa ulikuwa ule Rayford ameshuhudia kati ya madhehebu mbalimbali. Yeye aliamini kwamba Mwenyezi Mungu angalitenda miujiza, lakini mambo hayakuwa hivyo.

"Ndio mimi ni shahidi wa Yehova," alijibu Yohana Doorman, kwa madaha huku akishika kidevu chake kwa majivuno.

"Na wewe Je?" Matayo Baker alisema, akielekeza swali kwa Dada Maria Teresa. "Kutokana na mavazi yako, nakuchukulia kama mfuasi wa kikatoliki. Je nyinyi humuabudu Maria?"

"Naam, Mimi." Maneno yalimpotea Dada Maria.

"Waona kinachotendeka hapa?" Mike aliingilia kati, huku akinyosha kidole kumuelekezea Matayo. "Hii ndio sababu sikupata nafasi kwa dini au dhehebu lolote. Hakuna lolote ila malumbano na kushutumiana. Chukua gazeti lako. Sina haja." Alirudisha jarida la Amkeni kwa Yohana Doorman.

"Labda sote tuweze." Sheila alianza, huku akitarajia kuwatuliza; lakini alikatizwa, huku Mike akiendelea:

"Sikuja hapa kusikiza yale mtakayo sema hapa. Nilikuja kusikiza yale waliyonayo Jesans!"

"Haijalishi kile wanachoabudu Jesans," Luis alisema kwa sauti, huku akiruka juu.

"Jambo muhimu ni yale mafundisho ya Bibilia."

"Na iwapo siamini maadili ya Bibilia?" Mike aliuliza.

"Basi labda hauko nasi hapa!" Matayo alijibu, huku akiruka tena huku akielekea upande wa Mike akiongea.

Sheila kwa haraka alisimama kati ya wanaume hao wawili akinyosha mikono yake kana kwamba anaongoza wana ndondi. "Mbona tusikae chini na ."

Lakini Luis alipaza sauti kumshinda Sheila. "Katika kitabu cha Matendo 4:12 Bibilia inatuarifu, "Kwa hakika hakuna wokovu kwa lolote lile; kwani hakuna mahali popote isipokuwa mbinguni."

"IMETOSHA!"

Kulikuwa na hali ya kutoelewana kufuatia mjadala huo. Wale walio kuwa hapo hawakupata kuelewana iwapo Rayford anggali toa maoni yake.

"Ulikuwa kama mlipuko," Luis alisema hapo baadaye, "ila tu ilitoka kinywani mwake."

Lolote au chochote kile kiliwapelekea watu kukimbia ndani ya chumba na kumuelekezea mwenziwe. Dada Maria ndiye aliyeketi peke yake, alikuwa tayari amesongesha kiti chake. Irene aliyekuwa amesimama nyuma ya Rayford ndiye aliye epuka. Wengi wao walijeruhiwa. Mwangaza ulifuatia mlipuko. Kila mmoja kwenye chumba hakuweza kuona kwa muda.

Rayford alipigwa na butwa kama wale wengine. Lakini akaanza kunena-- kwa nguvu asizopata kuwa nazo mbeleni. Ilimuogopesha, lakini ingalimuogopesha zaidi laiti asingalizungumza, kwasababu alielewa kwamba yote yaliyotoka kinywani mwake hayakuwa maneno yake. Yalikuwa maneno ya Mwenyezi Mungu.

Alipoanza kuongea, chumba kilinyamaza na kutulia. Watu walisikiza kwa makini kuliko walivyowai kumskiza mtu yeyote hapo awali.

"Hamjafika hapa leo kwasababu maadili na imani yenu ni sawa na kweli. Mungu amewaleta hapa; na amefanya hivyo kwasababu nyinyi wote ni waaminifu. Kwa miaka elfu mbili amevumilia, na hata kushuhudia mgawanyiko ambao umedumu kati yenu na waumini wengine. Wengi wenu mmehubiri mahubiri yenu yasiyotosheleza, huku mkitumai kwamba mmetoa picha nzima, ilihali mlikuwa na sehemu tu. Kwa kupuuza mmebuni makundi na mkawa wabinafsi kwa kupuuza. Mkawa watu wa kuwatazama wafuasi wa madhehebu mengine kama walio chini yenu na wasiofaa.

"Mungu aliwaacha katika njia hiyo yenu ya kupuuza, ili kujaribu unyenyekevu wenu mbele Yake. Alitaka kuona iwapo mtaweza kutii yale mliyokuwa mkifundisha na kuhubiri, hata ikiwa yalinuiwa kuwatenganisha na jamii au marafiki. Mko hapa hivi leo kwa kufaulu majaribio hayo."

Rayford akapaaza sauti yake tena. "Lakini SASA. sasa, ni wakati wa kukua!" Wale waliokuwemo walisonga nyuma huku wakitarajia mlipuko mwingine.

Lakini haukutokea. Sauti ya Rayford ilipungua badala yake.

"Tafadhali muniamini. Njia ya kipekee ya kuitikia ukweli ni kwa neema ya Mungu. Amewateua nyinyi kwa ajili ya uwazi wenu-- sio kwasababu ya taaluma ya kidini.au kwa kuikosa." Alimtazama Mike alipokuwa akisema maneno hayo ya mwisho.

Rayford alichukua kifurushi cha vijitabu vitatu vilivyofungwa na kuwapitishia wote sita. Muda wa mwaka mmoja uliopita, alikuwa amefanya bidii kutayarisha yote yaliyokuwemo.

"Kuna makala ya kila aina kuhusu mambo tofauti kwenye nakala hii," alisema. "Mtapata baadhi ya kushangaza. Yatakuwa changamoto ya maadili na imani zenu.

"Ndugu na dada," alisema kwa kutua na kutabasamu, "Ni wakati wa kutafakari na kuchambua maswala ya kindani na ukweli ambao hamjawai kupata. Ni wakati wa kudhihirisha kujitolea kwenu na imani yenu kwa kusikiza kila mmoja wenu na kuweka kando tofauti zenu."

Rayford alijaribu kutoa taswira ya mambo aliyokuwa akitaraji.

"Muafaka wa makubaliano unatiwa sahihi kule Yerusalemi leo," alisema. "Kabla kufika alasiri hivi leo , ujenzi wa hekalu jipya utaanza kule Yerusalemi. Lakini muafaka mkuu wa makubaliano umeafikiwa kule mbinguni. Mungu atajenga Hekalu lake, amini musiamini atawatumia nyinyi hapa kujenga hekalu hilo. Tumeingia kipindi au awamu ya mwisho wa miaka saba ya historia ya ujenzi wa kanisa. Mambo makuu yanatukia tu katika kipindi cha miaka mitatu na nusu ijayo, ni jukumu letu kuanda dunia kwa wakati huo."

Rayford alitulia, ilikuwacha uzito wa masimulizi hayo kuwaingia. Kisha akaendelea.

"Kifo cha Yesu kiliadhimisha mwisho wa madhehebu. Mungu kwa miaka elfu mbili amekuwa akimchunguza mtu kivyake, akijaribu kujenga imani inayo zidi mkusanyiko au ufuasi wa dhehebu.

"Sasa hivi atajumuisha maadili mema na vipande vya ukweli na uaminifu kujenga kanisa lake, na wala sio lako".

Mike mwanaharakati za kibinadamu alifurahi kumsikia Rayford akiongea juu ya utu na tabia; lakini alikuwa akijaribu kupambanua kwamba yote yalikuwa yakitoka kwa Mungu-- wa kweli na wa Kikristo. Maneno kama "Kanisa" na "Yesu" yalikuwa magumu sana kwake kusadiki. Mike hakufurahia mazungumzo ya kuanda kundi lingine.

Katika njia moja au nyingine, kila mmoja katika kundi hilo alikuwa anaona uzito fulani. Walikuwa wamewekwa kwa pamoja na watu waliodhani kwa wakati mmoja kama adui. Lakini uwepo wa Mungu uliwashahuri kwamba Rayford hakuwa kama guru aliyetaka kubuni dhehebu.

Rayford aliendelea; "Hivi sasa, katika sehemu nyingine ya dunia kuna mkutano kama huu unaoendelea kama huu. Kuna watu wengine sita kama nyinyi. Mmoja ni Mhindi, mwingine Muislamu, na mwingine Muyahudi." Yale Rayford alikuwa akisimulia hayakutoka kinywani mwake kama hapo awali, bali yalitoka kwa Mwenyezi Mungu.

"Iwapo unafikiri kuna tofauti za kuepuka, fikiri jinsi inavyoweza kuwa. Lakini Mungu anawataka ninyi watu sita kwa pamoja na wale sita walio mahali kwengine, kuendeleza kanisa lake hasa nyakati hizi za mwisho. Nyinyi mtakuwa mahakimu wa nyakati hizi za mwisho. Lakini mwapaswa kuepuka tofauti mlizo nazo.

"Mpango wa Mwenyezi Mungu hapo awali ulikuwa kwa watu wake kuwa na makabila au koo kumi na mbili, na mahakimu kumi na mbili kusuluhisha matatizo yaliyotokea kati ya koo hizo. Sio wafalme. Sio utawala wa kihimla, Lakini mahakimu wa koo. watu kama Samweli, na Gideon, na Debora." Aliwatazama Sheila na Dada Maria Teresa alipotaja Debora.

"Kazi yenu itakuwa kuwasaidia wale wanaoamini kutoka maeneo yenu kufahamu mema na mabaya. Hamtaweza kufaulu kutekeleza hayo kabla ya kuzika tofauti zenu, na vilevile kufahamu upungufu wenu wa kuelewa."

Rayford alihisi upako kutoka kwa Mungu ukididimia na kujihisi tu kama wale wengine.

"Ndugu na Dada sina majibu yote. Yale niliyotayarisha kwenye makala hayo ni muongozo tu. Lakini muhimu zaidi ni kwenu kuelewa na kujifunza kufanya yale Mungu anataka iwapo hata wewe mwenyewe hutaki. Lazima mtazame mbele na sio tu madhehebu yenu. Kuna mengi ya kujifunza kwa muda mchache."

"Tutajaribu kujadiliana tena, wakati huu naomba msikize kwa makini, na kuomba na kufikiri kabla ya kuongea. Nyinyi wote mnaweza kueleza mliyo nayo, lakini hayawezi kuwa mengi mnavyofikiri."

Mazingira katika chumba yalikuwa yamebadilika. Kila mmoja alikuwa mpole. kwa kunyenyekea na kufuata ukweli aliosema Rayford, na uwepo wa Mwenyezi Mungu kwenye chumba hicho. Kwa utaratibu walianza kuondoa tofauti na uhasama baina yao; lakini mara hii kwa uoga. Iwapo hali ya utatanishi ilitaka kutokea, waliomba ili kupata hekima.

Hivyo basi, nusu ya kabila kumi na mbili kutoka Magharibi ilikuwa imebuniwa kama walivyojiita.

 

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Mtume wa Kihibrania, Danieli alitabiri kuhusu "Watu wa Mungu" miaka 453 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. (Danieli 9:24-26) Alisema kwamba imebakia miaka 490 kwa watu wa Mungu, lakini Masia "atakatwa" miaka saba tu kabla ya kukamilika miaka 490, mnamo mwaka wa 30A.D (Tazama Armagedon ya Kwanza" sura ya 6, wiki sabwini" kwa maelezo zaidi kuhusu fungu la maneno haya.)

Kusulubishwa kwa Yesu kuliadhimisha mwisho wa makundi ya madhehebu na dini. Mungu amekuwa akimhudumia mtu na kumtunza kivyake yapata miaka elfu mbili sasa. Mipango ya kuendeleza "Kanisa au dhehebu" fulani yameisha na sasa kuna "ufalme wa mbinguni" ambao Yesu alisema hauonekani. (Luka 17:20)

Lakini Danieli alitabiri kwamba watu wa Mungu wataonekana tena kufuatia "maelewano" yaliyoafikiwa miaka saba kabla ya "kumalizika" kwa vitu (Danieli 9:27) Unabii huu umeandikwa kama kwamba ni makubaliano mawili yaliyo sambamba. Moja ni kati ya Kristo na wafuasi wake na nyingine kati ya waasi wa Kristo na Kanisa.

Maafikiano yatapelekea kutoa kwa kafara mara nyingine (kwa sasa hakuna) Hekalu Yerusalemi. hasa kwa miaka tatu na nusu ya makubaliano. Na pia kuleta pamoja "makabila" kumi na mbili ya wafuasi wa Kikristo.

 

 

10. Makabila Kumi na Mbili

 

Majadiliano yaliendelea siku nzima. Kila mmoja kati ya watu hao sita waliokuwa kwenye sebule ya Neville walikuwa wameona mengi ya kusimulia. Mwisho wa siku walikuwa wameanza kuhisi uzito wa jaribio hili. Dini yao, kazi na familia zao yalikuwa sio muhimu, kila mara imani yao ilipoimarika na kujifunza mengi kuhusu Mungu.

Irene alileta chakula siku nzima, na pia kuhakikisha malazi yote yatakuwepo endapo hao wote wataamua kulala kwa Neville hadi pale watafahamu hatima yao kulingana na mipango ya Mungu. Majadiliano yaliendelea hata usiku wa manane. Waliweza kujilaza kwenye sakafu ili kupumzika na kuendeleza mjadala.

Siku chache zilizopita kulikuwa na mabadiliko kutokana na uamuzi wa wale waliotoa maisha yao na kumkubali Yesu Kristo. Mike alilazimika kukiri sio tu kuwepo kwa Mwenyezi Mungu bali pia yale Mwenyezi Mungu alikuwa amemtendea maishani mwake. Hata ingawa Sheila alikuwa hajashiriki kwenye tabia ya usagaji kwa miaka mingi, alikuwa ametetea tabia ya ushoga kwa maisha yake yote. Sasa alipaswa kukubali kwamba hali yake ya kukaidi na kuunga mkono tabia potovu haikuwa tofauti na yale aliyokuwa akipinga.

Mwishoni mwa juma, kundi hili jipya lilianza kupata miujiza ya kupendana na kuishi vyema, na kuanza kujadili hatua itakayofuata.

Barua pepe na mawasiliano kupitia kwenye tuvuti yaliongezeka. Jambo la ajabu lilikuwa kwamba nusu yake ilitoka Uingereza, na nyingine kutoka Afrika, Amerika ya Kusini, Uropa na mashariki ya kati, wote waliandika wakiuliza jinsi ya kupatana na Jesans, na pia kuungama na kutii mafundisho ya Yesu kama mbinu moja ya kubadili tabia.

Wale Jesans wa kiasili walirudi kutoka shughuli ya kueneza neno, nao Neville na Maria wakarudi kwa wakati huo. Wote hao walijiunga na kusherehekea tukio liliokuwa limetukia.

Kutokana na uzoefu wao kuishi ndani ya imani, Rayford alimpatia kila mmoja wa Jesans mhudumu wa kusaidia mmoja wa mahakimu jinsi ya kujitoa mhanga, kwa kiroho na kimwili katika nchi ya utumwa. Wiki tatu baadaye, kila mmoja wa wale waliookoka aliuza mali yake, na kutoa mali kwa jamii kwa kiwango ambacho walikuwa hawajawai kutoa. Kutoka kwa fedha hizo, tiketi za nauli ya ndege na Tarakilishi zilinunuliwa kwa hawa mamishonari wapya.

Watafutaji wa kweli wa wokovu walikuwa wakisubiri kuwalaki katika sehemu sita tofauti. Luis na Fran walienda Sao paulo, Brazil. Mike na Martin wakaelekea Ankara, Uturuki. Chloe na dada Teresa wakachukua magari kwenye feri kuelekea Ufaransa, na kisha Roma.

Sheila aliwai kuishi Moscow alipokuwa mdogo, kwa hivyo yeye na Reinhard (aliyefahamu Urusi) walijitolea kwenda Urusi. Na hata Raymie aliyekuwa mdogo na miaka kumi na mitano, aliambiwa amsaidie Yohana Doorman kule Johannesburg. Matayo Baker alibaki London kufanya kazi kwa pamoja na Rayford na Irene.

Jamii ndogo hiyo ilikuwa ikikua. "Inatendeka, sivyo?" Fran alisema aliposikia kuhusu wanachama sita. "Inakuja pamoja. Ahsante, Yesuu!" Na Fran aliwashukuru na kuwapungia wale wanaune aliokuwa akisafiri nao. Chloe, Reymie na wengine walitazama huku wakicheka.

Rayford alihutubia umati wa jamii hiyo iliyokuwa ikikua kabla hawajaelekea sehemu zao, mwezi mmoja tangu wakutane:

"Nyinyi wote mtawahudumia takribani watu nusu billioni" alisema. "Muda wenu ni miezi sita kutambua wale waumini 12,000 wenye imani kutoka kwa kabila mtakazo hudumu. Mtahitajika kuwafunza jinsi nilivyowafundisha. Vijitabu na makala hayo yatawasaidia, lakini yatahitajika kutafsiriwa katika lugha za huko na kuchapishwa tena haraka iwezekanavyo. Mtapata majaribio sawa nayale ambayo mmepitia muda wa wiki chache zilizopita. Muombe ujasiri, hekima na uvumilivu kwani mtahitaji hayo yote.

"Lakini msife moyo. Mungu yu pamoja nanyi!"

Licha ya yale wanayotarajia kukumbana nayo walijiona wakiwa na ujasiri kama ule wa Rayford. Mungu hakika alikuwa pamoja nao, na hilo ndio jambo kuu.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Ni hali ya kitamaduni kufikiria kwamba makabila kumi na mbila yaliotajwa kwenye kitabu cha Ufunuo wa Yohana ni ya kiyahudi. Lakini tunasahau kwamba wale wayahudi tunaojua kwa sasa lilikuwa kabila moja (ukoo wa Judah). Tabaka nyingine za Israeli ziliangamizwa hata kabla ya kuzaliwa kwa Yesu. (Hata yale majina ya makabila hayo kwenye Ufunuo wa Yohana ni tofauti na yale majina ya makabila kumi na mbili katika agano la kale. Hebu linganisha kitabu cha pili katika agano la kale (Kutoka) 1:2-7 na Ufunuo wa Yohana 7:4-8, utaona kwamba tabaka la Dan limeondolewa na mahali pake kuchukuliwa na kabila la Manasseh.)

Yale makabila kumi na mbili ya unabii yanawakilisha "Watu wa Mungu". Watu wake kwa vyovyote sio wale waliomkana Mwanawe Yesu. Watu wake ni wale waliomkubali Mwanawe. wale wanaomfuta Yesu (Mwanakondoo) kwa utaratibu popote anapowaelekeza, jinsi Bibilia inavyosema. (Ufunguo 14:3-4)

Mawazo ya kikaidi katika taasisi ya jamii wayahudi ni mfano wa hali ya kototii na kupuuza yale mafundisho na dhamira ya Mwokozi Yesu. Lengo la Mwenyezi Mungu sio kujenga na kuendeleza taifa la ukoo na damu ya Abrahamu, bali ni kujenga na kuendeleza taifa lililo na imani kama ya Abrahamu.

Kitabu cha Ufunuo wa Yohana kimemfananisha Yesu mara kwa mara kama "Mwana Kondoo", ili kutoa taswira ya wafuasi wake wanaofuata Kanisa lililojengwa kwa mkono (Matendo 7:48) ilikuwatoa kafara wanakondoo wengine. Wayahudi wa kiroho hawana haja kuhonyesha kanisa, bali wale wa kimwili hawana matarajio ya juu.

 

 

11. Mavuno ya Kiroho

 

"Miezi sita! Sio nafasi ya kutosha kuwafikia watu nusu bilioni, au sivyo?"

Yohana Doorman alikuwa akiongea na Raymie Straight huku wakipaa kutoka London hadi Afrika ya Kusini.

Lakini kichwa cha Reymie kilijaa mawazo mengine tofauti na hayo kwa wakati huo

Mamake-- Irene jinsi alivyokuwa akimuita-- hakuchukulia kuondoka kwake vyema. Hakufikiria kwamba yu tayari kwa jukumu kama hilo; lakini Rayford.(Raymie alifurahi kuwaona wazazi wake kama ndugu na dada katika Yesu.) Rayford alikuwa amemtetea Raymie, huku akimjulisha Irene jinsi kijana huyo alikuwa amekomaa kwa muda wa mwaka mmoja na nusu.

Raymie alimkasirikia Irene. Alijua kwamba alimdhania kuwa yule kijana mdogo, Lakini alifurahia kwamba babake alimuamini hata akiwa mchanga, na alitaka kutimiza jukumu hilo.

Hapa hivi yeye akiwa na umri wa miaka kumi na mitano na mshahuri mkuu wa wale mahakimu kumi na mbili duniani. Nani angaliamini kwamba kijana mpotovu kabla ya kuangamia kwa Amerika angaliweza kuwa na cheo mashuhuri kama mkuu wa kikundi kikubwa cha kidini duniani.!

Maneno ya Rayford yalimrudia. "Waweza kutimiza, Raymie, mradi tu unaelewa na kukumbuka kila hatua ya jinsi usivyoweza kutimiza. Sio bila msaada wa Mungu."

"Unisaidie nikumbuke hayo," aliomba kwa mara ya miamoja tangu aanze kujianda kusafiri pamoja na Yohana.

Yohana Doorman hakujaliwa kupata watoto. Hata alikuwa hajawai kuoa. Lakini alimpenda Raymie, na kuonyesha mapenzi na dhihirisho la kushahuri kijana. Hiyo ndio iliyokuwa sababu kwa Rayford kumuachilia Raymie awe pamoja na Yohana. Kwa pamoja Raymie na Yohana walikuwa na jukumu la kutafuta wafuasi 12,000 halisi katika mataifa yaliyo fanya Afrika Kusini na Afrika ya Magharibi.

Wazo la Yohana lilikuwa ndani ya akili ya Raymie, na mara moja Raymie aliitikia.

"Ndio. Ni kazi kubwa sana, ama sivyo?" alisema. "Lakini kumbuka kwamba twaweza kufanya? Tunaweza fanya iwapo tutakumbuka kwamba hatuwezi kufanya bila usaidizi wa Mwenyezi Mungu."

Yohana alitikisa kichwa kukubali, na kunyamaza kimya ili kutafakari kuhusu hayo ambayo Raymie alikuwa amesema, na kisha kuendelea;

"Niko na wazo fulani, Raymie," alisema, huku akitoa kijitabu kidogo kutoka kwa mfuko wa shati. "Nataka kupata wazo lako hapa".

Jambo moja lililo mfurahisha Raymie ni kwamba Yohana alimchukulia tu kama mtu mzima, hasa kwa mambo ya kiroho. Yohana alikuwa mtu wa kuisikiza wote, alimchukulia Raymie jinsi alivyowaona wanachama wengine wa makabila kumi na mbili, na hasa kama ndugu katika roho.

Yohana alikuwa na mipanga ya kuanda kambi nne kule Johannesburg kama alivyomueleza Raymie, moja kwa watafsiri, nyingine kwa waalimu, moja ya shughuli za uchapishaji na kueneza, na ya mwisho ya usimamizi na mawasiliano ambapo yeye na Raymie watafanya kazi.

 

"Hiyo ni sawa sana kwangu," Raymie alisema.

"Lakini itatuchukua kama miezi sita hivi kufundisha wafanyikazi wetu," aliyekuwa mfaasi wa Mashahidi wa Yehova alilalamika. "Na tutahitaji mamia ya watu kama hao kabla ya kumaliza."

"Unakumbuka yale Baba. Yaani, yale Rayford alisema kutuhusu kama mahakimu?" Raymie aliuliza.

"Nafikiri inamaana kwamba sio lazima kumfundisha kila mtu. Mungu atawafundisha iwapotutakuwa huko."

Raymie alipeana mkoba aliokuwa ameshikilia. Ndani kulikuwa na mafunzo aliyotumia kila moja ya makundi sita.

"Hapa ndani kuna majarida mbalimbali kuhusu mafundisho na juu ya kusikiza kila mmoja. Unakumbuka jinsi wale jamaa walivyojifunza wenyewe ulipowacha dini? Twapasa kuwacha wafanye hivyo kadhalika."

Yohana hakutaka kusema lolote kumuudhi Raymie, ila tu angaliweza kukariri "Kishindo kikuu" cha Rayford, lile kundi lililokuja kwenye sebule ya Neville lilikuwa na kishindo, alikuwa na shaka kuhusu uwezo wake kuwasihi watu "kukoma kuwa wafuasi wa dini" kama vile Raymie alieleza. Yeye pia alisema maombi yake kwa kimya.

Iwapo watahitaji mapumziko au kuhitajika mahali popote, kulikuwa na watu wengi kwenye kundi waliokuwa na uwezo wa kutafsiri hata kwa lugha za kienyeji.

Musa aliyeteuliwa kama mhasibu wa kundi, alikubali kutafuta na hatimaye kukodi nyumba tatu zaidi, na kutuma maombi ya kuletewa nakala za kingereza mara moja, huku Alama katika lugha zingine zikitayarishwa.

Ringo alichomoa kitabu kilichokuwa na orodha ya anwani zilizotayarishwa na kundi hilo kabla ya kuwasili kwa Yohana na Raymie. Yeye pamoja na Sylvia mkewe, walichukua jukumu la kuwakaribisha walioleta anwani zao katika kituo cha elimu (mara tu watakapopata kituo) na kuanza kujifunza na kuishi maisha ya makabila kumi na mbili.

Sylvia aliwaarifu kwamba mwanamke aliyetoka alitisha kuvuruga na kuhangaisha kundi. Aliuliza jinsi ya kuepuka majaribio na janga iwapo wanachama watakao hasi na kukaidi na kuwageukia.

"Isipokuwa wakuu au wasimamizi wa kundi, hakuna yeyote anayepaswa kufahamu mambo yanayoendelea katika kundi lingine," Abdullah alisema. Tunaweza fanya kazi katika vitengo. Kwa wakuu na wanachama, majina mengine yatatumiwa. Hivyo hata iwapo watadhulumiwa hawataweza kutoa maelezo."

Kwa mara nyingine Yohana na Raymie walitazamana jinsi walivyokuwa vichochezi katika mfumo uliokuwa ukiendelea kwa njia yake. hasa, kwa njia ya Mwenyezi Mungu.

Baada ya wiki mbili, sehemu zote nne za utendaji zilikuwa mbioni. Wanne zaidi walikuwa wameenda katika kituo cha elimu, mahali Ringo na Sylvia walikuwa wakufunzi washikilizi. Mmoja kati ya wanafunzi alielewa lugha mojawapo ya kienyeji na wale wengine hawakujua, hivyobasi kuteuliwa kama mmoja wa wale watafsiri punde tu atakapo maliza mafunzo hayo.

Mwishoni mwa juma la pili, kanda na majarida yaliyotolewa na kuandikwa na Rayford yalikuwa yakitolewa katika idara ya tafsiri. Muda huo ndio ombi la kwanza la makala yaliwasilishwa kwenye idara ya ugawaji. Ombi lingine la makala katika lugha ya Kiafrikana, lilitolewa, na lilikuwa tayari kusambazwa wiki inayofuatia. Musa alikuwa akijianda kununua Magari yenye nguvu ili kuweza kufikia sehemu za barabara mbovu na njia zisizopitika kwa urahisi. punde tu yale makundi ya kufanya kazi hiyo yatahitimu.

Katika kipindi cha juma kadha, utaratibu huo utaendelezwa mahali kama vile Accra, Capetown, Harare, Monrovia, Kinshasa na Lagos.

Ilikuwa jukumu la Raymie kupokea na kujibu barua, tayari alikuwa akipokea barua kutoka Afrika Kusini hasa wale waliofahamu kuhusu mtandao wa Jesan, na waliotaka kujifunza mbinu zao.

Lilikuwa pia jukumu la Raymie kumfahamisha Rayford kule Uingereza kuhusu matukio na yale yalio kuwa ya kiendelea. Wale wanagenzi wake pia walikuwa na jukumu la kuhakikisha kwamba Irene alitulia na maslahi yake kutunzwa.

Yale yaliyokuwa yakifanyika kule Johannesburg hayakuwa sawa na yale yaliyokuwa yakitukia katika miji mingine mahali mahakimu wa kikabila walikuwa wamewasili. Rayford alikuwa amewasiliana na wahudumu wenzake katika mashariki ya mbali, mtu aliyejulikana kama Chaim Rosenberg, aliyekuwa mkaazi wa Sydney, Australia. Chaim alikuwa na umri wa miaka sitini, naye pia alikuwa ameteua na kuanzisha mahakimu sita. Jukumu lao lilikuewa kusimamia Asia kubwa na vitongoji vya Asia. Mahakimu wa mashariki walikuwa Sydney, Tokyo, New Delhi, Karachi, Beijing na Hong Kong.

Katika miezi sita iliyofuatia , uanachama katika makundi ya makabila hayo uliongezeka kwa takriban mara tatu kila mwezi. Walifanya kazi kwa utaratibu, ili wasiweze kuzua taharuki. Dunia nzima ilikuwa imeja kasumba ya filosofia ya upendo na amani kwa wakati huo, kiasi kwamba hawakuwa wakiona au kuhisi yale yaliyokuwa yakitokea kufuatia kazi ya makabila kumi na mbili. Hata katika mataifa ambayo kazi ya umishonari ilikuwa imepigwa marufuku, kulikuwa na machache yaliyofanywa kuwasimamisha walipoweka mabango usiku wa manane, au walipochukua jukumu lakuwaarifu waumini yale Mwenyezi Mungu alikuwa akitenda.

Hata ingawa milango ilikuwa wazi, ni wachache waliokuwa wakipitia. Waliweza kupata mtu mmoja kati ya 50,000 aliyekaribia viwango vyao. Yale waliyokuwa wakipambana ni kupata kundi la kiroho litakalo kuwa na uwezo wa kutoa mafundisho ya Mwenyezi Mungu kwa dunia, katika yale yatakayo tukia kuwa kipindi cha giza katika historia ya dunia.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Makadirio ya Rayford yalikuwa kulingana na fungu la maneno katika kitabu cha Danieli, kwenye Agano la kale. Mtu anaweza kubashiri kipindi cha miaka saba katika makubaliano yatakayopelekeahali ya kutoa dhabihu kurudia Yerusalemi na "Kumalizana" (au mwisho). Mwengine anaweza kubashiri kipindi cha siku 2300 kutoka ule wakati wa kuanza kutoa dhabihu hadi pale sehemu ya utakaso itakapo safishwa.

Tofauti kati ya tarakimu hizi mbili (siku 2520 na siku 2300) ni muda unaoweza kuchukuliwa kujenga Hekalu. (Tazama jedwali.)

 

 

Danieli 9:24-27 imeandikwa kwa mbinu ambayo waweza kudhani inaarifu maagano mawili sambamba, moja kati ya mfalme wa dunia na wafuasi wake na nyingine Mfalme wa amani na wafuasi wake. Moja itapelekea kujenga hekalu, na nyingine kujenga roho kimiujiza.

Lakini kati ya hayo yote jambo la ajabu hutokea kati ya miaka ya mwisho saba, na kusababisha "mkumbo wa ukiwa" na kuharibu aina yote ya "hekalu"

 

 

12. Hekalu

 

Mike na Martin walikuwa na jukumu la kutunza tabaka la Judah, lililojumuisha eneo la mashariki ya kati na Afrika ya masharika. Hekalu la Yerusalemi lilipokaribia kukamilika, wote wawili walitayarisha safari isiyo ya kawaida mbali na tarakilishi zao huko Ankara ili kutembelea kundi ndogo la wafanyi kazi wa mji mtakatifu. Lengo na dhamira ya safari hiyo lilikuwa kujionea yale yaliyokuwa yakiendelea. Talanta na hekima ya Mike kuhusu utaalam wake wa mambo ya jadi yalimfanya kufurahia mitindo ya ujenzi.

Baba mtakatifu alikuwa ametaka kuhamia Yerusalemi, jumba la kifahari lilikuwa linaandaliwa kwa heshima yake karibu naHekalu la Mlima. Jambo hili lilichukuliwa na wanavyuo kuwa sawa na kujiunga na ukristo kwa Constantino. Kwa kutangaza ukristo kama dini yake na katiba ya utawala, na yeye mwenyewe kama mkuu wa dini, Constatino alikuwa amewashawishi wakristo wa hapo awali kutoka kwa makundi yao hadi upande wake, mahali wamedumu mpaka hivi sasa. Kwa kutumia maarifa hayo, Baba mtakatifu alikuwa ameanza kuwachukulia wayahudi na waislamu kama "ndugu" (iwapo walitaka au la) na kwa kufanya hivyo alikuwa amejitwika kama mkuu wa dini hizo tatu.

Wayahudi walitaka hekalu ili kuepuka kushirikishwa na mpango wa Rome, na kuwepo wanajeshi wengi wa Umoja wa Mataifa kule Yerusalemi kwa wakati huo kuliwachaWaislamu wakiwa na njia mbili tu, kufuat yale "ndugu" zake wawili walikuwa wameafikiana.

Miaka 2000 ilifanya mji wa Vatican kuwa mtakatifu kama vile Baba Mtakatifu, katika hali ya utakatifu, Yerusalemi inashinda mji wa Roma. Vicar wa Kristo alipaswa kufanya uamuzi wa kuishi katika mji ulio mtakatifu zaidi kuliko miji mingine.

Januari ya mwaka huo maafikiano yalikuwepo kujenga hekalu mbili. Sasa miezi saba baadaye mijengo ilikuwa iankaribia kukamilika. Mike na Martin walidhuru eneo hili kukagua mradi huo.

Mnara wa mwamba, mahali yaaminika kwamba Muhammed alipaa mbinguni, uliwachwa pasipo kuguswa. Hii iliwezekana kwa sababu hekalu la Kiyahudi liliwekwa upande wa Mashariki-Magharibi (wala sio Kusini Kaskazini) mbali na mnara uliokuwa yadi kadha kutoka kwa Msikiti. Langu kuingia hekalu lililinganishwa na Lango la Dhahabu la ukuta wa Mashariki. Kwa kufuta mtindo wa Hekalu la awali (lakini kufanya "refu" kuliko ilivyokuwa), Hekalu jipya liliingia upande wa Kaskazini kwenye sehemu iliyokuwa ukumbi wa wageni waliotembelea Mnara wa Mwamba.

Kulikuwepo Basilika ya Kikatoliki iliyojulikana kama Cathedral ya Ibaada Takatifu, iliyokuwa upande wa Kusini mwa Hekalu la Mlima. Kwa nje lilionekana kama pacha la Hekalu la Kiyahudi, lakini kulikuwa na mpangilio tofauti humo ndani, ili kuchukua mamia ya waumini na kwaya nzima. Mahali pa "Utakatifu kwa Watakatifu" palijumuisha kwenye mpangilio wa Kiyahudi, kulikuwepo hema takatifu la Kikatoliki kwa shughuli ya kutoa sacramenti.

Upande ule wa mbele ulikuwa umepanuliwa ili kutoa nafasi pana ya Hekalu Msikiti na Kanisa kuu la jimbo la askofu. Wakristo wale wawili hawakuwa na budi kukiri kwamba kuwepo mnara ule katikati ya majengo mapya meupe yaliyo fanana kilikuwa kielelezo chema cha ujenzi.

Wakuu wa madhehebu mbalimbali walifurahi na kuongea kuhusu jinsi Yerusalemi ("Mji wa amani") ulikuwa tayari kukaa kama jina lake. Hekalu zilizofanana zilikuwa dhihirisho la wazi kwamba amani kote ulimwenguni ilikuwa mbioni.

Sehemu zilizoandaliwa awali, kana kwamba hazikutokea mahali, zilipunguza muda wa ujenzi. Hatukuwepo na kungojea kwa vifaa vya ujenzi, kwani kila kitu kilikuwa kimenunuliwa hapo awali.

Ulimwengu wa kawaida haukujali kuhusu hekalu hilo; lakini baadhi yao ilikuwa ishara ya mambo makuu. Yakustaajabisha zaidi, miongoni mwa watu hawa alikuwemo Katibu Mkuu Xu Dangchao, mtu asiye na haja au kuwa na uhusiano na dhehebu lolote. Alikuwa amekatiza mashahuri mbambali na shughuli zake ili kufika Yerusalemi wakati makubaliano yalikuwa yakiafikiwa kuhusu mradi wa hekalu.

Mike na Martin walipokuwa Yerusalemi, habari kutoka kwa jarida la Time Magazine (Sasa hivi kule Hong Kong) kuhusu chimbuko na uzao wa Dangchao. Habari hiyo hata hivyo haikupewa uzito, aidha haikutoa maelezo kuhusu kiini cha Dangchao kuvutiwa na Hekalu , jambo ambalo Mike alitaka kuelewa.

Ilionekana kwamba licha ya Dangchao kuzaliwa na kukua kule Tibet, wazazi wake walitokea jimbo la mkoa wa Kaifang nchini China. Xu lilikuwa mojawapo ya majina saba ya Kichina yaliyo chukuliwa na baadhi ya Wayahudi waliokuwa wakitangatanga kule China yapata miaka elfu moja iliyopita. Wale Wayahudi walikuwa wameona na wanawake wa China kwa miaka mingi, kiasi kwamba sura ya uzao wao ilikuwa sawa na ile ya China na majirani. Hata hivyo, uzao na elimu yake kule China ni ya hali ya juu, haikusahauliwa kwamba mababu wa Xu kutoka Kaifeng walikuwa Wayahudi.

Wachache, kutoka uzao wa Juda walibaki. Lakini babake Dangchao aliwacha kumbukumbu. Alimbatiza mwanawe kwa jina la Levi Xu Dangchao.

Matumizi ya jina la tatu nchini China haikuwa ajabu, lakini jina la tatu la Kiyahudi halikuwa jambo la kawaida.nje ya jimbo la Kaifeng. Xu Dangchao katika ujana wake aliwacha kutumia jina la Kiyahudi alipo toka Tibet kuelekea Uingereza kusoma katika Chuo Kikuu cha Oxford; na swala la kuwa na jina lingine halikuibuka hadi hivi sasa.

Makala hayo yalieleza kwamba chimbuko la uzao wa Dangchao kutoka kwa Wayahudi ndicho kiini cha kutaka Hekalu kujengwa Yerusalemi. Ilibainisha wazi kwamba alikuwa akitoa heshima kwa mababu wake, jambo lililo gusa mioyo ya wengi. Lakini hilo halikutoa maelezo au sababu ya kutaka Kanisa la Jimbo kuu la askofu kujengwa karibu na Hekalu la Mlima.

Mike alihisi kitu fulani kuhusu, jina la tatu la Xu Dangchao, na katika Hekalu tatu. Alipomaliza kusoma alienda kutazama kwa makini majina kamili ya Dangchao, na kuanza kuhesabu na kukadiri jumla ya herufi zilizomo nadani.

"Hapo ndipo!" alimuambia Martin, aliyekuwa amesoma kwa pamoja naye yale makala. "Idadi ya herufi zilizokosea kwenye majina yake sasa zimeleta idadi kamili!"

Mike alikuwa akiongea kuhusu herufi ya L, V, na I kwenye jina Levi. Kuwakilisha 50, 5, na 1 katika herufi za kiRoma. Kwa pamoja na herufi za kiRoma X, D, na C kutoka kwa Xu Dangchao, zinazowakilisha 10, 500, na 100 katika kiRoma, idadi ya herufi hizo kwa kujumlishwa ilikuwa 666, idadi iliyotabiriwa kuhusu kiongozi wa mwisho wa ulimwengu. asiyemuamini Yesu. Mike alijua kwamba Rayford alikuwa akitafakari kuhusu maana ya jina la Dangchao, na hivyo basi kumpatia nakala hiyo.

Rayford alimjibu kwa utabiri wa Makabila kumi na mbili: "katika muda usiozidi miaka mitatu," alisema, "Dangchao atasimamisha kafara, naye mwenyewe atachukua mamlaka ya Hekalu. Ndiposa anataka kujua utaratibu wa ujenzi. Siku moja yatakuwa makazi yake rasmi ya utawala, na kuulazimisha ulimwengu mzima kumsujudu na kumuabudu."

Hapo awali, Rayford alikuwa ameandika kuhusu yale aliyofikiri kuhusu Hekalu zile.

"Hekalu hizo, kama vile Dangchao, ni sanamu," alisema. Yawakilisha ujinga wa Mwanadamu kwamba amani itakuja kupitia mikono yao wenyewe, na wala sio kunyenyekea na kumuamini Mungu.

"Itaonekana kama isiyo na madhara kwa watu ambao hawajapata kumtambua Yesu. Mengi ya makanisa yanadumu nyakati za Agano la Kale, siku ambazo wat waliamini makanisa. Hivyo basi majengo au jengo moja la kifahari, linalojumuisha madhehebu matatu makubwa na yenye nguvu duniani, daima machoni mwao ni kitu cha kuvutia. Lakini ni kwa sababu wanaamini na kutumaini kwenye mijengo, na sio kujitoa kwa moyo wao."

Kulingana na Rayford, kuungana kwa taasisi hizo za madhehebu ilikuwa ni muigo wa kuunganika kwa pamoja makanisa yasiyoonekana, kama ilivyokuwa ikidhihirika kwa kubuni Makabila Kumi na mbili. Madhehebu ya ulimwengu hu yameweka matumaini kwenye suluhisho la kisiasa, alisema, huku waumini wa kweli walikuwa ndani ya roho mtakatifu na mwenyezi Mungu, atakaye waunganisha kwa njia yake.

"Iwapo Mungu hatajenga nyumba, basi wanafanya kazi bure wale wanaojaribu kujenga," alinakili kutoka Agano la Kale.

Mike na Martin walikuwa wamerudi Ankara wakati wa ufunguzi rasmi. Lakini walitazama sherehe hiyo moja kwa moja kupitia kwa runinga pamoja na ulimwengu mzima.

Midpoint

* * *

 

Kanisa kuu la jimbo la Askofu halikuwa limekamilika wakati wa ufunguzi wa hekalu, mwishoni mwa kipindi cha joto mwezi wa Juni. Vyombo vya habari havikujishughulisha na yale yaliyokuwemo kwenye kanisa hilo kuu. Wangaliona Makanisa kama hayo wakati wowote na popote. Haja yao ilikuwa ni Hekalu.

Kulikuweko uwezekano tu wa Hekalu moja la Kiyahudi.

Ingawa jamii ya wahubiri ya Walawi (Levi) ilikuwa imekufa, chimbuko mpya la wahubiri lilikuwa limeanza kuibuka la vijana wa Kiyahudi chini ya masharti fulani. Kutoka kwa kundi hili, Kuhani mkuu alikuwa ameteuliwa ili kuongoza shughuli za Hekalu ikiwemo ufunguzi rasmi.

Watu mashuhuri kutoka jamii ya Kiyahudi walikuwepo pamoja na wanasiasa. Ingawa watu wasiokuwa Wayahudi hawakuruhusiwa humo ndani, Picha na michoro ya mpangilio wa humo ndani zilitolewa kwa waandishi wa habari. Solomon angalifurahia. Karibu kila kitu kilikuwa dhahabu au fedha, au jumla ya dhahabu na fedha. Sakafu iliyotandikwa mkeka nadhifu,, visawazishi vya hewa, na kipaaza sauti cha hali ya juu vyote kuonyesha tofauti kati ya hekalu la awali--lile lililojengwa na Solomon, au lile lililojengwa na Zerubbabel.

Hekalu za kwanza zilikuwa mfano wa Safina ya makubaliano, sanduku takatifu lilio kuwa na Amri Kumi na nyimbo zingine za utakatifu. Kuhani tu ndiye aliyepaswa kuingia "Patakatifu kwa Watakatifu" mahali pa safina, na kwamba ungaliingia tu mara moja kwa mwaka. Kuhani aliyeingia humo ndani alifungwa kwa kamba kiunoni, iliaminika kwamba angalipigwa dhoruba na Mwenyezi Mungu endapo alifanya dhambi na kisha kufa.

Hekalu jipya halikuwa na chochote kulinganisha na Safina au Amri Kumi. Lakini ulikosa makabadhiya Kiyahudi, kwa heshima ya historia, katika Agano la Kale na nyakati za kisasa. Makabadhi ya vitu hivi hayakuwa tu kwa utakatifu wa watakatifu. Yalonyeshwa kote katika Hekalu nzima.

Wakati Solomon alitakasa Hekalu, moto ulitoka mbinguni kumaliza kafara. Ule moto wa kimiujiza, ulikuwa umeendelezwatangu hapo ili kuendelea kuchomeka. Lakini hakuna aliyetaraji Mwenyezi Mungu kutoa ishara ya Uwezo na nguvu zake kwenye Hekalu hilo mpya. Mwanga wa miali ya kisayanzi (Laser beam) ulielekezwa kwenye mazibao na kuwasha moto wa milele, ili kutolea kafara.

Watu mashuhuri walitoa hutuba kila baada ya mwingine kwa matumaini kwamba Mungu alikuwa amewaelekeza watu wake katika nchi aliyowaahidi Waisraeli. Kafara zilizidi kutolewa mchana na usiku kucha, huku wale waalikwa wasio mashuhuri wakingoja fursa yao ya kutoa kafara baada ya takriban miaka 2000 kwa niaba yao na mababu wao.

Kulikuwepo machozi ya furaha na sherehe kwenye mji huo usiku wote. Ukuta wa majonzi ulibadilishwa na kuwa ukuta wa furaha, na jumuia ya dunia kufurahia kwa pamoja na Wayahudi, waliokuwa wameteseka kwa karne nyingi, na waliokuwa sasa wakiabudu kwenye Hekalu lao.au katika lile lililo tayarishwa na Katibu wa Umoja wa Mataifa Jenerali Levi Xu Dangchao kwa matumizi.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Pazia iliyokuwepo kati ya utakatifu na watakatifu iliraruka, kutoka juu hadi chini (Matayo 27:50-51), kwa wakati ule Yesu alisema "Yamekwisha", na akafa msalabani, yapata miaka 2000 iliyopita (Yohana 19:30). Yesu alikuwa ametabiri kuharibiwa kwa Hekalu (Matayo 24:2), utabiri uliodhibitishwa mnamo mwaka wa 70 A.D.

Hata ingawa hatukuwepo na maelewano kuhusu yale aliyoyasema, shtaka moja lililo mpata lilimwezesha kupata zaidi ya shahidi mmoja kukubali wakati wa mashtaka, ni kwamba ati Yesu alikuwa ametisha Hekalu lao la dhamani (Matayo 26:59-62). Kile alichowasilisha kilikuwa muhimu kuliko Hekalu (Matayo 12:6). Aliongea kuhusu wakati ambao umoja hautahusu mahali tunapoabudu, lakini kuhusu yale maadili ya kindani , kama vile uaminifu na imani (Yohana 4:21-24). Miili yetu sasa ni hekalu la Mungu (Wakorintho ya kwanza 3:16).

Ukristo wa kisasa umerudia ule wa Agano la Kale kwa kuabudu Kanisa, kiasi kwamba taasisi ya Kanisa la kisasa ni Uyahudi uliopakwa rangi nyingine.

Lakini ongea juu ya muungano au ushirika unao husu siasa na utaikosa ile alama. Ongea kuhusu mapenzi bila kumhusisha aliye na mapendo, bila shaka hautapata mavuno.

 

 

13. Alama

 

Wengi wa wafuasi wa Uropa waliojiunga na tabaka la Maria Teresa (lililo jumuisha Afrika Kaskazini), walikuwa na utajiri mwingi, ambao haungaligawia tu watu maskini kutoka Afrika, bali pia tabaka zingine katika mataifa yanayostawi. Lakini kupata msaada kutoka sehemu moja hadi nyingine haikuwa rahisi.

Uropa iliongoza mataifa mengine kupokea "Alama", chembechembe ndogo iliyokuwa ikipata umaarufu kote ulimwenguni, kutokana na utendaji wake hodari. Makabila Kumi na mbila, kama Jesans kabla yao, hawakutaka matumizi ya kadi za pesa, kadi za kukopa na kadi nyingine zinazotumiwa badala ya pesa, na hasa matumizi ya Alama. Jambo hili lilifanya shughuli za kibiashara kuwa ngumu kwa makabila yote, na hasa wanachama wa Uropa.

Msimamo uliochukuliwa na Makabila Kumi na Mbili ulitokana na utabiri na laana inayojitokeza katika sura ya 13 na 14 ya kitabu cha Ufunuo wa Yohana:

"Yeye (asiyemfuasi wa Yesu) husababisha wote, wakubwa kwa wadogo, tajiri na maskini, walio mateka na walio huru, kupata alama kwenye mkono wa kulia, au kwenye paji la uso ili mtu asiuze au kununua, ila tu yule aliye na Alama, au jina la mnyama, au nambari ya jina lake." (Ufunuo wa Yohana 13:15-16)

"Yeyote atakaye abudu mnyama huyo au sanamu yake, na kupata Alama kwenye paji la uso au mkono wake, atapata kuonja divai ya ukali na adhabu ya Mwenyezi Mungu, itakayo mwagwa kwenye kikombe chake pasipo kuyeyusha; na kisha kuchomwa kwa moto mbele ya malaika watakatifu, na mbele ya mwana kondoo. Moshi kutoka humo utaelekea juu milele na milele, na hawatapata kupumzika usiku wala mchana, kwa wale wanaoamini mnyama huyo na sanamu yake, na yeyote atakaye pokea Alama ya jina lake." (Ufunuo wa Yohana 14:9-11)

Bila Alama, haikuwa rahisi kwa Chloe dada Maria au yeyote aliyekuwa katika tabaka lao kununua chochote. Rayford na Chaim hawakuwafundisha kwamba kadi hizo zilikuwa muhimu, lakini walifundisha kwamba mfuasi wa kweli alipaswa kukosea kwa kuwa muangalifu badala ya kutoa radhi na kuelekea kupokea alama. Ukweli ulioumiza ulikuwa kwamba mengi yalifanyika kwa kutumia kadi hizo. Dada Maria alianza kujihusisha na biashara za magendo, ambazo zilihitaji pesa nyingi ili kuhusika.

Hata ingawa Waingilisti wa awali waliapa kupinga matumizi ya Alama ilipokuja, punde tu walipoona inawasonga, iliwabidi kuchukua mwelekeo mwingine ili kuitumia, kama walivyo fanya kadi hizo za ubadilishanaji. Mabishano yao ya mara kwa mara yalikuwa kuhusu iwapo Mwenyezi Mungu angewaadhibu watu kwa kutekeleza kitendo kisicho na hatia kama kununua na kuuza.

Njia moja ya kufikiri ilikuwa kwamba Wakristo wangalichukua Alama bila kuabudu shetani, na hasa bila "kuuza roho yao" kwa shetani, huruma ya Mwenyezi Mungu ingaliwarudhuku kwa matendo hayo. Katika hali ya uhalisi walicho sema ni kwamba, hata iwapo wangali abudu sanamu au kuuza roho zao, wangalisema swala la "Kumuomba Yesu moyoni mwao" kabla ya kuuza, Mungu angelazimika kuwasemehe. Fundisho hilo lilidhihirisha ubinafsi, kujipenda, tamaa lutokuwa na uaminifu, na kila aina ya dhambi ungalifikiri kwa karne nyingi kabla ya Alama, hivyo basi ilikuwa ni kawaida kuchukua mwelekeo huo wa kukaidi.

Alama ilichukua miundo tofauti. Kwa umbali, ilikuwa ile alama ndogo, nyuma ya mkono wa kulia. Teknologia ilikuwa imefaulu kutengeneza chembechembe ndogo (au kitu kisicho na uzito) kilichokuwa kidogo sana hata kisionekane kwa macho makavu. Kilikuwa na nambari ya kujitambulisha ya kimataifa isiyo lingana na aina yeyote. Kwa alama hiyo mtu angaliupunga mkono wake wa kulia kwenye miali fulani iliyotumia nguvu za radio ili kutambua kiasi cha fedha za kuongeza au kutoa kwenye akaunti ya benki. Hii ingalifanyika kila mara unapohitaji kununua au kuuza chochote.

Kwa walemavu wasio na mkono, au wale wasio na uwezo wa kutumia mkono wao wa kulia, tulikuwa na Alama ya kibadala. Watu hawa wangalipata Alama hiyo kuwekwa kwenye paji lao la uso. Wangaliweka kichwa chao mbele ya kifaa hicho cha miale ili kuidhinisha uuzaji au ununuzi.

Aina nyingine ya tatu ilikuwa kuhusu watu (hasa wale wenye utajiri mkubwa) walioogopa kwamba wangaliuawa kisha kile chembechembe kuondolewa na watu wakora. Mamlaka iliwahakikishia kwamba chembechembe hiyo ilikuwa ni ndogo sana, na haitakuwa rahisi kuipata baada ya kudungwa, na kwamba kile kifaa cha miale kingalitambua mtu aliye na chembechembe mbili na kukata kutoa huduma.

Kwa wale wasiotaka kudungwa na kupachikwa chembechembe hiyo walikuwa na fursa ya kuwekwa tu alama iliyoonekana kwenye mkono wao ili kuonyesha rasmi kwamba "Wamekubaliwa kihalali kutopachikwa chembechembe" (Declared and Certified Legally Exempt from Verification Implant) iliyo kuwa kwa kifupi kama DCLXVI, au 666 katika herufi za kiRoma!

Watu wasio kubali kupachikwa chembechembe wangaliruhusiwa kuweka nambari ya kujitambulisha kwenye mashine ya miale, kama ilivyofanywa hapo kabla ya Alama.

Labda Dangchao peke yake ndiye hakupaswa kupata aina yeyote ya Alama kwani jina lake lilikuwa ni Alama.

Chloe na Maria waligundua kwamba, kutokana na matumizi ya Alama yalivyoenea kule Uropa, wanachama wapya walikata kutiwa ile alama au kupachikwa chembechembe kwa sababu moja au nyingine. Kwa wengi lilikuwa ni jambo la ajabu tu kwani hawakuelewa yaliyokuwa yakiendelea kwenye benki. Mshangao huu ulidhihirisha kwamba Mungu alikuwa akiwakinga dhidi ya Alama.

Hata hivyo Rayford na Chaim walifanya juhudi kuwaelimisha wanachama kuhusu yaliyokuwa yakiendelea, na haja ya kujianda kufa kabla ya kukubali Alama.

Wachache kati ya wanachama wao walikuwa na kadi hizo za kukopa au kulipia. Hii ilikuwa hakika kwa wale waliotoka Uropa. Lakini daima walijaribu kutumia pesa kwenye biashara. Kwa muda kadi hizo ziliaribiwa.

Benki zilianza kuweka masharti mapya kwa watu waliokuwa na pesa nyingi. Malipo ya nauli ya ndege, kodi, kuchapisha, magari na hata vyakula na mavazi kwa kutumia pesa yalicheleweshwa, na hata kuwapelekea watu kulipia juu zaidi kuliko kawaida.

Rayford na Chaim waliomba makabila kumi na mbili kujitayarisha kwani itafika wakati hawatakuwa na uwezo wa kutumia kadi hizo au pesa. Chloe alikuwa amejifunza mengi kwa zaidi ya mwaka mmoja na nusu aliokuwa pamoja na Jesans na kutayarisha mwongozo juu ya kuishi bila kutegemea usaidizi kama huo. Mbinu zake tatu za kuishi zilikuwa "Omba, Badilishana au Iba." Kuomba na kuiba kuliwashangaza wanachama wenzake hadi pale alipofafanua.

"Ni fahari ya kidini tunayokumbana nayo," Chloe aliandika. "Tunaongea juu ya kuiba vyakula vilivyotupwa kutoka kwa maduka ya jumla au kuomba wakulima kuturuhusu kuokota matunda yaliyosalia baada ya mavuno. Kizingiti kinacho tushikilia sio kwamba tunafanya maovu. Ni hali ya kujivuna."

Kule Uingereza Rayford alikuwa ametafiti kwa pamoja na wale viongozi wengine na kisha kumaliza na kundi lililotembelea duka moja la jumla lililokuwa mashuhuri kwa Jesans kule London Magharibi. Kila kiongozi alipaswa kuingia kwenye pipa na kuchakura chakula au bidhaa zingine za dhamani. Ilipowadia zamu ya Irene, aliingia kwenye pipa moja kwa kusita huku Rayford akishika doria nyuma ya gari karibu naye.

 

Irene aliyekuwa ameepa kutekeleza mambo kama hayo walipokuwa wakiishi na Rayford kwenye vyumba vya Guildford, alikuwa na wasi wasi. Alijipinda nyuma ya pipa la kiwanda, ili kukanyaga ua lililokuwa karibu, kabla ya kupanda ndani.

Lakini kabla ya kujiinua, aliona kitu kikisonga ndani ya pipa, na kuingiwa na hofu. Mbele yake alimuona mwanamke mkongwe aliyekuwa amevaa matambara, nywele zisizo laini na uso mweusi kwa uchafu. Wanawake hao wawili walitazamana kwa mshtuko.

Lakini alikuwa mwanamke yule dhaifu wa matambara aliyeongea kwanza.

"Irene!" aliita kwa sauti na mshangao, na kisha kujifunika mara moja kama kwamba ni aibu.

Irene hakuwa na la kusema. Ni vipi huyu mwanamke mkongwe na mchafu aliweza kujua jina lake? Kisha aliona kitu fulani usoni mwa mwanamke yule alichokitambua.

"Elaine? ni wewe? Elaine!"

Irene aliinama kumkumbatia yule mwanamke dhaifu, aliyekuwa ameanza kulia, kwa hofu na kuokaka.

Wakati Rayford alikuja kuona mbona amechukua muda, Elaine alikuwa amesimulia yote yaliyompata. Yale aliyowacha yalikaririwa kila mara walipokuwa wamemaliza shughuli hiyo ya kuchokora.

Elaine Billings aliweza kutumia gari na pesa za Tom na Betty kununua mafuta, na kujiendesha pamoja na mmewe hadi kule Montana, walipomuacha Irene kule Dakota Kaskazini; lakini Vernon alikufa kutokana na miali ya jua wiki moja baada ya kuwasili.

Wale wanahiji walikuwa wamesambaratika walipokuta kwamba hakuna Masia kule Montana. Baadhi ya watu kadhaa walijifanya kuwa Yesu, ili hali wengine waliona wampatie Mungu muda, na ndoto zao zitakuwa kweli. Kwa jumla lilikuwa kundi la wanahiji waliosikitika. Wengi wao kama Elaine walipotewa na imani huku wakishindwa la kufanya. Wengi walikufa walipokuwa kule Montana kabla ya helikopta kuwanusuru baada ya wiki kadhaa.

Ilikuwa ni bahati tu au utaratibu uliokiukwa ndio uliomfikisha Elaine Uingereza. Alikuwa ameelewa kwamba alikuwa na binamuye kule Uingereza ambaye angalijali maslahi yake. Lakini kwa kuchanganyikiwa, mamlaka ya wakati huo (wengi walikuwa wa kujitolea) walifanya machache kudhibitisha madai yake. Alipowasili, Elaine alipata maskini binamu wake aliaga dunia baada ya kukumbwa na mshtuko wa moyo mwaka mmoja kabla. Alikuwa peke yake katika nchi ya ukiwa pasipo msaada wa aina yeyote.

Elaine hakufanya juhudi zozote kuomba kutunzwa au kupata msaada kutoka kwa kanisa lolote au shirika lolote la kibinadamu. Na kuchagua kujitafutia tu katika vitongoji vya miji. Licha ya hali yake hiyo ya kushangaza na kutisha, Elaine alikuwa na tabia timamu iliyo muwezesha kuishi katika maisha hayo ya ukiwa kwa zaidi ya mwaka mmoja na nusu.

Elaine kwa utaratibu alianzakurejelea hali yake kutoka kwa hayo masaibu. Kwa sababu wote walikuwa wamepitia kwenye njia hiyo ya hiji, yeye pamoja na Irene walikuwa pamoja kuliko dada wa aina yeyote. Irene alimuona mwenzake huyo kama baraka kutoka kwa Mungu, kwa niaba ya mwanawe wa kike na kiume alio waaga miezi kadhaa iliyopita. Elaine alikaribishwa na kukubaliwa kwenye tabaka la Yusufu kama mojawapo wa waasimamizi wa kundi la Guildford.

Tukirudia maelezo ya Chloe kuhusu kuishi bila Alama. "Kuiba" kilikuwa kitu cha hapo awali ambacho Elaine alikuwa hodari, baada ya mwaka mmoja na nusu kwenye vitongoji vya mji. Alikuwa na ujuzi wa kuchokora na kuishi kwa kutumia vyakula vya mapipa. Lakini bila shaka alikuwa hodari katika ubadilishanaji. Alikuwa amejifunza kuokota vito vya dhamani, na kisha kubadilishana na kwa vyakula, nguo na hata mahali pa kujikinga usiku. (ingawa alitegemea kuomba kujikinga).

Kubadilishana ilikuwa njia muafaka ya kuepuka Alama, hasa kwa wanachama wa Makabila Kumi na Mbili waliokuwa wakitoa utajiri wao, na kutoona haja ya vitu vya ulimwengu kwenye maisha yao mapya. Katika miaka ya usoni walihitaji kufanya hivyo ili kupata mavazi na chakula. Iwapo walikuwa tayari kupata hasara yeyote, walitaraji kupata mtu wa kuwapatia walichohitaji kwa pupa.

Upungufu ni kwamba ubadilishanaji hautawezekana ili kupata tikiti za usafiri au gari, kwa sababu ya hati za makaratasi zinazohusishwa. Hivyo basi Makabila Kumi na Mbili yalionywa na msemaji wao kwamba watakumbana na nyakati ambazo watakosa vitu fulani kama hivyo.

Wafuasi hao walikuwa wamebaki na muda wa miaka mitatu na nusu baada ya kutiwa saihi makubaliano ya ujenzi wa Hekalu, na kisha kulazimishwa kuondoka kwenye mfumo wa kiuchumi; lakini kwa majaribio, walikuwa tayari wameanza, hasa wale waliokuwa wakiishi upande wa Magharibi.

Jesans na wengine waliokuwa nje ya mfumo huo kama Elaine hata kabla ya mkataba huo, walitambuliwa kama walio na umahiri wa kuishi katika nchi za utumwa. Walikuwa wamefaulu kwa kukata kutumia Kadi za aina yoyote--- na kipao mbele chaAlama.

"Hatuhitaji maelezo mengine kuhusu Alama zaidi ya yale yaliyo kwenye injili," aliandika Chaim Rosenberg, akiwa Australia "Alama haizungumziwi huko," aliendelea. "Lakini huko, kuma mafundisho yaYesu, tunahimizwa, kuwa kama maua au kama ndege, viumbe visivyo na kazi, hakuna kazi ya kulima, na hawana haja ya kufuma nguo. Mungu anawalisha, na atatulisha iwapo tutaweka kazi yake mbele. Laiti tungalitilia hilo maanani karne kadha zilizotangulia, , tungali kuwa tayari kukabili yanayotarajiwa kutukia."

Chaim alifundisha kwamba shida zitakazo wakabili wafuasi wakati wa mwisho itakuwa ni kutokana na kuasi au kutozingatia mafundisho ya Yesu.

"Wasio mfuata Yesu hawapaswi kutuwinda," aliendelea. Wale wasio na imani kamili wanajitayarisha kupokea Alama. Wengine walio werevu wako tayari kukana Alama, hivyo basi wataangamia na kufa. Itatendeka hivyo kwasababu hawajapata kumti na kumskiza Mwenyezxi Mungu kila mara. Hayo ndiyo tunayojifunza hivi sasa. Lakini wale wanao kimbia adabu kama hii watalipa kwa uchungu miaka michache ijayo."

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Alama ya Mnyama ni karibu sana na kweli, wale wanaojadili na kudai kwamba sio utimilizo wa Ufunuo wa Yohana 13:15-17, wanajihusisha au kuelewa kiufundi. Hapana shaka kwamba tutakuwa na maendeleo katika taaluma ya kiufundi miaka michache inayokuja, Ulimwengu mzima utajiingiza kwenye mfumo wa biashara uliotabiriwa miaka 2000 iliyopita. Na Bibilia inatueleza kwamba uvumbuzi huo utatoka kwa wanao muasi Yesu. Waweza kutafakari kuhusu usemi huu au kumtupa Mwenyezi Mungu na Bibilia.

Kutokana na onyo kali linalotolewa na utabiri huu kuhusu kukubali Alama, itahitaji mtu aliyekufa kiroho kutozingatia na kuendeleza anasa na hali ya maisha ya vitu vya ulimwengu huu (wakiwemo waumini wa makanisa) pasipo kubadilika.

Hivi sasa wengi wa watu walio Magharibi, inaonekana kwamba hawako tayari "kuwa salama" na kuishi kama Wakristo wa jadi. Kuna utajiri mwingi katika jamii zetu, na kuna neti za kushikilia yeyote anayetaka kufanyia majaribio aina ya maisha ya kiroho kuliko jinsi ya kununua kabati mpya yakuweka nguo na magari mapya. Lakini wanaendelea kumuasi Yesu.

Bila au na Alama, dunia (tena yakiwemo makanisa) imeendelea kuweka imani yake kwenye mambo yasiyofaa, na kupoteza muda mwingi kujishughulisha na maovu wanayodhani yatawaletea furaha.

 

 

14. Amani! Amani

 

Kutoka siku ya ufunguzi wa Hekalu, uanachama wa Makabila Kumi na Mbili (idadi iliyokuwa 144,000) uliweza kudidimia. Kwa ghafla ilikuwa ni vigumu kushawishi na kutafuta wafuasi, kama ilivyokuwa kabla ya kutiwa sahihi kwa makubaliano ya Hekalu.

Rayford na Chaim walikuwa wamejitayarisha kukabili hali hii. Walibadili himizo lao baada ya kufunguliwa kwa Hekalu la kuhubiri ndani na wala sio nje. Vikao vilihamishwa kutoka mahali pa kulipa kodi hadi kuwa maskwota kwenye nyumba zisizotumika; tarakilishi sogevu ziliweza kuunganishwa na simu ili kuwasiliana kwa mtandao. Katika miezi saba na nusu ya kwanza, wachache kati ya wanachama 144,000 waliweza kupata fursa ya kusoma jarida la digest, ukweli halisi uliokuwa umetayarishwa na kuandikwa na Chaim na Rayford. Sasa walikuwa na nafasi ya kujadili yale yaliyokuwa yameandaliwa hususan kuwahusu na nafasi yao katika historia.

Wale waliokuwa na jukumu la kutafsiri walikamilisha jukumu hilo, na Neville pamoja na Rayford waliweza kuboresha ukurasa wao kwenye mtandao, na kuanda maelezo katika lugha tofauti kwenye tuvuti. Kanda za CD na zile za mziki zilitayarishwa, kwa pamoja na mamia ya tani za makala.

Marekebisho na haja ya kuhariri makala hayo ilikuwa ni lazima, kwani walikuwa wakienda kutoa ujumbe uliotofauti baada ya tukio hili ukilinganisha na ule wa hapo awali. Rayford alieleza katika makala aliyoita "Kutia mhuri na Ng'ambo". aliandika:

"Enyi watu mmetiwa mhuri au kuchaguliwa spesheli na Mungu ili muweze kuwa nguvu yake katika kueneza ujumbe wake wa mwisho katika miaka mitatu na nusu iliyobaki katika historia ya Kanisa."

"Msishangae kwamba hamuwezi kuona dhibitisho la mhuri kwa nje. Mhuri huo unatambuliwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe. Lakini kuja kwetu pamoja na kuunganika kama jamii moja kutoka mbali na mbali, ni dhihirisho kwamba alituchagua."

"Mungu ataweza kujaza nafasi endapo mmoja wetu atakufa au kukata kufuata mwana kondo. Licha ya hayo idadi yetu haitaongezeka kamwe. Mwaweza kusema kwamba hatima yetu imefungwa. Lakini kama mnavyotambua, bado tuko na uamuzi wa kibinafsi. Tunaweza kuchagua kukana wito huu na tupotee. Usijipeleke kumjaribu Mungu kwa kuamini uongo kwamba hawezi kuchukua uridhi wako (kama alivyofanyia Wayahudi, na jinsi alivyofanyia taasisi ya kanisa); kwani ukifanya hivyo, nafasi yako itachukuliwa na kutolewa mtu mwingine"

"Vile vile Mungu anayejua kutofautisha mwanzo na mwisho, anajua kwamba angalau wengi wetu tutaendelea mbele na hatutarudi nyuma. Aidha pia anafahamu kwamba, wengi wa wale walio kataa kumfuata na hawajajumuishwa kwenye uanachama wetu, watamuasi, hata nini ifanyike.

"Kilichobakia sasa ni juu yetu kuelekeza umati mkubwa ili usiadhiriwe na adhabu ya wasiomfuata Yesu. Lakini ili kufanya hivyo tutahitaji kujenga Huzuni Kubwa. Nitafafanua:

"Kama mnavyojua, watu kila siku wanakubali Alama ya Mnyama, na wafanya hivyo kwa mamilioni. Wameambiwa na wakuu wa madhehebu yao wafanye hivyo kisha kusingizia kutojua, au kutaka msamaha kutokana na huruma ya Mwenyezi Mungu punde tu Yesu atakaporudi, na kuokolewa. Itakuwa ni jukumu letu kuhubiri kinyume na hayo, na wakati huo kuwapa mabilioni ya watu waliopokea alama fursa ya kuungama na kuokoka."

Makabila Kumi na Mbili yalishangazwa sana na maelezo ya Rayford kuhusu kuokolewa kwa watu ambao tayari walikuwa na Alama ya Mnyama. Lakini Chaim alimuunga mkono.

Hawakuelezwa jinsi ya kuwahubiria au kuwatolea ujumbe wale waliokuwa na Alama. Waliambiwa tu itadhihirishwa na kufunuliwa baada ya miaka tatu na nusu ya mwisho. Kwa sasa walipaswa kufundisha kwa bidii kama kwamba hakuna fursa kama hiyo.

Makabila hayo yalisikia mengi kiasi cha kutenda angalau mawili. La kwanza lilikuwa ni kuomba uhakikisho kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwamba hawajadanganyika. Walikuwa wakiishi katika nyakati za uongo kama ilivyotabiriwa, na kwamba yale Rayford na Chaim walisema yalionekana kama uongo, mhali ambapo wameepuka.

Jambo la pili lilikuwa jinsi ya kuwachukulia wale walio kuwa na Alama. Ilikuwa rahisi kuwa mchoyo, kiasi cha kuto wapenda wale waliopotea. Lakini nini kingalitokea iwapo ulimwengu haujapotea milele? Na je iwapo wale 144,000 wangalikuwa wamepotea milele? Utatanishi kama huu kuhusu imani yao na ile ya wasio na imani ulikuwa bora; ulifanya kinyume na mwelekeo wa kujivunia dhehebu.

Huku wakingojea wakati huo wa kuhubiri kuwadia, Makabila hayo Kumi na Mbili yalishindwa kusadiki kwamba walikuwa wakiishi nyakati za mwisho. Ulimwengu kwa kimiujiza ulikuwa unapata marekebisho kufuatia mkasa mkubwa kuwai kutokea duniani, mkasa uliosababisha vifo vya watu milioni thelathini na tano huko Amerika. Baada ya maafa hayo, ulimwengu ulikuwa unastawi kwa haraka kuliko hapo awali. Uongozi wa Xu Dangchao ulileta mabadiliko ya kila aina, yote yaliyomnufaisha karibu kila mtu. Hata Makabila Kumi na Mbili yalikuwa yamenufaika kutoka kwa masikizano baina ya madhehebu.

Ilikuwa vigumu sana kuamini kwamba hapo usoni kulikuwa na maandalizi ya huzuni na kuhangaika kwa ulimwengu, ambao ulilinganishwa na kuangamia kwa Amerika!

"Itumie! Itumie!" Chaim alikuwa ameandika katika utaratibu wa matumizi ya wakati nyakati hizi za amani duniani. "Lakini usiamini hata kwa sekunde moja kwamba ni hakika," alionya.

Chaim na Rayford walifikiri kwamba kufikia sasa mamlaka yalikuwa yameanza kutambua kuwepo kwao na kwa kiasi kidogo yale waliyokuwa wakifanya, na ni muda tu kabla ya shoka kuwaangukia.

Utabiri wa watu wa Mungu kuhaidiwa "mabawa ya mwewe" ilikuepuka kusulubiwa, ulikuwa umewafikia. Kwa hakika ilikuwa ni ushairi tu. Hawakutarajia kumea mabawa. Lakini hata kama walipata ndege ya kuwasafirisha, walishindwa mahali pa kujificha ili wasitambuliwe na zana za kiteknologia zilizokuwa zikitumiwa na mataifa kuwinda na hatimaye kupata chochote au mtu waliyehitaji.

Usafiri wa ndege ulikuwa ni mgumu kutokana na hitaji la kuwa na Alama, ili kupata tiketi, aidha pia mamlaka yaliyo miliki ndege na viwanja.

Wataalamu wa Bibilia walifundisha kwamba mahali pa kujificha ni Petra, mji uliochongwa kwa miamba ya mawe, kule Yorodani. Lakini hatujui iwapo taaluma ya kisasa itakosa kuingia mahali kama pale, na iwapo palikuwa mahali pa siri, basi siri hiyo ilitambuliwa na wale walioandika na kueneza ujumbe kwamba ni mahali pa siri.

Maandiko yalieleza kama mahali pa kujificha "jangwa" au "mahali pa ukiwa" lakini hakuna yeyote kati ya viongozi hao wawili aliyesema ni mahali papi. Kwa sasa waliwasihi wanachama kuchukua mwenendo wa utaratibu, na kutamai kwa Mwamba Imara wa Milele, na mafundisho yake, tuliyoambiwa na Bibilia yatakuwa Mwamba usiotingika, na kuwakinga dhidi ya "mafuriko" na "dhoruba" (Matayo 7:24-25)

Wataalamu wengine wa Tarakilishi waliokuwa miongoni mwa kundi hilo walijiunga na Neville, na kwa pamoja wa kaanda mawasiliano kupitia kwa tuvuti hadi kwenye mtandao wao, ili iweze kuwa vigumu kuwafikia. Lakini walielewa kwamba baada ya muda fulani, mtandao wao utagunduliwa.

 

*.*.*

 

Ilikuwa yapasa miaka mitatu tangu kufunguliwa kwa hekalu kule Yerusalemi. Wakuu wa usalama wasiopungua nusu dazani walikuwa wamejikusanya kwenye sehemu isiyo na mwangaza mwingi, kuzunguka mashine ya kisasa ya tarakilishi na vifaa vingine vya mawasiliano katika afisi fulani kule Moscow, ilikuwa ni Jumatatu jioni mwishoni mwa Juni. Wafanyi kazi wengine walikuwa wameenda nyumbani jioni baada ya shughuli za siku nzima.

Mmoja wa wale wataalamu, mtu mnene aliyejulikana kama Sergei, alivunja kimya huku wakitazama kio cha tarakilishi moja, huku wakitaraji kitu fulani kutokea. "Yeyote kati yenu aliyeuzuru ukurasa wa mtandao huu?" aliuliza., ili kutuliza uchovu wao.

Walitazamana tu, huku wakiofia kujibu. Sergei alidhani kwamba ameuliza swali la upuzi, lakini alijaribu kuendeleza swala hilo kwa mazungumzo zaidi.

"Ni stihizai, kweli. Wanafikiri kwamba watu wanaweza kuishi bila pesa. Wanasema chembechembe itakayopachikwa imetoka kwa shetani." Sergei alicheka sana. Hatukuwa na jibu. Waligeuka na kumtazama Sergei kama kwamba walitaraji aongee.

"Nili-nili niliutazama tu kwa sababu kijana wangu wa kiume aliniambia niutazame," alisema kwa kujitetea. Lakini hayo yalimuweka fikira zaidi. Macho yaliinuliwa, na moyo wa Sergei kuzama kwa kutatizika na yale aliyosema juu ya mwanawe ili kujiondolea lawama.

"Kweli, haku. na maanisha." aliaanza bila uhakika wa kumaliza aliyokuwa akisema.

"Ndio hiyo!" alipaaza sauti mmoja kati ya wale maafisa, ambaye alikuwa akitazama kio cha tarakilishi. Sergei na mwanawe kwa muda walikuwa wametengwa, hasa kwa muda.

"Ni Uingereza. Magharibi mwa London!"

Wale wanaume walifaulu kupata chimbuko la mtandao wa Rayford.

"Tutausimamisha mtandao huu wa wasaliti hawa sasa hivi!" alisema yule mzee, aliyeonekana kuwa msimamizi wao. "Lakini twapasa kujua kwanza ni nani aliye nyuma ya mpango huu. Oleg tafuta London kwenye simu!"

 

* * *

 

Wafanyi kazi wa Web Wonders, kule makutano ya Clapham, ndio walikuwa wakimaliza zamu yao kuingia usiku, ulipotendeka. Mlipuko haukutokea humo ndani bali kule juu, miale ya nguvu iliyopenya ndani ya jumba lile, na kisha kulipuka, na kuteketeza kila kitu humo ndani wakiwemo watu wale na kubaki jivu, na kwa wakati huo kuwacha tu yale majumba yaliyokuwa karibu na alama za moshi kwenye ukuta. Web Wonder nawafanyi kazi wake wote hawakuwepo tena.

Mwanzo wa huzuni kuu ulikuwa umewadia.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Wafasiri wengi wa Bibilia wanatafsiri kuhusu miaka saba ya huzuni mkuu kabla ya Yesu kurudi. Lakini Ufunuo wa Yohana unaeleza wasi kuhusu kuwepo kwa awamu mbili za nusu ya miaka hiyo saba ya mwisho. Imeelezwa kama miaka tatu na nusu, miezi 42, au siku 1260. (Ufunuo wa Yohana 11:2-3, 12:6 na 14, 13:5, na Danieli 7:25, 9:27) Ni nusu ya mwisho, yaani miaka mitatu na nusu ya mwisho iliyo jaa dhiki kuu. Nusu ya kwanza ndio hujulikana kama "amani ya plastiki".

Wengi wamesema kwamba vita ndiyo ishara ya siku za mwisho, Yesu alisema kwamba vita ni ishara yakwamba sio karibu (Matayo 24:6). Lakini, maandiko yanatoa onyo kwamba waasi na wasio mfuata Yesu ndio watakao tawala dunia na kuongoza `amani' au kwa tafsiri nyingine `Maendeleo' (Danieli 8:23-25). Mtume Paulo, akiandika kuhusu nyakati za mwisho, alionya kwamba `uharibifu wa ghafla' utafuatiwa na kila mtu kusema "Amani! Amani!" (Kitabu cha I cha Wathesolonika 5:3)

Ufunuo wa Yohana pia unaeleza kuhusu wanajeshi waaminifu 144,000 walio wafuasi wa mwana kondoo (Ufunuo wa Yohana 7:2-4, na 14:1-12), na wakati huo kuongea juu ya "umati mkubwa usio hesabika." (Ufunuo wa Yohana 7:9-17) Umati huu umeletwa mbele ya mwenyezi Mungu wakati wa Huzuni Mkuu. Wafuasi kadha kwa kimiugiza wamelindwa (Ufunuo wa Yohana 12:14), lakini wengine wamechinjwa kwa wingi (Ufunuo wa Yohana 13:7). Fumbo la kweli iliyo kama uongo!

 

 

KITABU CHA TATU

15. Mauaji ya Siri?

 

"Nitafanya. Sitaogopa! Nitafanyia Mwenyezi Mungu."

Neville alikuwa akiwaza na wenzake kuhusu barua-pepe aliyo pata sio iliyotanguliwa kutoka kwa Mike aliye Ankara. Mike alisema kwamba lile kundi lililokuwa Yerusalemi lilipita mita mia moja kutoka eneo alilokuwa Dangchao mara nyingi, katika shughuli zao mjini humo. Alisema kwamba usalama wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa haukuwa wa hali ya juu kama alivyodhani.

"Yuko na walinzi," Mike aliandika. Lakini iwapo mtu angalikwenda mbio na kumkaribia huku amevalia bomu, sidhani kama wataweza kumsimamisha."

Ujumbe wa Mike ulisababisha mjadala katika makao makuu ya Guildford, kuhusu iwapo itakuwa bora, huku wakifahamu mengi kuhusu Dangchao, kufanya mipango ya kumuua.

"Huyu sio kama binadamu," Neville alieleza. Ikiwa yeye ni Ibilisi, nini mbaya kwa kumuua?"

Rayford hakuwemo humo, lakini Irene ndiye aliyeuliza fikira yake kuhusu hayo. "Zaidi na hayo, je iwapo ni kiongozi bora kama vile dunia nzima inavyo dhani?" wote walimtazama Irene kwa mshangao. Je, alikuwa amedanganyika? Aweza kuwa alikuwa akiongea kuhusu kumtetea aliye muasi Yesu?

"Sisemi kwamba hawezi kuja kuwa shetani aliyezaliwa upya," alieleza. "Lakini tazama aliyofanya hadi hivi leo. Amewaleta watu pamoja kama vile ulimwengu haujawai kushuhudia. Amesaidia mataifa maskini kwa njia ambayo hayajawai kusaidiwa. Ameleta uwiano baina ya dini na madhehebu mbalimbali jambo ambalo limetufaidi." Mshangao ulikuwa unaibuka, hivyo basi Irene alianza kufafanua.

"Ninayo sema ni kwamba anaweza kuwa akifanya mazuri haya yote kwa nia mbaya." na akakimya. ".ama kwa kweli anaweza kuwa akitenda mema haya na kisha baadaye kutawaliwa na shetani hapo baadaye. Je vita vyetu ni kati ya Xu Dangchao aliye binadamu au ni shetani atakaye chukua mwili wa Dangchao wakati ujao?"

Matayo kama hakimu wa ukoo wa Yusufu ndiye aliyekuwa wa kwanza kumuunga mkono Irene.

"Hatujui kwa hakika iwapo Dangchao ni binadamu, na ni kama mimi nawe kwa wakati huu." alisema. "Lakini kama ni Ibilisi nasi ni wapatanishi!"

Maelezo hayo yalikuwa na maana ikikumbukwa yalikuwa yanatoka kwa aliyekuwa mbatizaji, aliyeamini kwamba majeshi yangalitumiwa kutekeleza mapenzi ya Mungu. Lakini hiyo ilikuwa kabla ya kukutana na Jesans.

"Wakristo hawaangamizi maadui zao," Matayo aliwakumbusha wenzake. "Na hiyo inajumuisha hata adui wetu mkubwa. waasi wa Yesu. Malipo ni kazi ya Mungu, wala sio yetu. Iwapo tumefahamu Bibilia Vyema, Dangchao atapata jeraha kubwa hatimaye. Labda ndio wakati atakopoingiliwa na shetani. Na labda yeye kwa wakati huu hana hatia kama vile mimi nawe."

"Labda ni sisi ndio twapasa kumpatia jeraha hilo," alipendekeza Neville. Twapasa kumpigania vita Mwenyezi Mungu kule Magedoni. Sasa iwapo twaweza kuua watu kwa niaba ya Mungu, mbona isiwe hivyo?"

"Iwapo waweza kumuua Dangchao kwa kusema tu neno, basi muue," Matayo alidhihaki. Neville kumbuka kwamba silaha yetu kule Magedoni yapasa kutoka kinywani mwetu. Silaha yetu ni ukweli. hakuna kupunguza hakuna kuongeza. Wanelewa?"

Maria na Elaine walisikiza kwa makini, bila kusema lolote. Walikuwa katika zile nyakati za jadi ambazo wanawake hawakupaswa kusema lolote, ila kukimya.

"Unafikiri vita hutoka wapi?" Matayo aliuliza, akisukuma wazo lake mbele zaidi.

"Kutoka kwa serikali zilizo na tamaa ya mafuta na utajiri," Neville alijibu kwa ujasiri. Alikuwa amesoma makala ya Rayford kuhusu mambo hayo.

"Hasaa. Kweli." Hilo sio jawabu alilokuwa akitaraji Matayo, hivyo basi alijibu mwenyewe. "Lakini wanapata wanajeshi kupigana kwa kushetanisha wapinzani." alisema. "Iwapo unaamini kwamba mpinzani wako ni nusu-binadamu, basi utajihisi umetosheka kufanya lolote. lakini Mungu hafanyi hivyo Neville. Yeye yuko na njia za kuwakabili wapinzani wake."

Mjadala ulimalizika punde tu Rayford alipoingia na gazeti mkononi.

"Mmesikia habari?" aliuliza.

Bila shaka hawakuwa wamesikia kwani jukumu la kupitia magazeti na kuleta habari lilikuwa la Rayford, ambaye alienda kila asubuhi kwenye mkahawa, na kisha kurejea na nakala ya bure. Lakini kwa wakati mwingine walifunga na kuitegea idhaa ya BBC, na alikuwa akjiitegea kabla ya kuongea.

Alitupa gazeti lile kwenye meza, ambapo kila mmoja angaliona kichwa chake:

Dangchao Auawa

Ripoti hiyo ilieleza jinsi Dangchao alikuwa amedungwa kisu na mshangiliaji alipokuwa akikagua ujensi wa sanamu kubwa ya Maria, Malkia wa Mbinguni, iliyokuwa ikijengwa mbele ya kanisa kuu la jimbo la askofu kule Yerusalemi. Jeraha la mduara wa sentimita tatu lilikuwa limedunga moyo wake.

"Alikufa alipofikishwa katika hospitali ya Chuo kikuu cha Hadassah," msemaji wa hospitali ile alitangaza.

Ripoti hiyo ilikuwa na maelezo kumhusu muuaji wa kujitolea, ambaye baadaye aliuawa na maafisa wa usalama baada ya shambulizi. Habari hizo pia zili dadisi kuhusu nani angalitwaa mamlaka ya Dangchao. Risala za rambi rambi zilizidi kupokelewa kutoka pembe nyingi za dunia, risala hizo zilimtambua Dangchao kama kiongozi mashuhuri na mkuu ulimwenguni, dunia ilikuwa imempoteza kiongozi mashuhuri kuliko mwingine yeyote.

"Je hilo sio jawabu kwa swali lako?" Matayo alimuuliza Neville, waliporejelea hali ya kawaida kutoka kwa mshtuko huo. "Iwapo Mwenyezi Mungu anataka kumzuia mtu, anaweza kufanya hivyo, bila kuzuiwa na wewe au mimi."

"Sasa ni nini kitatukia?" aliuliza Neville?" aliuliza Neville. "Je atapata uhai tena?"

"Ataweza iwapo yeye ni muasi wa Yesu," Rayford alisema. "Twapaswa kungoja. Hivi sasa tuombe kuhusu kile tunataraji kufanya. Leo ni siku ya 1,260 tangu kutiwa sahihi kwa ule mkataba."

Kundi hilo liliomba asubuhi ile na kujadili kuhusu muelekeo wa mambo. Hawakuona lolote jipya au mwelekeo usio wa kawaida. Rayford hakupata habaari sahihi?

Walitazama barua-pepe kutoka pembe zingine na hawakuona lolote likiendelea huko.

Irene alikuwa na shughuli kule London, kwa hivyo alipanda gari moshi mchana. Jioni alirudi na uso ulio guna.

"Je mlitazama barua-pepe asubuhi hii?" aliuliza Rayford kwa mshangao.

"Yeah. Mbona?" alijibu.

"Mmerudia tena tangu hapo?" aliuliza.

"Saa moja iliyopita nilituma bara-pepe kwa Chaim na kutazama mtandao," alijibu. "Mbona?"

Wasiwasi ya Rayford haikuwa kwa swali bali ni hali ya kutatanisha jinsi alivyouliza.

"Ulipata shida yeyote?" aliendelea.

"Yote haya ni ya nini?" Rayford aliuliza. "Kuna shida yeyote?"

Irene alieleza. "Nilisimama ili kulipia akaunti yetu pale Web Wonders. Polisi walikuwa kila mahali, bila kuwepo Web Wonders."

"Unasema nini, hakuna Web Wonders?" Rayford aliuliza.

"Hakuna kitu," Irene alisema. "Hakuna wafanyi kazi, hakuna afisi, hakuna jengo. Mabaki ya jivu tu, na yaliyokuwa matofali."

"Haiwezekani. Una uhakika ulienda mahali panapohitajika?" Rayford aliuliza, huku akisonga karibu na tarakilishi ili kujaribu anwani yake kwenye tuvuti.

"Hakika nina uhakika," Irene alisema. "Mimi huenda pale kila mwezi."

Neville alichagua huduma ndogo ya tuvuti kwa sababu ilikuwa ndio taasisi ya kipekee ya huduma za mtandao iliyokuwa ikikubali malipo kwa kutumia pesa mjini London. Irene alilipia akaunti zao kila mwezi.

Rayford alibonyeza ili kupata barua. "inaunganisha," alisema, huku wakijikusanya kando ya tarakilishi, na kusikiza mlio wa kawaida wa tarakilishi.

"Inajibu," Irene alijibu kwa mshangao. Walisikiza huku hayo makelele ya kuunganisha mitambo yakilia, na kadhalika kuashiria kwamba tarakilishi ilikuwa ikiunganika na mtambo mkuu kule Web Wonders.

"Wako na afisi nyingine mahali kwengineko?" Rayford aliuliza.

"Labda sifahamu," Irene alijibu. Mike ndio mwenyewe, na anafanya kazi hapo kwenye afisi iliyo makutano ya Clapham. Sijapata kumsikia akiongea kuhusu afisi nyingine."

Hapo tu, Neville aliwajulisha kutazama tarakilishi, ilikuw sasa inapokea mawasiliano na kiunganishi cha tuvuti kisichokuwepo!

"Tazama hapa!" alisema huku akigusa kio.

Ratiba ilionyesha kwamba Rayford alikuwa anapokea zaidi ya barua 200 katika ukurasa wake.

"Nimeangalia tu ukurasa huu saa moja iliyopita!" Rayford alishanga, Hatujawai pata kiasi kama hicho, hata wakati wa miezi sita." Alikuwa akiongea juu ya yale waliyopitia baada ya mkataba wa Hekalu kutiwa sahihi.

"Ni kweli tena!" Neville alieleza. Alitazama kila aina ya anwani zikichezacheza kwenye kio huku barua zikiingia kwenye ukurasa wa Rayford.

"Lakini zinatoka wapi?" Rayford aliuliza. Nini kilitukia kule Web Wonders? Unafikiri mamlaka inatukabili?"

Maswali hayo yalikuwa tu kebehi. Hakuna yeyote ndani ya chumba kile aliyekuwa na jawabu.

Ilichukua muda wa nusu saa kukusanya barua zile, huku hayo yakijiri, Neville alikuwa akiwaza jinsi ya kukabili barua nyingi kiasi hicho siku za usoni, iwapo zingaliendelea kuingia kwa kiwango hicho.

Rayford kwa upande mwingine alikuwa akiwaza iwapo wangalikimbia. Kulingana na wote, Huzuni Kuu ilikuwa imeanza. Ulikuwa ni wakati wao kukimbilia "Jangwa". Kilichotokea Web Wonder, kilikuwa ni dhihirisho la wazi kwamba utawala au mamlaka yalikuwa yamewapata.

Lakini waende wapi? Wapi mabawa ya kimiujiza kuwawezesha kupaa na kuepuka shida hii? Au ilikuwa tu kwamba walikuwa karibu kunaswa? Huduma yake ilikiwa imefikia kikomo?

Iwapo hitimisho lilikuwa limewadia, basi Rayford alikuwa tayari kupigana, sio kwa bunduki, lakini kwa ukweli. Kulikuwa na mengi yaliyokuwa yamejadiliwa kati ya wanachama wa makabila yale miaka tatu na nusu iliyopita. Sasa ulikuwa wakati wa kusambazia ulimwengu mzima.Iwapo angalisikizwa.

Baadaye usiku huo alikaa mbele ya tarakilishi. Hakufikiri sana kuhusu yale aliyoamini kuhusu Levi Xu Dangchao na utawala wake wa ulimwengu. Rayford alieleza kuhusu idadi ya herufi za jina la Dangchao, na kutabiri kwamba kiongozi huyo atafufuka, lakini watakachoona sio mwili wa binadamu. Itakuwa ni zombi.mzoga uliozingirwa na kukaliwa na Shetani mwenyewe.

Alitabiri kwamba utoaji wa kafara utakoma, na kwamba Dangchao atachukua mamlaka ya Hekalu, akijitangaza kwamba yeye atadumu. Baba Mtakatifu atatoa ombi kwa ulimwengu mzima kumuabudu Dangchao kama Masia wa Ulimwengu.

Yalikuwa ni matumaini ya ajabu, lakini Rayford alihisi kwamba hakuna muda wa kutosha, na alitaka kueleweka vyema kabla ya kunaswa. Ungalikuwa ujumbe wake wa mwisho duniani, na hata ikiwa alikosea katika maelezo yake mufti, alipaswa kupata ujumbe wake kuwafikia wale ambao angalishawishi: yaani iwapo Dangchao angalifufuliwa, angalikuwa yule Muasi wa Yesu aliyetabiriwa. Hakuna shaka. Angalikuwa ibilisi. Yeyote aliyemtumikia atakuwa ni shetani, iwapo walitaka kuona hayo au la.

Rayford aliona haja ya kumtumia Chaim makala yake kabla ya kuyachapisha kwenye mtandao. Alimuuliza Chaim kuweka kwenye ukurasa wake kwanza, ili ujumbe huo uweze kupatikana, endapo yeye angalinaswa au kukumbana na janga sawa na lilie lililopata wafanyi kazi wa Web Wonders. Chaim alitoa mapendekezo kadhsaa aliyoyakubali Rayford kabla ya kuchapisha.

Neville muda huo alikuwa akitazama msururu ule. Iwapo kulikuwepo afisi nyingine ya Web wonders na barua kuzidi kuingia kwa kiwango kile, basi walihitaji mashine ya kuchambua na kujibu. Alianza kwa kutunga barua ya kueleza watu kwamba hakuna haja ya kujibu, na kwamba wangalipata ujumbe wote walio hitaji kwa kuangalia kwenye mtandao. UKurasa utahaririwa kila siku bora tu ubakie kwenye tuvuti.

Iwapo watu walitaka kupata ushahuri kutoka kwa makabila kumi na mbili, basi walipaswa kumuomba Mungu ili awaelekeze jinsi ya kupata kuwasilisha barua zao. Hii ilikuwa ni kama kamari, na Neville akaomba Mungu kuwawezesha watu wanaostahili kuufikia ukurasa huo. Neville alitayarisha tuvuti ili barua zote zilizoanza na 7 kama herufi ya kwanza ikifuata na barua, ndizo zitakazo wafikia wanachama wa makabila kumi na mbili.ikitoa mojawapo ya herufi kumi na mbili zilizo sawa. Mbili kati ya tabaka za makabila hayo zilianza na J: Mike na Martin (tabaka la Kiyahudi) Matayo na Rayford (tabaka la Yosefu) watu waliotaka maelezo ya ukweli walipaswa kuandika Ju kwa Mike na Martin na Jo kwa Rayford na Matayo.

Barua ya Neville haikutoa maelezo kuhusu kile watu walihitaji kufanya ili kufaulu, iwapo utaratibu haungalizingatiwa, basi barua zao hazitapata kuwasilishwa. Ili baki kwa Mwenyezi Mungu kuwaelekeza watu walio na haki kile cha kuandika. Neville alielekeza watu kwenye ukurasa uliowafundisha jinsi ya kumtii na kumsikiza Mungu.

Hakuna aliyejua iwapo barua zitaeendelea kuwajia kwa kiwango kile, au iwapo wangalikuwepo kuzipokea.

Kwa sababu hii Neville na Rayford hawakulala usiku bali walilala mchana na Matayo na Irene kushika doria. Irene alifungua Redio kusikiza habari. Ukweli halisi ulikuwa kwamba kwa miujiza Dangchao alikuwa "ameamuka". Ripoti kutoka kwa Umoja wa Mataifa lilidhibitisha kwamba habari ya hapo awali iliongezwa chumvi, na kueleza kwamba Dangchao alikuwa anaendelea vyema baada ya kupokea matibabu katika Hospitali ya Hadassah, na alikuwa anapata nafu. Picha ilionyesha akitoka hospitalini huku hajafungwa sana kwenye jeraha.

Wakati huohuo, Dangchao alitangaza kwamba hali duni ya usalama iliyopelekea majaribio ya mauaji ilipaswa kutazamwa upya, na kufanya mabadiliko makuu katika Umoja wa Mataifa. Alitangaza Yerusalemi kuwa chini ya Umoja wa Mataifa, na kusema kwamba atatumia Hekalu kama makaazi ya "muda" na kama Makao makuu ya shirika hilo la dunia., kwa sababu eneo hilo ndilo lililokuwa salama mjini humo. Waandishi wa habari na vyombo vya habari vilikubali tukio hilo na kuunga mkono, kutokana na hofu iliyosababishwa na "mauaji ya siri". Hakuna aliyeuliza mbona uhamisho upelekwe Yerusalemi.

Baba Mtakatifu alinukuliwa kuunga mkono, huku akisema ulimwengu ulikuwa unakaribia dini moja, na ilikuwa bora iwapo dinio hiyo ingeshirikisha shirika kuu kama vile umoja wa mataifa. Kuwepo kwa Dangchao kwenye Hekalu ni ishara ya ule umoja, alisema.

Kulikuwepo pingamizi kutoka kwa baadhi ya makuhani wa Kiyahudi; lakini ajabu ni kwamba, kulikuwa na sauti za kuunga mkono. Wengine walisema kwamba Dangchao ndiye Masia aliyesubiriwa kwa muda mrefu. Kwa kiwango fulani alikuwa Myahudi, na alidhihirisha uwezo wake wa kuleta amani. Ilikuwa ni haki tu "mji wa Amani" ufanywe makaazi yake. Kuani hao ndio waliosikitishwa, hata hivyo Dangchao hakuwa tayari kutambua ukuani wao, kutokana na jukumu lake kwenye Hekalu.

Kwa yale makabila kumi na mbili, mtazamo wao ulikuwa tofauti. Kufikia saa za maankuli ya mchana Jumatano , wote kwa pamoja na wasimamizi wao walikuwa wamechukua tahadhari. Huzuni Kuu ilikuwa, kwa hakika, imeanza; ulinzi wa kikabila ulikuwa umekiukwa; na hawakujua mahali pa kuenda au kujificha.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika:

 

Watu wengi wamekosea kwa kuamini kwamba, wakati fulani siku za usoni, Mungu atadhihirisha nguvu zake kiasi cha kumtambua na kutofanya lingine ila kumuabudu. Kwa bahati mbaya, ukweli halisi sio hivyo. Lazima kuna nafasi ya shaka; na utabiri haukosi. Tazama utabiri kuhusu Yesu katika Agano la Kale. Hata sasa, baada ya miaka 2000, hakuna uhakika kamili katika sehemu nyingi.

Wengi wa walimwengu hawatajua kinachoendelea kiroho nyakati za mwisho kabla ya kurudi kwa Yesu. Hata wale watakao elewa watashuku baadhi ya utabiri na kukosa kuelewa, kama ilivyodhihirika kwenye sura hii. Lakini hapo ndipo wapaswa kuegemea nafsi zao.

Anachohitaji Mungu ni watu watakao muamini, kumtumikia na kumtumaini hata ingawa hawana jibu. Wale wafuasi 144,000 wanawakilisha haya. Mtu mmoja kati ya 50,000 atakayefanya kitu kifaacho, kwa sababu ki sawa, na sio kwamba wamelazimishwa kutenda.

Hata hivyo kitu kimoja tusicho paswa kufanya, ni kujaribu kutosheleza au kuharibu yaliyo tabiriwa. Sio kwamba hatuna uhuru wa kuamua, lakini ni kwa utabiri unatueleza yale yatakayo tokea kutokana na uhuru wetu.

 

 

16. Mashahidi Wawili

 

Alhamisi asubuhi, Rayford aliamua kwenda kujionea eneo la Web Wonders. Alipanda gari la moshi kuelekea makutano ya Clapham na kisha kutembea hadi eneo alilofahamu kwamba ni afisi za Web Wonders. Polisi walikuwa wangali kwenye eneo hilo, ingawa vifusi vilikuwa vimeondolewa. Watazamaji wachache walikuwepo, wakijadili kilichotukia. Rayford alijongea karibu ili kusikiliza habari kuhusu kilicho sababisha.

Watazamaji hao walijua machache kuhusu kilichokuwa kinaendelea. Lakini punde tu alipofika mahali hapo, Rayford alimuona mtazamaji mmoja akiongea na askari huku akitoa ishara. Hakutaka kuwatazama moja kwa moja, lakini ilionekana kwamba mtu yule pamoja na Askari walikuwa wakielekea upande wake, na yule raia alikuwa akionyesha kidole kumuelekeza. Rayford alichagua kutulia. Aligeuka na kuenda.

"Wee! wewe hapo! Simama hapo ulipo!" Bila shaka walikuwa wakimuambia Rayford, lakini kwa kuwapa mgongo alijifanya kama kwamba hasikii, na kuendelea kutembea. Hapo tu askari wawili walitokea mbele yake. Alikuwa ameshikwa.

Aligeuka na kuinama huku akijinyoshea kidole, huku akitafuta maneno yakusema, "Mnaongea nami?" kwa mudomo wake.

"Ndio, tunaongea na wewe, jinga!" mmoja wa wale polisi alisema huku akimchukua kutoka nyuma kwa kiburi.

Alisukumwa karibu na yule mjulishaji, na Rayford akamtambua kama Nuhu, aliyekuwa mwanachama wa kabila la Yosefu. Nuhu aliama baada ya mabishano zaidi ya mwaka mmoja uliopita. Alikuwa amekiri kwamba kundi hilo lilikuwa dhehebu lisilo la kawaida, na kwamba viongozi wake walikuwa a kiimla. Rayford alikuwa awali akimuona Nuhu kule Liverpool yalipokuwa makaazi ya idara ya ugawaji. Idara hiyo iliamishwa, na huo ndio uliokuwa mwisho wa kumsikia Nuhu, au kumuona Nuhu. hadi leo.

"Ndio, ni yeye!# Nuhu alisema.

"Mnaongea juu ya nini?" Rayford aliuliza.

"Je una kitambulisho?" afisa wa polisi aliuliza.

"La, kwa hakika sina," Rayford alisema kwa uhakika.

Hakuona haja ya kubeba kitambulisho kwa wakati huo. Hawataweza kumpata Irene na wenzake iwapo hawakujua alipoishi.

"Unajua lolote kuhusu kulipuliwa kwa jengo hili?" afisa wa polisi aliuliza

"Mimi? La," Rayford alijibu, kwa kushangaa na swali hilo. Mbona walikuwa wakimuuliza yeye kuhusu bomu ilihali ni wao walio tekeleza?

"Nitakupeleka hadi kwenye kituo kwa maojiano," afisa wa polisi alisema.

"Nina shtakiwa?" Rayford aliuliza.

"Sio iwapo hautakuwa mkaidi."

"Sielewi. Nitajua nini kuhusu yaliyotendeka hapa?" aliuliza.

"Watu sita walifariki wakati wa mlipuko kwenye jengo hili siku tatu zilizopita. Tunaamini kwamba unazo habari kuhusu mlipuko huo. Unalolote la kuficha?"

Ilikuwa ni ajabu. Mamlaka hayo yaliamini kwamba Rayford Strait aliharibu Web Wonders? Ilionekana kama kwamba Nuhu aliletwa hapo kutambua wafuasi watakao fika pale. Rayford alikuwa amejiingiza kwenye mtego.

Kulikuwa na mengi yasiyo leta maana sawa. Polisi hawakuwa na anwani yake, ambayo ingalikuwa katika mojawapo ya orodha zilizokuwa Web Wonders. Na iwapo kulikuwa na afisi nyingine kwengineko, basi aidha hawangalitambua. Hata hivyo wangali pata maelezo kutoka kwa nakala za orodha. Rayford alikuwa mashakani, lakini maskani ya Neville na Maria yasije kuvumbuliwa.

"Kwenye gari, gaga wewe!" mmoja wa polisi aliamuru, na kumsukuma kutoka mgongoni.

"Eee, pole pole bwana!" alilalamika, akianguka chini na kujipanguza.

"Hii sio sarakasi, rafiki!" askari alijibu "Fanya tunavyokuelekeza."

"LA!"

Ilifanyika tena. Hatukuwepo na tahadhari wakati huu. Rayford hakuhisi njaa. Neno lilimjia tu kutoka kinywani alipokuwa ameketi.

Aliposema lile neno "La", miale ya moto iliwazingira wale polisi watatu. Miali ilikuwa kali sana na kuwajeruhi kushinda ilivyokuwa kule Neville.

Rayford alijiona kama aliye mashakani asipokimbia. Punde tu baada ya kutamka neno hilo aliruka na kukimbia. Alikuwa amefikia kona kabla ya umati kuona yaliyotendeka, hata hivyo hawakutaka kumkimbiza mtu anaye pumua miali ya moto.

Wale maafisa wengine wa polisi walikimbia kuwanusuru wenzao waliokuwa wakiteketea, lakini walichelewa. Askari watatu walikuwa wameuawa na mwanakombora. Askari hao hawakutaka kujumuishwa kwenye orodha ya Rayford, basi hawakuona haja ya kumfuata. Walipiga simu kuomba msaada.

Rayford alikuwa amefika katika makutano ya Claoham na kuchukua gari moshi kuelekea Guildford. Alikuwa na hofu, huku akiofia kwamba anaweza kuwa anaandamwa. Alikuwa pia akisumbuliwa na aliyowatendea wale askari watatu. Na sasa ilikuwa pia habari ya wale watu sita waliokufa kule Web Wonders. Nini ilikuwa ikiendelea? Alikuwa ameshiriki kuwaangamiza?

Ndani ya nafsi yake alielewa jibu. Alikuwa najibu yapasa miaka tatu na nusu iliyopita, lakini hakutaka kufikiri juu yake. Wakati wengine waliongea juu ya hayo, alibadili mazungumzo.

"Siwezi kumudu," angalisema. "Siwezi kufanya hivyo sasa, nitangoja hadi nifike mbinguni kupata maelezo." Alikuwa akiongea juu ya ule mlipuko uliotokea kwenye sebule ya Neville miaka tatu na nusu iliyotangulia.

Bibilia inaarifu kwamba wakati mwisho wa kipindi kile cha miaka tatu na nusu, tutakuwa na "Mashahidi Wawili" ambao watawindwa na utawala wa wakati huo kote duniani. Mitume hao wawili watakuwa na uwezo wa kuwakabili maadui zao kwa miale ya moto kutoka kinywani mwao. Watu wengi walitamani na kutumai kuwa manabii hao, lakini Rayford alionekana kuwa na sifa walizokosa wale wengine. Askari watatu katika makutano ya Clapham walikuwa tayari wamekufa kutokana na ushahidi wa sifa hiyo.

Rayford alipowasili kule Guildford, aliwasukuma wenzake na kuelekea moja kwa moja kwenye tarakilishi, alipomtumia Chaim barua iliyokuwa na alama "Dharura". Ndani yake alimuarifu Chaim kukatiza mawasiliano kupitia kwa huduma za tuvuti zingine ila tu kuunganisha na mtandao wa Web Wonders.

Kwa bahati utawala haukuweza kupata njia ya tuvuti aliyotumia Chaim. Akikatiza mawasiliano kule Australia, hawataweza kumpata huko. Watu hao wawili watakuwa wakiyaweka mayai yao kwenye kapu moja, lakini lilikuwa ni kapu lililotunzwa kimiujiza.

Lazima kulikuwa na afisi nyingine za Web Wonders ambazo hazikuweza kutambuliwa na mamlaka, au Mwenyezi Mungu aliandaa tuvuti yake kuwaunganisha makabila kumi na mbili. Rayford aliamini hivyo.

Kisha akarejelea dhamira kuu ya barua-pepe.

"Lazima nijue," aliandika, "Iwapo umepata kuona miale ya moto kutoka kinywani mwako unapoongea. Kuashiria iwapo wewe yu anayedhani yu, utajua ninacho sema."

Saa chache Rayford alitazama ukurasa wake kwenye tarakiliahi na kupata majibu.

"Ndio nimepata," ilisema. "Sasa tuende wapi kutoka hapa?"

Tuende wapi? Rayford alifikiri. Alikuwa amejiuliza hhivyo yapata wiki moja sasa. Orodha ya maswali ilikuwa ikongezeka kwa haraka kuliko majibu.

Walakini, iwapo yeye na Chaim walikuwa wale Mashahidi wawili, basi hawangaliweza kunaswa kwa urahisi. Kulingana na Bibilia, walikuwa na wakati mwema katika hiyo miaka mitatu na nusu, ili kuwafanya wasikike ulimwengu mzima, na kutumia wakati huo bora.

Kitu cha ajabu, kama alivyofikiri Rayford, ni kwamba watu wengi walitaka kutekeleza jukumu hilo (Hospitali za Akili punguani zilijaa watu kama hao) na kwa karibu, kazi ya "mashahidi wa nyakati za mwisho" haikuwa na kiinimacho walicho husisha watu wengi. Kwa sasa Rayford alikuwa akitambulika kama jitu linalopumua miali ya moto.

Chakutia hofu ni kwamba utambulizi huo ulikuwa karibu na ukweli.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Marejeleo kuhusu "Mashahidi Wawili" au Mitume (nyakati za mwisho) Wawili, yanaweza kupatikana kutoka kitabu cha Ufunuo wa Yohana 11:3-2. Wamelinganishwa na Elija na Musa, katika Agano la Kale. Yoyote atakaye kuwa miongoni mwao, bila shaka watakuwa na nguvu au uwezo wa ajabu, ili kutimiza mamlaka yao. Katika kitabu cha Ufunuo wa Yohana tunaelezwa kwamba Mitume hao wawili watatabiria ulimwengu kwa siku zile 1,260 za mwisho (Miaka mitatu na nusu au miezi 42) wa miaka ile saba kabla ya kurudi kwa Yesu.

Kwa sababu ni kawaida kwa watu wendawazimu kudai kwamba hao ni "Mashahidi", makanisa mengi yamekatisha maongezi ya Mashahidi Wawili. Lakini wale halisi hawapaswi kudanganywa na wasio wa kweli. Kuwepo au kokosa kwa wenye akili punguani, tutakuwa na mitume wawili nyakati za mwisho wakieneza ukweli kwa walimwengu.

Ni dhahiri kwamba ni mashahidi wawili na manabii wa uongo nyakati za mwisho wataendesha shughuli zao bila ushirikiano.kwa sababu tamaa zao na kujitakia makuu hakutaruhusu kushirikiana na kusikiza wenzao.

Kuna usemi mmoja katika Bibilia kwamba kila kitu cha kiroho kuweza "kudhibitishwa kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu", (Matayo 18:16, Wakorintho wa pili 13:1, Timotheo wa kwanza 5:19, na Wahebrania 10:29)

Iwapo itatendeka kwamba mmoja lazima atekeleze kibinafsi, basi kutakuwa na dhibitisho kamili kwamba nguvu za ajabu zitajulikana kama "shahidi" wa pili. (Yohana 5:36)

 

 

17. Dangchao

Levi Xu Dangchao alikuwa akijadili mipango na Baba Mtakatifu Pius XIII, aliyekuwa amehudumu kwa miaka mingi kuliko Dangchao aliyekuwa Katibu wa Umoja wa Mataifa. Walikuwa katika makazi ya kibinafsi ya Baba Mtakatifu Yerusalemi.

"Kichwa chatarajiwa kuwekwa kwa sanamu iliyo mbele ya kanisa kuu la jimbo la Askofu Kesho asubuhi. Ni kweli?"

"Ndio hasa," alijibu Pius. "Jana kilimiminwa kwa kalibu, na kitawasilishwa leo"

"Nina kichwa cha badala kwa sanamu" Dangchao alisema kwa kiburi.

"Kichwa kingine?" Baba mtakatifu aliuliza kwa mshangao. "Wamaanisha nini? Kwanini tuhitaji kichwa kingine?"

"Ninamaanisha kwamba niko na kichwa kingine kilichoandaliwa kwa sanamu, nataka kitumiwe badala."

"Lakini mbona? Nini mbaya na kile tulichonuia kutumia?"

"Nini mbaya?" Dangchao alijiuliza kana kwamba anatafuta jawabu. Aliangalia nje ya dirisha kwa muda, Kuongeza sarakasi kwa yale yatakayotokea, aliongeza tena kimzaha na kwa upole. "Nini mbaya na kichwa kilichoidhinishwa na Pius?"

Aligeuka na kumuangalia Baba Mtakatifu Pius. Uso wake ulibadilika na kukunjamana. Sauti yake ilikuwa nzito na ya kukwaruza.

"Nini mbaya kwani sio mimi!" aliguna.

Pius alirudi nyuma kwa uoga. "Xu! Nini kimetendeka kwako?" aliuliza. " Uso wako.!"

Dangchao alipoa na uso wake kurudia hali yake nzuri ya upole.

"Wapenda hiki zaidi?" aliuliza.

"Ulinishtua," akasema Baba mtakatifu, akijiliwaza kwa kuona Dangchao akirudia hali ya kawaida.

"Hilo ndio lengo langu," Dangchao alijibu. "Watu wengi huniamini, Pius. Wewe waniamini au sio?" Pius alitingisha kichwa kukubali shingo upande bila hakika.

"Ningalipenda wewe uniogope," alisema Dangchao. "Ningalipenda wote waniogope.

Na itakuwa hivyo, " aliongezea baadaye.

Pius alijaribu kurejelea mazungumzo ya awali. "Haya yote yanahusu nini sanamu ya Bikira Mtakatifu?" aliuliza.

Dangchao aliongea kwa unyenyekevu, kama kwamba anamuongelesha mtoto. "Yote ni kuhusu sanamu, Pius. Waona, sio sanamu ya Bikira Mtakatifu bali ni sanamu yangu."

"Sijui kama hiyo itafaa, Baba Mtakatifu alijibu. Kanisa halioni shida kwa kutengeneza sanamu za mitume; na Dangchao atatunukiwa hivyo siku moja. Lakini sanamu hii ingelikuwa mojawapo ya sanamu kubwa iliyowai kutengenezwa na kanisa, ilikuwa haki kumtunuku Malkia wa Mbinguni, na wala sio katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, hata ikiwa ni kiongozi anayetambulika na kuheshimiwa hapa ulimwenguni.

"Wataka kuiona sura yangu nyingine tena?" Dangchao aliuliza, Kwa mara nyingine akiongea na Baba Mtakatifu kama kwamba anamkaripia mtoto. "Fahamu sijakuuliza. Ninakuambia.

"Wewe umepata kanisa kuu la kiaskofu na makao hapa Yerusalemi. Hata hivyo nahitaji makao hapa vilevile; na itakuwa jinzi nitakavyo."

Basi, baada ya muda, sura ya ukali na uchovu ikaonekana. Kulikuwa na hali ya kutatanisha chumbani humo, Baba Mtakatifu Pius alikumbwa na uoga kiasi cha kuona na kushika.

"Je waelewa?" aliguna kiumbe Dangchao.

"Ndio.ndio! Ninaelewa," Pius alisema kwa hofu tele.

Lakini hakuelewa. Angalielezea ulimwengu vipi?

"Utaona," Dangchao alisema, wakati swali lilipoulizwa baada ya kurejelea hali yake ya kawaida. "Watakubali, jinsi ulivyokubali. Labda hawatafurahia, lakini watakubali. Na watakubali mengi kabla ya hatujamaliza."

Dangchao aliendelea mbele kumuelezea Baba Mtakatifu jukumu la Pius katka utawala mpya.

"Lengo kuu la dhehebu kwa kawaida ni kutilia mkazo uhalali wa mamlaka ya utawala," Dangchao alieleza. Na jukumu lako sio kinyume.

"Kitu ambacho kimetendeka kwa wakati huu wa mpito ni kwamba nitatoa vazi. Nimechoka na ukafira. Nataka watu wanione jinsi nilivyo, na pia nataka waniogope".

Ndio mwanzo ilikuwa inamfikia Pius kwamba anaongea, ana kwa ana na yule asyependa Kristo. Kanisa halijatilia mkazo mambo kama haya. Hawataki kutafakari juu ya wanautamaduni. Kwa sasa Pius alikuwa akikabiliwa na ukweli halisi; hakuwa tayari kukabili tukio kama hili.

Kwa hivyo alikuwa amedanganyika kuelekea Yerusalemi. Alikuwa huku kwa minajili ya kuweka wakfu utawala wa mtu huyu mkatili. Iwapo Dangchao kweli alikuwa mwanaume.

Lakini Pius hangerudi Roma. Hata akijaribu, je Dangchao atamuachilia? Alikuwa amehisi sekunde chache za hofu ambayo Dangchao alikuwa amemtia kwa kuwepo hapo, na kufahamu kwamba jitu hili halingalimwachilia kwa urahisi. Alikuwa mtumwa wa Dangchao, na hatukuwa na njia yeyote.

Kwa sasa hivi hakua na namna bali kufanya vile ilivyotakikana.

Kile kichwa cha sanamu kiliwasili, na Pius akasumbuliwa sana kuona sura hiyo ilikuwa uso wa Dangchao na wala sio ule alionuia. Ama uso huo wa kijificho ulikuwa wa hakika?

Dangchao alijibu swali hilo baadaye siku iliyofuatia walipokuwa na Pius.

"Ili kufikia mahali nilipo hivi sasa," alieleza, "Nimeweza kuvaa barakoa za kila aina. Na zote kuonyesha mtu mzuri.

"Lakini mimi sio mtu bora. Sitaki hata watu kufikiri mimi ni mtu mzuri. Nataka waniogope. Nataka niweze kuwaongoza. Na ninataka kutekeleza hayo bila kujifanya mimi ni mzuri.

"Waona Pius, huo ndio ukweli halisi wa kuwa katika mamlaka. Mtu yeyote anaweza kuongoza watu wanao muamini. Lakini nataka kuwatawala watu wanao niogopa. Waniogopa, au sio?"

Pius hakuwa na lakusema, ila kukanganya azimio lake la awali la imani yake kwa Dangchao na kutikisa kichwa kuhafiki uhusiano mpya na kiongozi wa dunia.

"Ndio waniogopa," Dangchao alisema kwa tabasamu. "Watafuta njia ya kuepa. Lakini bila shaka hakuna, au sio? Utaenda wapi? Nina tawala ulimwengu, niko na uwezo huo hata ikiwa watu kama nyinyi hamtaki.

"Nimeweza kufaulu kufanya haya kutokana na alama. kutokana na alama," alijivuna.

Mtakatifu Pius alionekana kama aliye zuzuliwa, lakini hakudhubutu kuuliza swali lake. Hata hivyo, Dangchao alibahatisha alichokuwa akifikiri.

"Swali lako iwapo alama ni yangu?" aliuliza. "Ni sababu unaona tu alama na kusahau ukweli ulio nyuma yake. Uso wa Dangchao sio sura yangu, Pius. Umeona mimi halisi. Je ninafanana na Dangchao? La hasha. Nilichukulia mafao ya mwili wake.

"Oh, kwa hakika alishirikiana nami vizuri kabla ya kufa kwake, kama wewe, na waliokutangulia, mmefanya hivyo tangu jadi. Ilikuwa tu baada ya kifo chake cha ghafla ndio nilichukua mwili wake.

"Lakini alama. Nimekuwa nikifanya kazi zaidi ya miaka elfu. Ni ishara ya utu kunitegemea, na inaelekea kukamilika. Ndio Pius, ni alama yangu na, ninatawala ulimwengu kwa alama hiyo."

Dangchao alimlazimu baba mtakatifu kukiri kwamba ulimwengu mzima unamuabudu, na kwamba waweze kuabudu sanamu yake. Ile sanamu ya Maria mbele ya kanisa kuu la jimbo la askofu ilitakiwa kubadilishwa na kuwa sanamu ya Dangchao au mnyama aliyekuwa Dangchao.

"Usijifanye mtakatifu," Dangchao alisema, wakati Pius alisema kwamba hivyo ni kumtukana Mwenyezi Mungu. "Mmekuwa mkimuabudu Maria kwa karne nyingi, na yeye sio mtakatifu jinsi nilivyo. Misa haikunung'unika kuambiwa kwamba Maria ni mamake Mungu? Iwapo uliwafanya kuamini hivyo, mbona usiwaambie kwamba umepata Ufunuo wa Yohana kwamba mimi ni Babake Mungu?"

Kwa hayo Dangchao aliangua kicheko cha kishetani kilicho mugandamiza Baba mtakatifu Pius XIII kwenye mifupa.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

Ufumbuo kuhusu `Joka la mabawa' kufukuzwa kutoka mbinguni. (Ufunuo wa Yohana 12:7-9) Joka hilo laja ulimwenguni na kuanzisha vita kati ya Kanisa, au "Bi arusi" wa Yesu. (Ufunuo wa Yohana 12:12-13) "Joka" hili kwa hakika ni shetani, aliyekuja kupiga Mungu vita na wote wanaomuamini Mungu. (Ufunuo wa Yohana 13:5)

Joka hilo litachukua umbo la mwanadama aliyepata "Jeraha la kutisha". Mwili huu ulio na shetani ndani yake huitwa "jitu". (Ufunuo wa Yohana 13:3)

Ibilisi huyu anasaidiwa na "Manabii wa Uongo" (Ufunuo wa Yohana 16:13), wanaopelekea ulimwengu wote kumuabudu ibilisi na sanamu zote alizojenga. (Ufunuo wa Yohana 13:11-14)

Kama vile tutakavyoona kanisa lisilo la kweli likiwa sambamba na Kanisa la Mungu ndani ya miili ya wateule, ndivyo hivyo tutakavyoona manabii wa uongo wakiwa sambamba na kufanya kinyume na Manabii wa kweli siku za mwisho.

Huku waamini wa hakika wakimuamini Mungu wasiye muona, wale wasio wa kweli wataabudu miungo na sanamu, na kuweka imani yao kwenye alama (au pesa) kukidhi mahitaji yao. (Waefeso 5:5)

Jambo la kujivunia kuhusu wale wasiomuamini Yesu, ni kwamba, yote hayo yatafikia kikomo. watu watalazimishwa kuchukua muelekeo, upande mmoja au ule mwingine. Hakuna mapatano, masikilizano au kutokuwa na hakika. Hakuna kuita uovu wema na kuita wema uovu! Shukuru Mungu kwa hayo.

 

 

18 INJILI

 

Alipokuwa amerejelea hali yake ya utulivu, akipanguza machozi yaliyokuwa yakimbubujika, wakati aliangua kicheko, Dangchao alizungumza zaidi kwa Baba mtakatifu.

"Nitahitaji usaidizi wako na jambo jingine dogo", alisema.

Tunalo dhehebu ambalo limekuwa likisema vitu vibaya kunihusu miye na serikali yangu. Tumejaribu kuwaandama kwa Mtandao, lakini waliharibu nyumba nzima iliyokuwa na hifadhi ya mtambo wa mtandao kabla ya kunakili anwani yao. Wanajiita Jamii ya koo kumi na mbili. Una habari gani kuwahusu?"

Kanisa liliweka rekodi kubwa kuhusu makundi yote mapya ya kidini, katika afisi zake kule Roma, lakini mbona, aliwaza Pius, amsaidie Dangchao? Je, iwapo watu hawa wangesaidia kumsimamamisha huyu mtu mbaya? Wangalifanya hivyo, basi angaliwasaidia kuliko kumsaidia Dangchao.

Katibu mkuu alipumua kwa ndani huku akichukua muelekeo mpya ambao Pius angekuwa akifikiria. Angalilazimika kucheza mchezo wa Pius kwa mara nyingine, kama alivyokuwa amefanya mara nyingi miaka iliyopita, ndiposa ana uwezo kwa Baba mtakatifu.

"Lolote lile unaloweza kufikiri kunihusu", alisema kwa ukarimu.

"Ukweli wa mambo ni kwamba hili ni dhehebu baya sana."

Tayari wamewaua watu tisa ambao tunajua na tuna habari kuwa kuna wengine ambao wameuawa kule Australia pia. Pius tafadhali! Ungekuwa unasaidia ulimwengu huu iwapo ungalitusaidia kuwasimamisha"

Pius alifikiria kwa muda kisha akaamua kuwa ikiwa angalikuwa anaelekea kuwa bingwa, hii isingalikuwa sababu nzuri au wakati mwafaka kuchukua hatua. Angalimsaidia Dangchao mara hii, angeshinda kwa kumpendelea. Basi angeweza kutumia hayo mapendoleo kupata uzuri zaidi wakati mwingine.

Dangchao alitabasamu. Uwezo wa kufurahisha tangu kitambo haukukosa kufaulu. Mfanye aendelee kuchelewa na angeweza kumkabili milele.

Kwa muda wa saa moja na nusu, Pius alikuwa na habari kamili kuhusu ndugu kumi na mbili kupitia kwa barua-pepe kutoka Roma, lakini alikuwa na usaidizi mdogo kwa wote wawili.

Wadadisi wa Kikatoliki walikuwa na jarida ndogo kutoka siku za Jeseni ambalo lilikuwa na jina la Reinhard. Hata hivyo, karibu habari yote waliyokuwa nayo kuhusu vuguvugu la koo kumi na mbili, ilikuwa inapatikana kwa Mtandao wa koo kumi na mbili.

Licha ya majaribio ya kamati mpya ya kanisa kuhusu makundi, kuwashawishi wa Jesani halafu koo kumi na mbili kutoa habari zao za ndani, hatukuwa na majibu kutoka kwa Reinhard, Rayford au Chaim. Hata majina yao hayakujulikani kwa sababu Rayford na Chaim walizoea kutoweka sahihi kwenye barua. Kamati haikuwa imepata kitu chochote hatari katika yale waliyokuwa wakifunza, kwa hivyo kamati haikufafanua zaidi. Tulikuwa na waliosema kuwa vuguvugu lilikuwa kubwa, kufikia idadi ya mamilioni, lakini kuna wengi walioamini kuwa hii ilikuwa ni ndoto, iliyosababishwa na watu waliotaka kutoa wazo kuwa kundi hilo lilikuwa kubwa kuliko lilivyokuwa. licha ya hayo hapakuwa majengo, hatukuwa na anwani za posta, hapakuwa kumbukumbu za mikutano, hapakuwa majina ya viongozi au wafuasi kando na Reinhard na wachache waliokuwa wafuasi mbeleni. Ilikuwa ni ukweli kuwa walitengeneza maandishi mengi, lakini maandishi yao yalipeana tu anwani ya mtandao.

"Tumeweka baadhi ya watafiti wanaotumia Tarakilishi walio bora ulimwenguni kwa kazi hiyo, na wao wote wamekwama".

Dangchao alilalamikia Pius walipokuwa wamemaliza kusoma ripoti kutoka Roma.

"Kila kitu kinaonyesha kwamba mtandao unashangaza, mtambo wao haupo lakini mtandao wao unafanya kazi. Ni kama hatuna maarifa ya kusimamisha.

Hata hivyo wanamgambo wa koo kumi na mbili walikuwa wamezunguka kwa kasi sana. Kasi hii iliongezeka kwa miezi michache iliyofuatia. Kila wakati, habari nyingine kuhusu Dangchao kutoka kwa vyombo vya habari ilijitokeza, Maelfu zaidi wangalitembelea mtandao wa koo kumi na mbili ili kupata habari motomoto kutoka kwa wale mashahidi wawili kuhusu yaliyokuwa yakiendelea.

Je, Dangchao alikuwa ameonyesha ujasiri kupita kiasi? kuashiria kwamba vyombo vya habari havikujua jinsi ya kuitikia kwa ripoti kuwa Dangchao alikuwa mbabe, au jambo jingine lolote jeuri kuwa yeye na Baba mtakatifu Pius walikuwa wanaelekea Yerusalemi.

Ile sanamu ya kuogofya na kile kichwa cha gargoyle na kiwiliwili cha kike, ikidaiwa ni sanamu ya Dangchao, ilishangaza ulimwengu, lakini ilikuwa tu mwanzo wa maajabu na mishangao mingine.

 

Dangchao alirarua patakatifu pa utakatifu kutoka kwa hekalu, na akajiwekea pale kiti cha enzi akalie huku akiabudiwa na kutamaniwa na uma. Aliwaalika watu wa dini zote na wale wasiokuwa na dini waje kumuabudu, kwa hivyo aliharibu uhusiano wake na viongozi wa kiyahudi waliotarajia kuwa angekuwa mkombozi wao.

Alisisitiza kwa kutoa burudani kwa wageni wake na chaguo lake la burudani lilikuwa la kufukuru waziwazi. Kwanza ilikuwa nyimbo ya kumsifu yeye kama mkombozi wa ulimwengu, kisha nyimbo hizo zikaanza kumkejeli mungu halisi. Wachezaji waliletwa, ambao walizidi kuashiria ngono katika shughuli zao. Madawa kali ya kulevya yalitolewa bure kwa wageni. Katika muda wa miezi chache tu, Dangchao alikuwa amejumuisha vitendo vya ngono hadharani na matendo mengine ya kutia najisi katika mpangilio wa hekalu la kiyahudi.

Lakini jambo la kushangaza kwa yote ni kwamba, watu walikuwa wanaikubali. Kwa mfano alikuwa ametabiri kuwa hata wale waliochukia matendo yake walikuwa wadhaifu sana kwa tabia na hawangeweza kumpinga.

Kulikuwa na wale walioenda kumuabudu kwa wingi na kushiriki katika sherehe zake zilizojaa kelele na ulevi, kwa furaha iliyokuwa wazi. Miongoni mwa watu walio hudhuria walikuwa wanadiplomasia, na watu walioheshimiwa sana kuonekana katika mojawapo ya sherehe najisi za Dangchao.

 

Ilikuwa imeripotiwa kwamba katika baadhi ya matendo makuu yaliyoendeshwa kwenye hekalu, umbo lake lote lingalibadilika kisiri na watu wangalifahamu mara moja kwa hofu baadhi ya nguvu za kiajabu alizokuwa nazo.

Vyombo vya habari, ingawaje viliduwaa, havikuwa na nguvu au uwezo wa kufanya chochote ila kutangaza yaliyoendelea kama kwamba ilikuwa tabia ya kawaida kutoka kwa kiongozi wa ulimwengu. Dangchao aliyeonekana kuwa na uwezo wa kufanya kazi siku nzima na kusherehekea usiku kucha, alikuwa na benki na washiriki muhimu wa umoja wa mataifa mfukoni mwake. Kati ya hizi jumuiya, aliumiliki ulimwengu na wala hakuna yeyote aliyedhubutu kumpinga.

Hata, hivyo, msimamo wake wa hadharani kumpinga Mungu na majaribio yake ya kuchukiza kwa wepesi, ndio iliwafanya mamia ya maelfu ya watu kutafuta wasia wa koo kumi na mbili na maelezo. Hapakuwa na taashishwi yoyote zaidi kuhusu alikotoka Dangchao. Alikuwa mpinga Yesu kamili aliyedhihirisha uovu. Neno lilisambaa kote ulimwenguni kuhusu mtandao wa kumi na mbili. Anwani yake ilipakwa (chini ya giza) katika kuta na mabango popote pale waumini 144,000 wangepata nafasi ya kujaa.

Kwa hivyo, watu walipoona yaliyokuwa yakitendeka Yerusalemi wangaliwageukia Rayford na chaim kuwafafanulia. Kwa muda mfupi, hakika mamilioni ya watu walikuwa wakitembelea tuvuti au mtandao ambao ulikuwa kiwasilishi rasmi cha mashahidi wawili wa Mungu wa siku za mwisho.

 

Watu wachache walikuwa wamegundua ishara ya siri katika anwani pepe ya Neville na walikuwa wameweza kuwasiliana kwa barua moja kwa moja na koo. Watu hawa walikuwa wanashugulikiwa kibinafsi. Wengi wao walikuwa hawajapata alama kwa hivyo wakachukuliwa haraka kwa ushirika, kwa dhana kuwa mungu alikuwa amewakinga kutowekwa alama na pia alikuwa amewezesha kuwasaidia kugundua ishara ya siri ya anwani-pepe. Kwa kuzingatia dhana hii, watu hawa hawakuwa tisho kwa usalama.

Kati ya ishara ya siri ya anwani-pepe na kukosa jina kwa mtandao, wale 144,000 hakika walikuwa wametorokea 'jangwani' mwa usalama kutoka kwa watawala. Mungu mwenyewe alielekeza wale wangaliowafikia, na ulimwengu uliosalia ulifungiwa nje.

Mbali na wachache waliotawanyika na wengi katika mashambani na wasiostarabika vijijini mwa ulimwengu wa tatu, hakika, kila mmoja ulimwenguni alikuwa amepolea alama hadi wakati huu. Ilikuwa vigumu kufanya biashara bila alama hiyo. Wale koo kumi na mbili ambao hawakufaulu kupata kodi ya bure kutoka kwa marafiki binafsi katika jumuia, walikuwa wakilazimishwa kukaa kwa njia katika mitaa au kwenye mahema na kwa makaazi mengine ya dharura. Lakini kwa jumla walikuwa wakiishi bila matatizo yasio ya lazima, kwa kutumia sheria ya kuomba, kubadilishana na kuiba mahitaji ya kimsingi ya maisha katika huu mpangilio mpya wa dunia ulio muovu na wazimu.

Watu waliokuwa katika shida kuu ni wale waliokuwa wakiwasiliana na koo kumi na mbili kwa kukosa matumaini. Yale waliyokuwa wamesoma kuhusu ile laana juu ya wale waliochukua alama ilikuwa hakika imewaweka katika hali ya kukosa imani kiroho. Walikosa mbinu yoyote ya wokovu, na walikuwa wakiishi katika dunia iliyokuwa inakua haraka katika uovu kila siku.

Dangchao alirudisha michezo ya kitambo ya waRoma, ile ya kupigana hadharani na watu wengine au wanyama ambapo wapiganaji walipigana hadi kifo.

Pia alikuwa amepanga kuonyesha mateso ya hadhara na mauaji huko Yerusalemi kupitia kwa kama burudani. Lakini watu wengi ambao hawakuwa wamemfikiri Mungu kwa dhati awali, walikuwa wanachukizwa na haya yote na hawakutaka.

Kwa hivyo, Chaim na Rayford walitoa mpango wa wokovu uliokuwa umegusiwa katika ujumbe kwa wale 144,000. Ulikuwa ndio ujumbe tangulizi kwenye mtandao na kushtua ulimwengu.

Haya ndiyo aliyoyasema:

"Mpango wa Mungu wa wokovu si tofauti na vile ilivyokuwa. Unahitajji kumpokea Yesu Kristo kama Mwana wa Mungu na pia kama tegemeo la pekee la wokovu".

"Tofauti (Kwa wale wanaojua kitu fulani kuhusu yale yaliyokuwa yakichukuliwa kuwa Ukristo) ni kwamba hatuzungumzi kuhusu kujisingizia katika imani, wakati huu. Kumpokea Yesu ni maana ya kupokea kila alilosema. Mafundisho yake ni sehemu muhimu ya mpango wa Mungu wa wokovu kwako. Soma mafunzo yake na utagundua kwamba anatarajia imani kamili. Kanuni zake ziko juu lakini anachopeana ni uzima wa milele. Hakuna gharama iliyo juu kwa hayo."

Rayford alieleza kwamba kusulubiwa kwa Yesu msalabani, kulipelekea kutoa wokovu kwa yeyote aliye hitaji; lakini haikumpasa Yesu kuchagua yeyote. Alikuwa akiangalia viwango fulani.

"Mengi ya madhehebu yenu yamefundisha kwamba Mungu wa Upendo hawezi kuweka viwango, kutaka kwa lazima au kuweka "zawadi" kwa yale anayotoa," alisema. "Lakini wamewapeleka wapi? Wamewasukuma kwenye ukingo wa kuangamia. Yale waliyofundisha yalisikika kama 'habari njema' kwa wakati ule, kwa sababu ilikuwa rahisi. Lakini imebadili kuwa janga kuu.

"Kinyume na hayo, injili aliyofundisha Yesu ilikuwa ukweli halisi na habari njema, hata iwapo haikuwa rahisi. Ilikuwa ni habari njema kwa sababu ujumbe huo ulijaribu ulifanya yale tuliyo puuza katika maisha. Aliona upuuzi na udhaifu wetu. Aliona kwamba , kwa matukio yanayotokea hivi sasa au la, siku moja utaaga dunia, na kushtakiwa kwa kukosa kufuata Mwenyezi Mungu. Alijua kwamba zawadi aliyokuwa akitoa. msamaha, na maisha ya milele katika nchi ilyo nzuri, ya kupendeza na kutosheleza kuliko ulimwengu huu wa sasa.

"Je ni dhamana gani anayouuliza? Anauliza uwache yote, yaani utoe kila kitu ulicho nacho. utajiri wako, maisha yako, jamii yako na marafiki na hata maisha yako.

Uchukue ama uwache. Hiyo ndio dhamana. Imekuwa ni malipo yake, na itabakia gharama yake. Toleo hili lingali wazi kwako. Lakini hakutakuwepo udanganyifu wakati huu.

"Wengi mnaosoma ujumbe huu mtafahamu na kukiri alama ya mnyama, katika mkono wa kulia au kwenye paji la uso. Wengi wenu mnafahamu kwamba Bibilia inasema kwamba, yeyote atakaye pata alama atapokea adhabu ya Mwenyezi Mungu, na utachomwa na kusaga meno mbele ya Yesu na malaika watakatifu. Utatupwa kwenye ziwa la moto, na kuungua milele. Hivi ni vitisho vya kweli. Huwezi kufikiri kwamba huo ni 'upendo', lakini kumbuka. hautaweka sheria; Mungu ataweka. Kabla ya kukubali hayo hautapata kufahamu jinsi anavyotupenda.

"Sasa haya ndio maelezo ya habari njema ya Yesu Kristo kwenu nyinyi mliopokea alama ya mnyama. Ina maana kwamba ukubali kukatwa mkono wa kulia au kukatwa kichwa kwa ajili ya neno la Mwenyezi Mungu!

"Hiyo ndio kweli halisi. Yesu alisema kwamba, iwapo mkono wako wa kulia utakukera, basi ukate. itakuwa bora kuingia ufalme wa mbinguni bila mkono, kuliko kuelekea jehanamu kwa maelekezi ya mkono wako wa kulia. Kwa miaka mingi watu wamechukulia usemi huo kama kwamba hakutaka tuuchukulie kama jazanda. Lakini sasa ni jukumu la kila muumini au mfuasi kila mahali kudhihirisha imani yake kwa matendo.

"Labda wengi wenu hamjapata kusikia ilani kuhusu Alama ya Mnyama. Lakini mmesikia sauti ya Mungu kupitia kwa nafsi zenu, na kisha kukaidi. Kwa sababu moja au nyingine muliamua kufuata njia zenu, kusonga mbali kutoka kwa maadili ya ujana na maadili ya dini zenu. Na ni kutokana na kukosa imani na muelekeo wa kuchanganyikiwa ndiposa mmejikuta mahali mlipo.

"Kumbuka Mungu hajauliza chochote kile ambacho hajawai kuuliza mtu yeyote. Tofauti ni kwamba sisi tunaoandika tulisikiza , ule moyo wa kiroho cha ndani kwa makini kabla ya kukubali Alama ya Mnyama, na kukataa kukubali. Tulimkubali Mwenyezi Mungu na mafundisho ya Mwanawe."

Kwa hakika tulikatiziwa na twazidi kukatiziwa kwa uamuzi wa kuweka Mwenyezi Mungu mbele. Lakini kwa jumla tumeibuka na kuwa mbele. Wewe unaye soma ulichelewa kutoa uamuzi, ukidhani kwamba ni vigumu au inakatiza mipango yako kwa kumuweka Mungu mbele, na kisha kujiletea haya yote."

"Tunaweza kuhitimisha kwa kukueleza kwamba uamuzi huu unafaa na ni kweli. Mbingu ni hakika. Yesu ni mwana wa mungu. Yale anayotoa ni hakika. Uzima wa milele. Upendo wa milele. Amani ya milele.

"Lakini mapatano halisi ya hayo yote yatahitaji kubadili hali yako ya maisha. Uamuzi ni wako.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

Maelezo mengi na ufafanuzi kuhusu Alama ya Mnyama yazidi kutolewa na jinsi Wakristo wapaswa kuchukulia, na kisha kuepuka adhabu kwa kutenda hivyo. Yote huzungukia "Hisani ya Mungu", na jinsi Mungu wa Upendo hawezi kumtia adabu yeyote atakaye sema Bwana Bwana kwa Yesu. hata iwapo hawajapata kumtii au kujaribu kumfuata. Lakini fundisho kama hilo ni kinyume cha hekima ya Mungu, na kufanya stihizai kwa yote yaliyo kwenye Bibilia (na hasa Yesu) kuhusu imani.

Inaweza kuchukuliwa kwamba kukubali Alama ya Mnyama (kama inavyoelezwa kwenye kitabu cha ufungua) yatosha kumpeleka mtu kwenye ziwa la moto wa milele, bila matumaini yoyote. Lakini yale Yesu alieleza pale kwenye mlima kuhusu kuukata mkono iwapo umekuudhi (Matayo 5:30) yatoa ufafanuzi kuhusu gharama ya "nafasi" ya pili. iwapo kutakuwepo kitu kama nafasi ya pili.

Jambo la muhimu ni kwamba, iwapo unachukua muda mwingi kuweza kumuamini Mungu, ndiposa utapata shida nyingi. Nani anayeelewa kwamba hakuna fursa ya kuungama dhambi kule jehanamu? Lakini nani atataka kuingia huko ili ajionee?

Bibilia inasema,"Sasa huu ndio wakati, Wakati wa wokovu ni leo. Leo hii ukisikia sauti yake usifanye roho ngumu kama wale Waisraeli walipokuwa jangwani, na kumfanya Mungu akasirike." (II Wakorinzo 6:2 Wahebrania 3:7-8, na Wahebrania 3:15)

 

 

19. Msukumo wa Mahangaiko

 

Wanachama kumi na watano wa tabaka lile walijikusanya kwenye ukumbi wa nyumba ya mafunzo kule Sao Paulo. Fanicha ziliondolewa ili kuwepo nafasi kwao, na pia sehemu ya juu ya Meza isiyo na matende-guu katikati ya ukumbi ule. Ilikuwa na kamba za ngozi zilizofungwa kila upande.

Luis alikuwa amewasili kutoka Rio asubuhi ile. Kule Rio alikuwa amemuona muuguzi akitenda hayo mara mbili, kabla ya kutwikwa jukumu la kutekeleza mwenyewe. Sasa katika muda wa wiki mbili alipaswa kuwafundisha wenzake, jinsi ya kufanya. Kulikuwa na orodha ndefu ya watu waliokuwa wakisubiri kule Sao Paulo, huku watu wengi wakijaribu mtandao na kuomba msaada wa kuepuka Alama.

"Uko na kauli mbili tu," Luis alimueleza mgonjwa wa kwanza kumtembelea asubuhi ile, huku wengine kumi wakimskiza. Wote walikuwa wameletwa pale bila hiari yao na kwa kidota. "Tunaweza kutoa ngozi ya mgongo, au kuuchukua mkono wote. Tuna uhakika wa kupachika chembechembe kwa asilimia tisini kwa kutoa ngozi, na yaweza kufanya bora hata chini ya misuli"

"Tafadhali hapana, amogo! Toa yote!" mgonjwa yule aliomba, mkulima maskini wa umri wa miaka 40 hivi, kwa jina la Joaquin.

"Mashetani, wako kila mahali," aliendelea. "Siwezi kulala. Siwezi kufikiri. Tafadhali iondoe yote. Mungu, nisaidie!" na macho yake kuangalia mbinguni.

Sasa Joaquin alikuwa akivuliwa chini ya sakafu, kama mfungwa kwenye msalaba.

Mlango wa mbele ulifunguliwa kidogo na Fransisco kuchungulia. "Nimewapata," alisema huku akiingia kwenye chumba na kuufunga mlango nyuma yake. Alichomoa visu vya aina ya Stanley kutoka kwa mfuko. "Niliviiba. Mungu anisamehe." kichwa chake kikaegemea kama kwamba kuomba msamaha.

"Natumai kwamba katika hali kama hii Mungu ataelewa," Luis alisema kwa kumshawishi.

Fran aliinua kichwa kwa furaha. "ninafurahi kwamba umetazama mambo haya hivyo, luis," alisema, "Kwani sikuona hatia kwa kuchukua. Nilijihisi bora kabisa!"

Wale wengine walicheka kidogo. Mahali hapo palikuwa pa utesi kiasi cha kutocheka.

Joaquin aliyekuwa amepewa vidonge vya kuzuia uchungu dakika kumi zilizopita, alikuwa amenyatwa pale chini. Wanaume wawili waliinama, na kupanua miguu yake. Wanawake wawili walisongea karibu na kichwa. Hao pia walipiga magoti huku wameshikilia Bibilia. Wangepokezana kwa zamu huku wakiimba nyimbo za kiispania, huku Luis akitekeleza tambiko.

Walipokuwa tayari kuanza, kipande kizito cha ngozi kiliwekwa kwenye mdomo wa Joaquin, ili aweze kukiuma. Ilikuwa ni muhimu wasiweze kutambuliwa na majirani, kutokana nahayo, Jouquin hakuwa na budi ya kunyamaza kimya licha ya uchungu.

Kitita cha viraka kiliwekwa kwenye mkono wake wa kushoto. Aliambiwa kushikilia mkono wake wa kulia bila kusongesha hadi mwisho wa tambiko hilo.

"Bwana ni mchungaji Wangu. Sitapungukiwa," Felicadad alianza kwa kiispania. Aliendelea kusoma huku Joaquin akiwaza juu ya maelezo hayo.

Kisu cha kwanza chenye makali kilikuwa kimesafishwa kwa kileo. Luis alimwagilia tone fulani la dawa, kunyakua mkono wa Joaquin, na kuukata kwa kutumia kile kisu cha makali. Mwili wa Joaquin ulitingisika huku akiuma ile ngozi.

"Ijapokuwa nitapita kwenye bonde la kivuli cha kifo, sitaogopa ubaya; kwani Yu nami," Felicidad aliendelea. Fimbo yako, hunikinga na kuniliwaza."

"Twapasa kutoa nafasi kwa ngozi kutoka kwa mkono." Luis alieleza, huku akichukua uzi na shindano kushona mshipa wa damu. "Tukimaliza tutahitaji ngozi kufunika kiduta, na kuunganisha kwa sehemu ya juu."

Kwasababu ya kukosa vifaa vya upasuaji. Alitumia tu kipuli aina ya pliers kushikilia ngozi ile. Mishipa ya ndani ilipaswa kuchomwa kwa waya iliyokuwa moto .uchungu zaidi.

Tone la dawa ile lilizuia kuvuja kwa damu, haikuwa rahisi sasa kutambua iwapo uzi au waya ile ilifanya kazi. Luis alikuwa na picha mbele yake iliyomuonyesha mahali pa kupata mshipa.

"Kufunga kwa bandeji kulipaswa kutunza sehemu za mishipa ya ndani," alisema.

Macho ya joaquin yalijawa na machozi, na sehemu za mkono ulioshikilia ngozi, nusra zionyeshe mfupa kwa kushika kupita kiasi. Sehemu zote za mwili zilisonga kiasi cha kuepusha kutingika kwa mwili.

"Majonzi yaweza kuwepo usiku, lakini furaha huja asubuhi." Maria alisoma, huku Felicidad akitafuta wimbo muafaka.

Luis alisukuma wembe ndani na kukata, mwili wa Joaquin ulijiinua kutoka kwa meza. Wale wanaume wawili walimshikilia kwa nguvu. Aliguna kwa uchungu huku kijasho kikimtiririka.

"Hapo! Tumekata mishipa ya kila aina," Yule mkufunzi alikuwa akiwaeleza wanafunzi wake.

Mahali pa kutatanisha pamekamilika sasa, Joaquin," alimuambia mgonjwa.

Luis hakusema mengi, huku akijifanya kuwa na kazi nyingi. Wale wanafunzi wake waliokuwa na mshangao walisonga karibu kujionea.

Ilikuwa ni dhamu ya Felicidad kusoma baada ya kukamilisha tambiko. "Heri yule aliyesamehewa dhambi zake, dhambi zake kufichwa. Heri mtu aliyepokea upako wa Bwana, na asiye na kikwazo rohoni mwake," alisoma.

Joaquin aliinua shingo lake na kumtazama Felicidad. Machozi yalimtoka, kulingana na maandiko yaliyo somwa, kama kwamba ni sawa na uchungu aliokuwa akihisi.

Kilichobaki ni minofu iliyoshikilia mifupa na mkono. Luis alisukuma ndani na Kile Kisu aina ya Stanley, kukata misuli iliyokuwa kubwa, na kuwacha mifupa.

Macho ya Joaquin yalijifunga na akazirai. Alikuwa amezimia.

Wakati tambiko lilikuwa limekamilishwa, na mwili wa Joaquin kufungwa, Luis aliwaarifu wanafunzi wake kwamba atafanya jambo moja, kabla yao kutekeleza kivyao. Walitarajiwa kuhudumia angalau mgonjwa mmoja kabla ya siku kuisha. Nakuwahudumia wengi hapo baadaye.

Aliwapatia maelezo kuhusu vile watakavyowatunza wagonjwa baada ya kupitia upasuaji huo.

Tukio hilo lile liliwaadhiri sana wale wanagenzi; hata kabla ya jereha kuanza kupona, wakati Joaquin alirudia hali yake, alitabasamu katika uchungu, alibadilika sana na kuongea juu ya amani aliyokuwa amepata.

Luis alimuonya kwamba angaliweza kupata matatizo. Maambukizi ya kipindupindu yalikuwa kawaida, na baadhi ya watu waliokatwa mikono walikufa kutokana na maradhi yaliyosababishwa sehemu ya jeraha kuoza.

"Hiyo sio shida," Joaquin alisema. Nina furaha kufa hivi sasa kwa kumpigania Mwenyezi Mungu vita. Moyo wangu ni huru. Ahsante Mungu! Wajua ndugu, nina furaha kufa kwa niaba ya Yesu sasa hivi. haki furaha."

Jaquin hakuwachwa nyuma miongoni mwa wale waliokuja kuondolewa Alama. Kote Ulimwenguni tofauti kwenye imani ilikuwa ikitukia. Watu ambao walikuwa hawajawai kuchukulia kazi ya Mungu kama ya dharura, walikuwa wakipokea amani, upendo, na motisha wakati huu wa kutazama amri ya Yesu. Ilikuwa mojawapo ya njia ya tambiko kwa wale walio teuliwa.ubatizo katika hali ngumu aliyopitia Yesu. Ilwakilisha tohara ya moyo, kwa kutoka katika uongo na kuingia kwenye Imani ya kweli ya Yesu na yote aliyofundishwa.

Lakini hata hivyo, kukatwa kwa mkono ili kuondoa Alama, ilikuwa ni mwanzo tu wa huzuni na mateso kwa watu hawa. Kukosa kuwa na mkono ilikuwa ni dhibitisho kwa ulimwengu mzima kwamba wamekata Alama. Mahali popote walikoenda, watu walisimama na kuwaangalia. sio tu kwamba walikuwa tofauti, lakini kwa sababu idadi ya watu wasio na mkono wa kulia ilikuwa inazidi kila siku. Lazima kuna jambo lililokuwa likiendelea na watu fulani walisimama kuwauliza.

"Ulipoteza mkono kupitia njia gani? nimeona watu wengi kama wewe. Hii inaashiria nini?"

Na kutokana na hilo, ujumbe ulikuwa ukienea kupitia njia ya mdomo, kwa yeyote ambaye hakupata kuutazama mtandao. Wale waliopata ujumbe huu waliupitisha kwa uaminifu kwa wengine kama walivyopata, kwa sababu hakuna yeyote aliyekosa kupata uguso kutokana na yale waliyosikia.

Palikuwepo haja ya kuwaficha wanamhanga hao kabla ya kupona majeraha kutokana na kukatwa mkono. Wakati huo walipewa mafundisho ya kutosha, na baadaye kuwekwa pamoja na wanamhanga wengine waliokuwa wamekatwa mikono. Wangalichukuliwa kwa kufunikwa macho, kwenye giza, hadi pale watakapoishi utumwani, wakiishi kama watu wasiotakiwa kwenye jamii. Walijua kwamba haitakuwa muda mrefu kabla hali yao ya ulemavu kutumiwa kuwatia mbaroni. Lakini walikuwa wamefanywa uamuzi, na kama Joaquin, walikuwa tayari kupoteza maisha, kutokana na imani yao mpya.

Kwa sababu Alama haikuwa ikionekana, wale 144,000 kati ya Makabila Kumi na Mbili hawakuwa na tofauti yeyote na watu wa kawaida mitaaani. Kutokana na hili waliweza kuishi ile miaka tatu na nusu bila kutambuliwa.

Lakini wanamhanga waliokatwa mikono walikuwa ni alama ya wazi kwa uma. Walijulikana na wale waumini wengine kama Msukumo wa Mahangaiko. kile ambacho hakingaliwasilishwa kupitia kwenye mtandao uliotayarishwa na Rayford na Chaim katika ujumbe wao (licha ya ukweli ulio kuwemo), ushuhuda wa kudumu kutoka kwa Msukumo wa Mahangaiko. Watu wale walioshiriki tambiko na kujivunia utajiri na mafanikio waliyopata. kama kwamba wokovu wao haukugharimu chochote. ulikuwa ni shuhuda ya kweli kulingana na mapenzi ya Mungu.

Msukumo wa Mahangaiko haukuwa na matumaini ya maficho katika ukiwa kama wale 144,000. Waliamini hivyo, kama walemavu wa kiroho, siku zao zilikuwa zimehesabiwa. Haitakuwa kitambo sana kabla ya Dangchao na jeshi lake kuwavamia kisha kuwahukumu, iwapo kuelewa kwa Rayford na Chaim kuhusu utabiri kulikuwa kwa kweli.

Lakini ufahamu wa haya uliwafanya kutia bidii katika kuhubiri kuhusu habari njema ya Yesu. Walitaka wengine kuepuka laana iliyokuwa ikining'inia duniani, na ushuhuda wao haukuweza kulinganishwa na Makabila Kumi na Mbili. Maelfu zaidi walikuja kila kila siku, kujiunga nao. Dunia ilikuwa ikipokea kutoka kwa hawa, muamuko kuhusu kupokea imani halisi katika kizazi kisichomti mungu.

* * *

 

Kwa wakati huo huo kulikuwa na mabadiliko yaliyokuwa yakiendelea kule Yerusalemi. Baba Mtakatifu Pius aliyekuwa ameapa kufanya kitu cha kishujaa "siku moja" alikuwa akisonga mbali na kutekeleza. Yeyote yule aliyedhani kwamba haikuwa na "Uwezekano" kuchukua hatua dhidi ya watu waliomuasi Yesu (Kwa sababu ingalitishia cheo chake, heshima yake,,shirika lake na amani yake) alikuwa ameaibika na kukasirishwa na shuhuda ya wanachama wa mkono mmoja katika Msukumo wa Mahangaiko, aliodhani kwamba hawakuyataka Makabila Kumi na Mbili.

Pius alikuwa tayari kusahau ukweli wa dhambi za Dangchao kwa kuzingatia ukinzani wa kundi hili, na shida na uchungu aliodhani wanapitishia ulimwengu. Mkataba wake na Dangchao kuyawinda Makabila Kumi na Mbili lilikuwa jambo lililowakera, hadi kumpelekea kuamini kwamba wito wake ulikuwa ni kikinga dunia dhidi ya mkiuko wa dini.

Kuishi na kufanya Kazi kwa pamoja na Dangchao kulikuwa na madhara kwa Pius kama vile watu wanaoishi karibu na eneo la kusafisha maji-taka huadhiriwa. Kinachowakera wageni wanapotembelea eneo kama hilo huonekana na wanaoishi pale kila baada ya siku. Dangchao alikuwa na upungufu wake, ilikuwa dhahiri; lakini alikuwa akijaribu kuleta amani ulimwenguni wakati mgumu. Hali ngumu katika afisi yake labda ndio iliyomfanya kutenda vile. Jambo muhimu ni kwamba, kama alivyojiambia Pius ni kuimarisha muungano wa Kanisa, na umoja wa serikali. Shida chache njiani ilikuwa ni jambo la kawaida. Ilikuwa ni mojawapo ya gharama atakayolipia katika wakati huo.

Pius aliwaza kuhusu kufanya marekebisho kwenye sanamu mbele ya basilika. Kipaaza sauti kiliwekwa, pamoja na bunduki chini ya sanamu hiyo. Umati wa watu ulijitokeza pale kila siku, na sanamu hiyo kubwa ingali "zungumza" kwa umati ule katika zamu, kwa kusema, "Tuiname na kumuabudu mfalme wenu pamoja na Mungu!" Sekunde tano baada ya usemi huo, zile bunduki zilizokuwa mita moja kutoka chini, zingalifyatuka.

Watu wengi walikufa au kujeruhiwa wakati wa kwanza bunduki zilifyatuka. Hatukuwepo na tahadhari kuhusu litakalo tokea, Dangchao alikuwa amefanya mzaha kuhusu vile watu wataanguka na kulala kifudifudi, hadi pale watakapo hakikisha kwamba bunduki zimewachwa kufyatuka, wakati mwingine sanamu ile "itaongea"

"Lazima kutakuwepo na uharibifu wa vitu fulani katika shughuli za kivita," alisema, wakati watu walilalamika kuhusu kujeruhiwa kwa watazamaji wa kawaida au hata kuuawa. wale waliosujudu kwa kujua walichotarajiwa kufanya. "Sio ya ajabu vile ujumbe unavyoenea kwa wale wengine wasio na 'hatia'," alicheka. "Sasa tumefanyia majaribio na kuonyesha mfano, nani atajificha nyuma ya ujinga?"

Waliomuasi bwana hawakuwa na la kujali katika kuua ili kutoa maelezo. Lakini alilotaka ni kuungamiza Makabila Kumi na Mbili kote ulimwenguni, waliokuwa wakipata umaarufu kila kukicha. Ujumbe kuhusu kukatwa kwa mikono ulikuwa umemfikia, na kuamurisha kwamba vifaa vikubwa vyenye makali vijengwe kwenye miji yote kote duniani. Iwapo umati mzima ungalichinjwa, basi watu wengi wangaliogopa, alidhani hivyo. Ingaliwatisha wafuasi wenzake ambao walikuwa na nia ya kujiunga na imani hiyo.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Imani yenye nguvu huwaadhiri wale wote wanaokumbana nayo. Baadhi watajaribu kuiga waliyoona; lakini baadhi hukasirika tu kwa kuona imani kama hiyo. Hawawezi kudumu kwa ukweli kuhusu umaskini katika roho, hivyo basi kuwashambulia walio wahaibisha. Hao huwaita warithi, wendazimu, na wanatabaka lisiloeleweka. Na hujaribu kuwanyamazisha, au kuwaangamiza.

Kitabu cha Ufunuo wa Yohana kinaongea kuhusu umati mkubwa usioweza kuhesabiwa (kwa pamoja na wateule 144,000 walioteuliwa na Mungu kabla ya Mahangaiko au Huzuni Mkuu kutokea). Inaeleza kwamba watu hawa watavaa kanzu nyeupe wakisimama mbele ya Mungu, kanzu zilizosafishwa kwa "damu ya Mwanakondoo" (Ufunuo wa Yohana 7;9, 14-17)

"Damu ya Mwanakondoo" inamaanisha damu ya Yesu iliyo mwagika msalabani kwa ajili yetu. Lakini pia Yesu alitoa wito kwetu sisi kuubeba msalaba wetu na kufuata nyayo zake. Ufunuo wa Yohana unatueleza kwamba wakati wa Huzuni mkuu na mahangaiko, wafuasi wa Bwana watawaungusha waasi wake kwa "Damu ya Mwanakondoo, na kwa wito yakwamba hawakupenda maisha yao, hata usoni mwa mauti." (Ufunuo wa Yohana 12:11)

Haya yote ni kuonyesha kwamba umati mkubwa "unaojitokeza wakati wa Mahangaiko na Huzuni mkuu" watakuwa wahanga, wakimfuata Mwanakondoo hadi kifo chao. Ufunuo wa Yohana unatuarifu kwamba "Watakatwa vichwa" (Ufunuo wa Yohana 20:4)

 

 

20. Maafa

 

Reinhard alitembea kwa kukwawa kwenye barafu. Moscow nzima ilikuwa katika hali ya kusikitisha. Hakuna jumba lolote lililobaki

Kwanza tulikuwepo na mawe kutoka kwa nyota yaliyokuwa yametapaka kote Uropa, Afrika ya kaskazini, mashariki ya kati, na sehemu za Asia. Alama ilibakia mahali yalipoanguka, na kuanzisha moto kwenye misitu katika sehemu nyingi za dunia. Wingu la ukiwa lilikuwa limeutanda ulimwengu, huku likifunika mwangaza wa jua. Hewa ya moto kutoka kwa miali ya moto ilijaa kote na kuyeyusha unyevu wote uliojikusanya na kugeuka mawimbi yaliyonyesa mvua ya barafu, mawe hayo ya barafu yalikuwa hadi uzani wa kilo moja kwa kila kigae. Maelfu ya watu yalikufa kwa kunyeshewa na mawe hayo ya barafu. Miji yote iliwachwa bila paa. Mamilioni ya magari yaliharibiwa kiasi chakutoweza kurekebishwa. Mizoga ya wanyama ilitapakaa kila mahali.

Basi ikafuata na ile nyota kubwa asteroid. Ikaunguka upande wa katikati mwa Atlantiki, na kufanya maji kujaa na kuruka hadi mamia ya mita kutoka baharini, na kuosha miji yote iliyokuwa kwenye ukingo au pwani. Mamilioni yalipotezwa kwenye pwani ya Mashariki mwa Amerika ya Kusini na Kati, na pwani ya Magharibi mwa Afrika na Uropa.

Idadi ya nyota zilizoanguka katika awamu ya pili zilisababisha maafa mengi kuliko ilivyokuwa awamu ya kwanza, hata ingawa zilikuwa tu mojawapo ya nyota zilizokuwa zikiruka mfano wa garika. Huko Urusi waliita maafa hayo "Chernobyl" kutokana na miali yake. Miali hiyo iliadhiri theluthi moja ya mikondo yote ya maji kote ulimwenguni, aafa haya yalizidi na kuwapelekea watu kunywa yale maji yaliyo na sumu, huku wakifahamu adhari ya kupata saratani, matatizo ya kizazi, na vifo vya mapema. Ilikuwa ni kuyanywa maji hayo au kufa kwa kiu.

Rayford na Chaim walikuwa awali wamesha tabiri, na Dangchao pamoja na baba Mtakatifu Pius walifanya yote waliyoweza kupambana walipofahamu kwamba nyota zina kuja. Wataalamu walisema kwamba msukumo wa nyota ile kubwa hautagonga dunia. Walisema uwezekano wa kugongana na dunia ulikuwa mara moja kwa milioni, hata baada ya zile nyota ndogo kuanza kuanguka, walianza kusema kulikuwa na nafasi ya moja kwa kumi ya uwezekano wa ile nyota kubwa kulenga dunia. Kwa wakati garika hiyo ya ajabu ilikuwa inasababisha maafa, watu walichelewa kunusuru miji. Na sasa dunia ya Dangchao ilikuwa imekumbwa na maafa kupita kiasi.

Ilikuwa ni sababu ya kuchikia Msukumo wa mahangaiko. (aliodhania Dangchao kuwa baadhi ya wanachama wa tabaka 144,000) kwamba hii ilitukia mwanzoni.

Ilianzia na tangazo kutoka kwa Rayford na Chaim kwamba ukame utatokea Israeli, hadi pale Dangchao atakoma kuwadhulumu wafuasi wa Mungu. Mvua ilipotea kwa miaka mitatu. lakini haikukomesha dhuluma dhidi ya wafuasi wa Mungu.

Basi wale Mitume wawili wakatangaza kwamba maji katika maeneo yaliyowaua wateule wa Bwana yatalaaniwa. Maangamizi ya wateule yalianzia kule Amman, Yorodani, huku zaidi ya wateule mia moja wakiuawa siku ya kwanza. Hata hivyo, kima wawili walipatikana wamekufa ndani ya bohari la maji ya kusambazwa mjini, wakijaribu kukimbia. Lakini uchunguzi ulibaini kwamba walikufa kutokana na maradhi ya ebola, na kisha janga la ugonjwa huo likazuka kule Yorodani, na watu hawakuruhusiwa kuingia au kutoka kule. La kustaajabisha ni kwamba mauaji yalikoma, hatukupata kushuhudia ukatili huo kwa miaka mitatu ya mwisho Lakini hata hivyo hapakuwa mahali salama pa kujikinga kwani virusi vile vilisababisha vifo sawa na eneo lililo shuhudia mauaji.

Lakini Dangchao alikuwa na mvukuto kutokana na kukasiriishwa na wale wafuasi wa Mungu hata baada ya tukio la Amman. Mauaji ya halaiki yalianza kote duniani baada ya siku chache. Katika kipindi cha mwezi mmoja, zaidi ya wafuasi milioni moja waliokuwa na mkono mmoja walikuwa wamekatwa vichwa.

Na hapo ndipo wale Mitume wawili walionya kwamba nyota kuu itaangukia dunia. Dangchao na Pius walikataa kutazama mtandao wa makabila Kumi na mbili, kama kwamba waliogopa itaadhiri fikira zao, walipata tu ujumbe kupitia kwa washahuri wao. Waliposikia kuhusu nyota ile, walitawanya wataalam wa kusoma nyota kote duniani. Wataalam hao waliambiwa kuweka habari hizo kwa siri na wasizitoe kwa vyombo vya habari au raia. Wanahabari walipata ripoti ya nyota kubwa kuanguka siku tano kabla ya tukio. Hata hivyo, haikuwa mapema kwa uma kufanya lolote kuhusu hali hiyo.

Hapa tulikuwa na Reinhard akipata shida kutembea katika barafu kule Moscow, akijaribu kutafuta mahali salama, nyumba nyingi zilikuwa zimeharibiwa na garika kuu. Lilikuwa ni jukumu lake kuona vile kazi ya marekebisho itatekelezwa. Sheila Armitage alikuwa mzee sana kutekeleza jukumu kama hilo, hivyo basi majukumu kama hayo yaliwachiwa Reinhard.

Mwanzoni alikuwa ni Rayford aliyefundisha, na kisha baadaye kulichukua jukumu la kuwaongoza Jesans. Reinhard alifanya kila juhudi kukubali, lakini halikuwa jambo bora kuenda mitaani kuuza majarida huku Rayford akifundisha kama kwamba yote aliyosema yalikuwa yakitoka kwenye akili yake. Hatimaye akawa ni Sheila. Watu walihiari tu kumuendea Sheila kwa mawaidha kuliko yeye, kwa sababu alikuwa na umri mara mbili kumliko. Na karibuni akawa Jerry, mmoja wa wahitimu wa kwanza wa kabila la Asher, aliyekuwa akipewa heshima sana kuliko Reinhard.

Kwa hakika alipowasili Jerry, mwanaume wa mapambo yaliyopendeza, mwenye umri wa miaka sitini, nywele nyeupe na kidevu, aliingia tu na watu wakaanza kufanya kazi kwa bidii ili kurekebisha jengo lile. Huku majirani waking'oa paa ili kuuzeka kwa chuma au vifaa vilivyonunuliwa katika maduka ya serikali, wafanyikazi wa Jerry waliingia mitaani kuokota kutoka kwa vifusi vilivyokuwa vya majengo, ili kuvitumia kurekebisha nyumba yao. Vifaa vilikuwa vikiingia, na utakuwa ni muda mchache kabla ya kukomesha barafu kuingia kwenye makaaazi yao.

"Karibu! Karibu!" Jerry alisema kwa ukarimu, wakati alipomfungulia Reinhard alipobisha mlango. "Ivan mletee ndugu yetu kikombe cha kahawa," aliyekuwa wakati mmoja Muamerika alisema kwa lugha fasaha ya Kirusi.

"Sitaki kahawa," Rainhard alijibu kwa haraka.

"Nimekuja hapa kufanya kazi."

"Bila shaka," Jerry alisema kwa ukarimu. Kisha kutazama uso wa Reinhard: "lolote limekukera?"

"La, hakuna lolote linalo nisumbua" Rainherd alimjibu. "kuna jambo linalokusumbua wewe?"

Kwa hakika ndio, natumai lipo," Jerry alisema. "Je twaweza kuingia katika chumba cha nyuma tukajadili?"

"kwani nini mbaya tukijadiliana hapa?" Reinhard aliuliza kwa lahaja huku akizama kwenye kiti kile, na kuweka mikono yake kwenye sehemu za kuegemeza mikono.

"Sitaki nikuhaibishe," Jerry alijibu, kwa upole. "Nafikiri haujafurahia jambo fulani, nilitaka kujadili nawe faragani. mimi nawe tu."

Reinhard aliamuka na kuelekea katika chumba kilichokuwa nyuma. Sikutaka nikuhaibishe alifikiri. Kwa kuwaza juu ya maongezi ya upole ya Jerry Anthony. Alifikiri tu hana dosari na wenzake wangalifuata amri yake.

"Je inakukera kwamba mimi ni kiongozi hapa?" Jerry aliuliza. Alikuwa ameona hayo yapasa wiki kadha zilizopita, na ulikuwa wakati wa kutatua.

"Labda," Reinhard alisema, kwa kutingisa mabega, macho na mdomo, kuonyesha hali isiyo ya kujali.

"Tafadhali, naweza kujadili kitu fulani nawe? Jerry aliuliza.

"Ni juu yako," Reinhard alijibu, kwa kujifanya kama kwamba hana haja, huku akiinama kwenye meza katika chumba hicho, na kuangalia kwenye sakafu.

"Kabla ya vita.kule Amerika.Nilikuwa na kazi niliyo dhani ni bora. Nilijiona kama kiongozi bora. lakini ilichukua vile vita na mauti ya halaiki kuona kwamba fikira zangu zilikuwa potovu. Cheo fulani hakimfanyi mtu kuwa kiongozi.

"Nilifika hapa Moscow kama mtu aliyepotea. Lakini nilipokutana nawe, Reinhard," (Jerry alikimia kwa sababu fulani). "Nilipo kutana nawe, nilijua kwamba nimekutana na kiongozi wa kweli. Haukutambuliwa kulingana na malimwengu, bila mshahara, bila cheo, lakini ulijua ulipokuwa unaelekea. Ulijua jinsi ya kutambua vitu vidogo na mambo makubwa, ulinipa changamoto kujaribu.kuwa kiongozi wa kweli.

Reinhard alijipata katika mashaka. Alitaraji shutuma kutoka kwa huyo mtu aliyemzidi umri. lakini badala yake alitiwa maneno ya kubembelezwa. Ilifanya zaidi ya shutuma. Ilikuwa ni kitambo sana tangu Reinhard kupata sifa kama hizo, na alifahamu kwamba yale Jerry alikuwa akisema yalikuwa ni ya kweli kuhusu kiongozi bora. Kuwa kiongozi bora sio kupokea sifa kila mara. Ilimaanisha ule uwezo wa kuweza kuona mbele kuliko wenzio.

Yale aliyosema Jerry yalitosha kumletea matumaini yule ambaye alikuwa amepoteza. Reinhard alikuwa ameona baadhi ya viongozi katika Makabila Kumi na Mbili wakipoteza matumaini, na maono ya milele, na mbingu na hata kurudi kwa Yesu, na wote walikuwa wamerudi nyuma. Baadhi yao walikuwa viongozi bora kabla ya kurudi nyuma. Hakutaka kujiona kama mmoja wao kwa kurudi nyuma. Alisimama na kumkumbatia yule mzee.

"Danke", alisema kwani Jerry alifahamu Kijerumani.

"Danke, Jerry! tafadhali nisamehe kwa tabia yangu mbovu."

Reinhard hakuwa na nafasi tangu kuingia Moscow, zaidi ya miaka minne iliyopita, lakini haikuwa kisingizio cha kushahuriana na mtu huyu mwenye busara, na jukumu kwa muungano kwa zaidi ya miaka mitatu, na aliyeongea ukweli uliomtoa Reinhard katika upembe wa kupotea.

"Nieleze zaidi kukuhusu," Reinhard alisema, katika juhudi za kuficha dhambi zake. "ulikuja aje huku Moscow?"

"Hatukuwa na chaguo," Jerry alieleza. Nilijificha kule Amerika kwa wiki kadha; lakini wakati elkopta ilikuja kuwanusuru wahanga, ilikuwa ni ile ya Urusi. Tuliletwa hapa na tumeishi hapa tangu hapo."

"Na je familia yako?" Reinhard aliuliza.

"Nilikuwa na watoto wawili, msichana na mvulana, wote wakiishi New York. Walikuwa karibu na eneo la mlipuko. Wangalikufa papo hapo."

"Na bibi yako?"

"Bibi yangu?" Jerry aliuliza. " Mi.Yeye." Alisita. "Sijawai ongea juu yake."

"Labda huu ndio wakati bora kuanza," Reinhard alisema kwa ukarimu.

Jerry alisita kwa mara nyingine. Ilikuwa dhairi kwamba alitaka kuongea, lakini kulikuwa na kitu kilichokuwa kikimzuia. "Nitahitaji kuongea juu ya hilo," alisema. "Na uliweke hilo kati yangu nawe?" aliuliza. "Ni muhimu sana."

"Bila shaka," Reinhard alikubali.

"Mke wangu aliuawa, sio kutokana na mlipuko. Aliuawa na muaji wa kujitolea, mbele ya macho yangu." Sauti ya Jerry ilianza kukatika, lakini alitaka kumaliza masimulizi yake. Bila shaka lilikuwa ni jambo ambalo alijiwekea kwa muda. "Alinuia kuniua miye pia!" alilia. "Hank.Hank Greenhorn. mmoja kati ya walinzi wangu, alijirusha mbele yangu. Hakuwa na nafasi."

Jerry aliketi chini ya sakafu na kuweka uso kwenye mikono yake, akidondokwa na machozi huku akisimulia.

Reinhard alisikiza kwa makini. Walinzi? Muaji wa kisiri? alikuwa akiongea juu ya nini?

"Mlipuko ulinifanya kiziwi kwa muda. Nilihangaika sana kiasi cha kushindwa kuongea. Hakuna yeyote aliyetoka mle ndani akiwa hai. Wakati Warusi walipowasili, Nilijua singalitumia jina langu la kweli. Nilitumia jina langu la kati. Gerald Anthony. Ndevu zangu zilikuwa zimeanza kumea na nikawacha. kwa pamoja na nywele zangu ndefu.

Rainhard alijiunga naye kwenye sakafu na kumkumbatia. Kwa yale aliyokuwa akiongea, alionekana kama aliye sumbuliwa.

"Mungu angalinisamehe kwa njia ipi?" alilia, huku akipanguza mapua kwa kitambaa.

"Ningalikuwaje mtu asiye na huruma? Niliwacha tamaa zangu za kisiasa kuwa muhimu kuliko maisha ya watu wale. Nilichelewa kugundua kosa langu. Singali nusuru Amerika; lakini nashukuru Mungu, sikubwenyeza chochote kuwaangamiza."

Reinhard alikuwa akijaribu kumuelewa Jerry. Ni vipi Jerry Anthony au Jerry fulani alisababisha kuanguka kwa Amerika? Alisukuma nywele za huyu mzee kutoka usoni mwake, kisha kumtazama. Nywele zake zote zilikuwa za kijivu, labda kutokana na yale aliyopitia, lakini kutoka kwa kidevu Reinhard alidhani angalimtambua.

"Fitzhugh?" aliuliza.

Jerry alitikisa kichwa.

Reinhard hakuamini. Alikuwa ameketi kwenye sakafu akimbusu aliyekuwa Raisi wa Amerika. Mtu huyu alikuwa amezeeka, mwenye nywele ndefu na kidevu, lakini alikuwa Rais.

Muaji wa kujitolea (labda mmoja kati ya askari wake) lazima aliingia kwenye Ikulu ya White House, pamoja naye na mkewe.

Yule Rais wa Amerika alimueleza Reinhard kwamba alikuwa ni Reinhard aliyemfundisha maana ya kuwa kiongozi. Na alikuwa amesema baada ya kufanya kazi chini ya Reinhard kwa zaidi ya miaka tatu. Sifa gani hizo za kufurahisha! Na alikuwa mjinga kiasi gani kutotambua kwamba hakuwa anatambuliwa na kuheshimiwa!

Hakika, wito na kumuita Mwenyezi Mungu lilikuwa jambo muimu kuliko kuwa Rais wa taifa lenye uwezo mkubwa. Rais Gerald Fitzhug alikiri hayo. Waliyokuwa wakifanya yalikuwa muhimu hata ingawa Reinhard hakuwa akitambulikana katika ufalme wake huo. Reinhard aliomba kupata nguvu ili kupata nguvu na kubaki mwenye imani, na kumshukuru Mungu kumuwezesha kutekeleza jukumu kama lile.

* * *

Kinyume, Dangchao na Pius walikuwa wamehangaika, kwa kupoteza mwelekeo katika juhudi zao za kuongoza ulimwengu. Pius alikuwa ni ibilisi tu kama Dangchao wakati huu. Huku akiwa amejifunza kutekeleza miujiza ya kishetani kutoka kwa Dangchao. Pius kwa aibu alikuwa akitembea karibu na ile sanamu iliyokuwa katika eneo la hekalu, huku akisujudu na kumuinamia Dangchao na kumuita majina ya heshima na hadhi, huu ulikuwa ni ushahidi kamili jinsi alivyokuwa akimuabudu binadamu/mnyama.

Sanamu ile ilikuwa imenusurika kutokana na garika, lakini hekalu zote zilikuwa zimeharibiwa kutokana na garika. Nyota iliyoanguka iliharibu makao ya Pius punde tu nyota zilianza kuanguka. kwa bahati hakuwemo ndani wakati huo.

"Lazima tuwakomeshe," Dangchao alisema alipokuwa akila maankuli ya mchana. "Lazima tuyatafute makao yao makuu. tuwaue wale Mashahidi Wawili, jinsi wanavyojiita. Tusipofanya hivi wataendelea kunawiri. Mateso yatawafaa. Lazima kuna mtu anayejua. Watatuarifu yalipo makao hayo."

"Lakini, Mwadhani," Pius alijibu, "Maumivu huchukua muda. Itadidimiza mauaji. Kila mmoja anahitajika kusaidia kujenga upya. Itahitaji mengi sana kuanza kutekeleza. Kuna mahojiano na wasemaji, wadadisi, maafisa wa kuweka kumbukumbu, maafisa wa kuwakamata, wauaji. Na hata vyumba vya kuhifadhi maiti vimejaa kutokana na maafa ya hivi punde."

"Laani maafa! Wacha walale walipo! Iwapo hatutawakomesha Wakristo hawa, kila kitu kitapotea. Vuka utepe mwekundu. Iwapo wapelelezi watashuku au kufikiri mtu ni mfuasi, nataka mtu huyo auawe. Sijali kama atakuwa na Alama au la. Lazima kuna watu humu ndani wanao wasaidia. lazima tuwatafute na kuonyesha mfano."

Dangchao aliendelea: "Watu watajenga upya baadaye. Nguvu zote zielekee kuwakomesha Wakristo. Tusipo fanya hivyo hatutakuwa na ulimwengu wa kujenga."

Na sasa, ulimwengu ulitazama kwa mshangao na kukosa kuamini kwamba, kiongozi wao mkuu-- mtu waliyemdhania yapata mwaka mmoja na nusu kama kiongozi maarufu ambaye hajawai patikana ulimwenguni--hakujali maslahi yao wala maumivu yao kwa ajili ya tamaa zake za kuwadhulumu Wakristo.

Dangchao alikuwa ameshawishika kwamba Wakristo ndio waliokuwa wakiangamiza ulimwengu, alitumia makarani wake na mojawapo ya waandishi mashuhuri kuhakikisha kwamba ujumbe huo unafikia wengi. Alifaulu kueneza ujumbe huo wa uongo dhidi ya Wakristo na kutoa taswira ya kwamba hao ndio waliokuwa wameapa kuangamiza dunia. Haya yaliwapelekea hata majirani kuanza kupigana na kuuana hata kwa visingizio visivyokuwa vya kweli. Maafa na mauaji yaliendelea, lakini watu wanane kati ya kumi waliokufa walikuwa ni wale wenye alama iliyo jikita katika mikono yao ya kulia!

Matokeo ya hasira za Dangchao, yalifanya hata idadi kubwa ya wafuasi wake kuungama na kumwacha. Walidhani kwamba, hata ikiwa ni mauti, heri wafe kwa njia ya haki na upande wa kweli.

Wale Mashahidi Wawili hawakuchoka kuwahimiza katika hekima yao "Iwapo tutakufa hatimaye," walisema, "Basi ni heri kufa kwa kutetea Mungu au kwa kumtetea shetani? Huu ndio ukweli na ujumbe ambao umekuwa ushuhuda wa injili karne nyingi zilizopita, iwapo dunia imetusonga au la."

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Maafa yanayofuatia baada ya milio ya kwanza minne ya "tarumbeta" ya Huzuni Mkuu (Ufunuo wa Yohana 8:6-12) yameelezwa katika sura hii. Ni ajabu kwamba neno "Chernobyl" ni jina la Kirusi la mmea wa sumu ujulikanao kwa kimombo kama "wormwood" Maelezo yaliyo kwenye kifungu cha Ufunuo wa Yohana 8, yanatuarifu kwamba nyota itakayolenga dunia itajulikana kwa jina hilo.

Sura hii pia inatoa maelezo kuhusu uwezo watakao kuwa nao wale Mashahidi Wawili. Somas Ufunuo wa Yohana 11:6.

Funzo kuu hapo ni lile la uongozi. Udhalimu wa utawala wa Kilimwengu ni kuhusu heshima, utajiri, mamlaka na kutambulikana. Lakini hali ya unyenyekevu na kujitoa na hatimaye kufa kwa "Mwanakondoo" ndiyo inayosimulia juu ya ufalme wa mbinguni.

Ni aibu gani kwa Constantine kukosa nafasi ya kujifunza kama vile Fitzhugh anavyoelewa katika sura hii, nini maana yakuwa kiongozi wa kweli katika ufalme wa mbinguni! ni hadi pale watu watakapo fahamu ndiposa viongozi wa mataifa yenye uwezo wataelewa na kuwa wahudumu bora wasiotumia mamlaka yao kuwaangamiza au kuwadhulumu wenzao, na "kutumia nguvu zao" kuleta faida kwa Mungu na watu wake.

Pius anawakilisha hatima ya wale ambao watatumia mamlaka yao kwa njia zisizofaa na kumuasi Mungu kwa kuwacha yale tunayopaswa kutenda ili kuona ufalme wake.

 

 

21. Apollyon

 

Vita kati ya Dangchao na Wakristo vilipamba moto, na vikaendelea huku miaka tatu na nusu ya Huzuni ikikaribia kukamilika.

Katika kipindi cha miaka miwili tangu Dangchao kusitisha kutoa kwa kafara, na kuingia kwenye Hekalu kule Yerusalemi, pande zote zilihesabu mamilioni waliokata Alama, na mamilioni zaidi waliochinjwa kumfurahisha Dangchao.

Ingawa Pius alikuwa mwenye akili timamu kuliko huyo muasi wa Yesu, alikuwa anaendelea kuadhiriwa. Ilikuwa ni tamaa, iliyowavutia, lakini ilikuwa ni tamaa iliyotawaliwa na maovu na kufanya uongozi wao kuwa wa kikatili.

Hata ingawa Dangchao na Pius walikuwa wakiua watu wengi kuliko vile Rayford na Chaim walikuwa wakipokea watu walio zaliwa upya., hakika Wakristo walikuwa wakishinda vita vya kiroho. Idadi ya watu waliokuwa wakiomba kuwa wanachama wa msukumo wa huzuni ilikuwa ikiongezeka kila siku licha ya mauaji.

Kuanguka kwa nyota kuliwacha maafa na mamilioni ya watu walioaga dunia. Sio shirika la umoja wa Mataifa au Serikali za umoja huo zilikuwa na uwezo wa kukabili maafa yaliyokuwa yakitokea. Dunia ilionekana kurudi katika nyakati za giza. Watu kila mahali walikuwa wameteseka. Dangchao bila shaka alikuwa akipoteza umaarufu.

Lakini kuchoka na serikali za kilimwengu haikuwa sababu ya watu wengi kujiunga na Ukristo. Watu waliojiunga na ule Msukumo walikuwa wakifuata shuhuda za wale waliotangulia. ushuhuda uliodhihirika hata walipokuwa wakiuawa. Hakika kulikuwa na kitu bora baada ya maisha haya, na hawa wafuasi wa Yesu walikuwa wametambua!

Mbali na wale mashahidi wawili kuwindwa na Dangchao pamoja na Pius, walikuwa wamehutubia waandishi wa habari mara kadha kule Sydney na mkutano mmoja kule London.

Matokeo ya mikutano na wanahabari yalidhihirisha kwamba, Dangchao hakuwa na uwezo juu yao. Wanajeshi waliokuwa na silaha walitumwa kuwashika au kuua Rayford na Chaim; lakini kila mara, kundi hilo la wanajeshi ndilo lililoangamia, wale Mashahidi wawili waliongea tu neno moja na kundi la wanajeshi kuanguka, na matumbo yao kuliwa na funza.

Wakati Rayford na Chaim walikuwa wakiufunga mkutano na waandishi wa habari, waliongea mara moja na waliohudhuria mkutano ule walikuwa vipofu kwa muda. Katika heka heka hizo wale mashahidi wawili waliondoka kutoka eneo lile bila kuonekana.

Mikutano na waandishi wa habari ilifaulu sana hasa kwa shughuli za Kikristo.

Wale mashahidi wawili waliongoza vita hivyo kwa ufasaha na kujibu maswali na maojiano kwa njia iliyowavutia na kufurahisha ulimwengu mzima. Chochote walichosema kutoka upande mmoja yalikuwa haki ule upande mwingine. Walitumia lugha nyepesi kuwaeleza watu kwamba nia ya Mwenyezi Mungu ni kutaka watu kuishi vizuri huku wakimtambua kama Muumba wao. Walieleza kwamba Dangchao, Pius na wengine wale waliwekwa duniani kama vibaraka kujaribu imani ya watu. Walimaliza kwa kutoa wito kwa watu kuwacha mienendo mibaya, kukoma kuwafuata waasi wa Bwana na kutozingatia Alama ili waweze kupata uponyaji wa milele kwa kumti Mungu na Yesu mwanawe kabla ya kila mmoja kupata laana. Hawakuweza kufafanua aina ya laana itakayowakumba.

"Utatamani kufa ili uepuke," Rayford aliwahakikishia. "Sitataka kumuombea yeyote apate hayo. Lakini itatendeka. Mniamini. Mko na muda mchache kuungama. Tafadhali, kwa faida yenu, mbadilike hivi sasa. Kuukata mkono wako hakuwezi kulinganishwa na yale yanayotarajia kutokea iwapo hautaungama sasa hivi."

Mkutano huo wa waandishi wa habari uliletwa moja kwa moja kutoka eneo hilo na kusikika dunia nzima, na ukapelekea watu wengi kujiunga na Msukumo uliokuwa umewakumba Wakristo. Watu walikuwa wengi kwa yale makabila Kumi na Mbili kuweza kuhudumia kivyao; hivyo basi watu ambao tayari walikuwa wamejikata mikono waliitwa kusaidia.

Haikuchukua muda mrefu kwa Ulimwengu mzima kutambua na kuunga mkono Ukristo.

Dangchao aliyekuwa ameumia sana tangu kuanza kwa mikutano na waandishi wa habari, alikuwa tayari amerukwa na kichwa.

"Sisi ni vibaraka?" alipaza sauti, wiki kadhaa baada ya kuripotiwa kwamba Rayford na Chaim walimuita hivyo. Alitupa gazeti baada ya kusoma sehemu hiyo.

"Vibaraka? Wamedhubutu!" Alipunga mikono yake kwenye hewa huku akitingisa kichwa kwa masikitiko huku akiongea kwa sauti ya juu. Wanahabari walikuwa wamechukua neno hilo moja na kulitumia katika habari zote zilizohusu Makabila Kumi na Mbili.

Dangchao alishikwa na kichaa ndani ya chumba chake, huku akipiga fanicha na kujigonga huku na huku na kurusha vitu. Alitupa chungu kikubwa cha maua kwenye kio. Pius alikuwa kadhalika na uso wenye wasiwasi. Alikuwa ameanza kuzoea hali ya Dangchao.

"Nitawaonyesha vibaraka ni akina nani, na ni nani anayesukuma nyuzi za kuongoza vibaraka! Nitawaonyesha!" Dangchao alisema.

"Apollyon! Amka hapa! Apolioni!"

"Naam, bwana!" Na mara moja upande wa mkono wa kulia wa Dangchao kulisimama kiumbe cha ajabu na cha kutisha na chenye nguvu za kishetani. Uso wake ulikuwa wa kutisha kuliko kitu chochote ambacho Pius alipata kuona. mbali na ile sura nyingine ya Dangchao. Pius kwa uoga alijificha kando akidhani kwamba kiumbe hicho hakimuoni.

“Apolioni, leta jeshi lako!"

"Yaani niwalete hapa juu?" Apollyon aliuliza kwa mshangao.

"Ndio walete hapa juu!" Dangchao alisema kwa sauti. Na uso wake ukabadilika katika sura iliyomtisha Pius. "Nataka ulimwengu kufahamu nguvu nilizo nazo. Nataka waonje ninachoweza kufanya. Ninataka kuwafundisha adabu wale Wakristo."

"Lakini wataumiza watu wetu. bwana," Apolioni alisema. "Twahitaji kufanya hivyo leo? Kabla ya wakati?"

"Najua ninachofanya!" Dangchao alisema. Iwapo siwezi kuwapeleka jehanamu, basi nitawaletea jehanamu!" Alifurahishwa na jinsi alivyotamka usemi huu, na kuangua kicheko chake cha kishetani. "Wanachukua wafuasi wangu. Nina fursa ya kuwahangaisha hivi sasa.kabla wakufe!" Na kicheko kikarudia tena.

Pius hakuwa na hekima kuhusu kuangamiza watu wao, lakini iwapo matendo ya Dangchao yangalisababisha mahangaiko kwa wakimbizi.(Jina la pius kwa wale mashahidi wawili; hakutumia neno Wakristo, kwa sababu lilimkumbusha dhehebu lake la hapo awali.) Iwapo mipango ya Dangchao ingaliweza kusababisha mahangaiko kwa Makabila Kumi na Mbili, basi ilikuwa bora "kufanya maafa makuu" kama alivyosema Dangchao.

"Sasa, Apollyon! Fanya hivyo sasa!" Dangchao aliwika, na sura yake ya kishetani kuwaka akitazamia kuona yatakayo tendeka.

Sakafu ya chumba kile ilipasuka katikati na kurarua kile kitambaa kilichokuwa kimetandikwa pale huku sakafu iliyokuwa imepambwa ikiharibiwa. Moshi ulitoka humo ndani.mwingi, moshi wa rangi nyeusi, na kujaza kile chumba, kujaza ikulu, na kuingia mitaani, na kujaa kote Yerusalemi. Watu walishindwa kupumua.

Kisha baadaye ndani ya ule moshi, kulisikika sauti kama ya kikosi kilichokuwa na silaha na makelele. Mwanzoni haikusikika kisha kuendelea. Watu waliokuwa na eneo lisilo na moshi mwingi ndio waliotazama mahali kulikotokea sauti, na kisha kugeuka na kukimbia.

Lilikuwa ni wingu la nzige. au viumbe waliokuwa kama nzige. Lakini walikuwa na sura ya ajabu. Miili yao iliyokuwa na silaha na mabawa yao ya chuma yalitoa sauti kama ya askari walio na farasi. Kwenye mkia kulikuwepo chenete iliyo kuwa kama ya kisusuli.

Nzige hawa hawakuvamia miti, nyasi au mimea. Badala yake watu ndio walioshambuliwa. Viumbe hao walikuwa na meno yaliyouma kabla ya kuwachilia chenete zilizokuwa na sumu. Uchungu huo haukuwa wa kuvumilia. uchungu kushinda ule wa kujifungua. Ile sumu iliwafanya waadhiriwa kupooza na kuguna kwa uchungu na kujikokota chini kwa saa mbili au tatu kabla ya uchungu kupoa. Dawa za kupoesha uchungu hazikuweza kufanya kazi, aidha hatukuwa na dawa.

Watu wengi walishambuliwa mara kadha licha ya kujaribu kuepa janga hilo.

Viumbe hao walizidi kutoka kwenye ule moshi mweusi siku ile. Walitoka Yerusalemi na kuelekea sehemu zote za dunia. Viumbe hao walitarajiwa kuadhiri ulimwengu kwa miezi mitano huku wakishambulia yeyote waliyempata mbele yao.

Isipokuwa tu wafuasi wa Makabila Kumi na Mbili. Labda kile chembechembe kilichopachikwa ndicho kilicho wavutia viumbe hao. Au ilikuwa ni upako wakuepusha wale 144,000. Kwa viwango vyote, haikuchukua muda kabla ya Rayford na Chaim pamoja na vyombo vya habari waliona jinsi Dangchao alivyojikejeli.

Rayford na Chaim walitabiri hali ya ukiwa kote duniani.maumivu ambayo yangaliwafanya watu kutamani kufa. Walikuwa wameeleza kuhusu laana, lakini Dangchao mwenyewe ndiye aliyekuwa "kibaraka" na ilidhihirika wazi wazi. Viumbe wake wa mabawa ya chuma, meno makali na chenete za sumu, yalikuwa ni kinjo jinsi jehanamu ilivyo. Mwenyezi Mungu aliwaepusha waja wake kutoka kwa shambulizi la Dangchao!

Msukumo wa mahangaiko haukuwa kama Makabila Kumi na Mbili yaliyochanjwa kutokana na nzige, lakini uchungu kwao ulikuwa tu kama kuumwa na nyuki na sio kama vile wale wengine walivyokuwa wakiumia.

Wakati Wakristo kutoka kwa Makabila Kumi na Mbili au kutoka kwa msukumo ule, walipowakaribia wenzao walioadhiriwa, waliweza kuwaliwaza, kuwaombea na kuwapatia aina yeyote ya msaada wangalitoa. Uchungu haukuondoka lakini ukabaki kama shuhuda, sio tu jinsi Mungu alivyo na uwezo wa kuwatunza wajaa wake, lakini pia jinsi Wakristo walivyo na upendo, hata kwa maadui.

Sehemu zingine za dunia.wale ambao hawakuwa wamemfuata Yesu. walikuwa wakiendelea kukaidi. "maadui" wengi wa Mungu na wale wafuasi wake. Upendo wa aina yeyote kutoka kwa Wakristo ulizidisha chuki.

Hata ingawa mamilioni yalibadili na kumfuata Mungu, wengi wa watu duniani waliendelea kumfuata Dangchao. Waliamini uongo wake kuhusu wale Mashahidi wawili, kwamba ndio waliokuwa chanzo cha maafa yote duniani., na kwamba walidhihirisha ukatili kwa Mungu.

Miaka mitatu na nusu ya Msukumo wa Mahangaiko ilikuwa imesalia mwaka mmoja kufikia ukingoni wakati janga la nzige lilipofikia kikomo. Miezi mitano baada ya kuwasili, nzige walirudi Yerusalemi, kila mmoja akiwa amezunguka dunia. Wingu lingine la moshi mweusi lilikumba mji ule, viumbe hao waliruka ndani, na kisha wingu hilo la moto kupungua na kutokomea kwenye shimo la makaazi ya Dangchao, kwa pamoja na viumbe wale.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Maelezo kuhusu "nzige" yametolewa kwa upana katika Ufunuo wa Yohana (9:7-10) waweza kuwa wadudu wa kizazi kisicho cha kawaida, mashetani (malaika waliasi) au viumbe katili vilivyonaswa kwenye mashine, kama sura yake ya uharibifu inavyoeleza.

Kwa ulimwengu unaochukulia jehanamu kama hekaya, na kwamba shetani ni mzaha, sura hii yaweza kuwa ya kutatanisha. na hata kuhangaisha.

Lakini fikiri jinsi ingalichukuliwa miaka mia mbili iliyopita, kama tungaliongea juu ya simu za rununu, tarakilishi, roketi, mabomu ya atomiki, na miali ya Laser. Miujiza ya mungu ni miaka kama mwangaza mbele yetu, hivyo basi kuna mengi kuliko vile sisi tunaoishi katika karne ya Ishirini na Moja tunavyoweza kutambua na kuelezwa na sayanzi kuhusu maisha, dunia na kila kitu

Tunaamini kwamba Mungu hufanya kazi kwa utaratibu wake . Aidha tunaamini kwamba Mungu anao utaratibu wa sheria zote. Kwa hivyo kuna sehemu ambazo hatujaanza kugusia.

Uchawi, hekaya, vyombo visivyotambulikana angani (UFO) na mambo mengine ya kutisha yanachukuliwa kwa umuhimu sana siku hizi. Mbona tusiamini kazi za malaika, shetani, laana na uponyaji wa kiroho, hasa tunapo pata ujumbe huu kutoka kwa maandiko matakatifu kama Bibilia?

 

 

22. Safari ya Yerusalemi

 

Katika kipindi cha miaka mitatu na nusu iliyopita, vifo na uharibifu yalikuwa mambo ya kawaida kote ulimwenguni. Maisha mengi yalikuwa yamepotezwa kutokana na vita vya kikatili katika kipindi hicho kuliko ilivyowai kutokea katika historia.

Nchini Uingereza Miji kama vile Swansea na Plymouth ilikuwa imeoshwa kutokana na wimbi kuu la bahari. Miji kama vile Liverpool pia ilikuwa imeadhiriwa na kupoteza maisha ya watu. Uingereza ilikuwa imejaribu kufanya ukarabati kuliko mataifa mengine (Hasa katika Afrika na Amerika ya Kusini na Kati) mataifa ambayo yalikuwa yameadhirika kutokana na mawimb; lakini hayo hayakutoa maelezo mengi. Kuzika mabaki ya watu ndilo lililokuwa jambo la dharura. Shughuli za marekebisho ziliwekwa kando.

Miji ya pwani iliyowachwa ilionekana kwa wingi kama dhibitisho la Msukumo wa Mahangaiko, huku watu wengi wakitafuta hifadhi. Watu waliokuwa katika maeneo hayo waliweza kutafuta samaki, hata ikiwa hawakupata mabaki ya vyakula kama ilivyokuwa katika miji mingine.

Umoja wa Mataifa ulitangaza Uingereza Kama "Nchi ya Ulimwengu" punde tu baada ya kuanguka kwa Amerika, kuonyesha kwamba ilikuwa chini ya Umoja wa Mataifa. Majeshi wa umoja huo walitii amri. Maazimio yote ya Umoja huo yalifanywa kulingana na uamuzi wa Katibu Mkuu Levi Xu Dangchao.

Uingereza ilikuwa imewapoteza watu milioni kumi kutokana na mauaji yaliyotekelezwa na Umoja wa Mataifa.

Yote haya yalizidishwa na kujifanya viziwi kutokana na idadi ya mauaji. Kwa wale waliomfuata Dangchao, ilikuwa ni dhihirisho la wazi kwamba mioyo yao ilikuwa migumu, hata kwa vilio vya watoto waliokuwa wakiuawa au kufanyiwa ukatili. Wakati wapenzi wao wakiuawa, walizidi kumkasirikia Mungu.

Kujifanya kiziwi ili kumtumikia Mungu, ilimaanisha kwamba walimtukuza Mungu na maadili yake--kitu ambacho hawakutilia mkazo wakati maisha yalikuwa ni rahisi. Mauaji hasa yale yaliyokuwa ya papo hapo kama kwa kisu kile chenye makali, ilikuwa ni tiketi ya kuelekea mbinguni moja kwa moja. Hatukuwepo na matumaini kwao katika ulimwengu, ila tu kuwashawishi wenzao kujiunga na imani yao kwa Mwenyezi Mungu na kukataa yote yaliyokuwa katika utawala wa Dangchao.

Lakini ilikuwa kama kwamba kila mmoja--wabaya na wazuri--walikuwa wakiishi katika hali ya masikitiko.

Jambo la kuhuzunisha sana lilikuwa mauaji ya watoto. Wazazi walipaswa kushikilia watoto wao mbele ya mashine ile ya kunyonga na kukata koo kwani nafasi iliyokuwemo ilikuwa kubwa kuliko vichwa vyao vidogo. Watoto wale bila shaka hawakuwa na Alama. Lakini sharti lilikuwa kwamba mayatima kutokana na Msukumo wa Mahangaiko walipaswa kupata alama kwa lazima na kisha kutunzwa katika makao ya Kiserikali.

Utawala haukutaka kuwatunza watoto wengi, lakini walichukua jukumu la kikatili kuwauliza wazazi iwapo walitaka watoto kukatwa na ile mashine au serikali iwachukue. Wengi walichagua mashine.

Watoto wakubwa (wale wenye umri wa miaka zaidi ya saba) walipaswa kutoa uamuzi wao. Wengi walichagua kufuata mamlaka, na hilo lilisababisha maafa zaidi kuliko mashine.

Watakatifu walikuja kuona iwapo ilani aliyotoa Yesu, ikiwaarifu wateule kuomba kwamba wasipate mimba au kuwa na watoto wadogo katika kipindi kitakachofuatia Msukumo wa Mahangaiko.

Vitendo vya ngono havikukoma miongoni mwa wafuasi, lakini sio kwa wingi kama ilivyokuwa kabla ya dhiki kuu. Hakuna aliyetaka kupata mtoto nyakati hizo za majaribio, mpango wa uzazi ulikuwa ni ghali kwa wale wateule kukidhi. Hali ya umati mwingi wa watu pia ilipunguza kuwepo kwa siri.

Wale waliokuwa wakitaraji kuuawa walifikiri sana. Na Makabila Kumi na Mbili yaliidhinisha hali ya kutooa, au kushiriki katika vitendo vya mapenzi. Wawili waliotaka kuoana walipewa kazi nyingi na kuwa pamoja na manyapara kila mara. Iwapo uamuzi wa kuoana uliafikiwa, ulifanywa bila kubusu au kukumbatiana. Sherehe fupi ilifanywa baada ya uamuzi kama ule.

Watu waliooana miongoni mwa Makabila Kumi na Mbili, walitengwa kwa muda mrefu; lakini walipaswa kukumbuka jinsi maisha yalivyokuwa magumu.

Kulikuwa na wachache kati ya wanachama walio kwenda kinyume. Lakini hilo liliwapa nguvu waliobaki.

Tulikuwa halikadhalika na majeruhi miongoni mwa Makabila Kumi na Mbili. Hata ingawa hakuna yeyote ambaye alikataa Alama alipata maafa kutokana na wale wadudu, kulikuwa na baadhi ya wanachama walioshikwa na polisi, wakati walipokuwa wakisaidia walio jeruhiwa kutokana na Msukumo wa Mahangaiko, na hata kulikuwepo na ulegevu wa kiusalama na kusababisha maafa. Vifo kutokana kwa njia hii, havingaliepukika, lakini mamlaka ilisita kuwatesa wale waliokosa alama, huku wakitumai kwamba walikuwa na maelezo zaidi kuhusu walipokuwa vviongozi wao.

Wengi walikuwa wamejisalamisha kwa mateso, na kusababisha kukamatwa; lakini njia kama hii haikuwa kawaida sana.

Wafuasi wapya katika mwanzo wa miaka ile tatu na nusu ya mwisho (wale ambao hawakuwa na Alama) wangalijaza pengo kutokana na wale waliohama kutoka kwa muungano wa Makabila Kumi na Mbili, ili katika mwaka mmoja uliobaki walikuwa karibu 144,000.

Lakini mwishoni mwa mwaka, idadi yao ilipungua kiajabu. Ndio waliobaki. watu waliokuwa duniani waliokata Alama. Kwa haraka walikuwa wakinyauka.

"Nini kilikumba ulinzi wetu?" Chloe aliuliza kupitia barua-pepe ya dharura kwa Rayford, pale Maria Teresa alipigwa risasi na kuuawa kule Roma.

"Ulinzi sio hakikisho," Rayford aliandika kwa kujibu wafuasi wote. "Mungu huwachilia mvua kunyeshea wazuri na wabaya. Jeshi lolote lililoshinda vita halikosi majeruhi, na tumewapata pia. Lakini tazama mbali tulikotoka. Hakika Mungu yuko nasi.

"Neno `waathirika' linamaanisha `Yule anayeishi juu'. Tunaweza kuwa hai katika mwili, na hiyo ni njia moja ya kuishi. Lakini kuna ushindi mkuu baada ya kupambana na adui wa mwisho--kifo--na kisha kuibuka kama mhanga. Ujumbe wa ufufuo ni kwamba kifo sio mwisho. Hufanya tofauti.

Kama alivyosema Mtume Paulo, kama hakuna ufufuo, basi sisi ni watu tulio taabani. Lakini kwa sababu kuna kufufuka, tutaishi--hata baada ya kuuchukua uhai wetu. Tutanusurika! Tutaishi zaidi ya hayo yote!"

Hata hivyo yeyote kati ya wale wahanga wa Makabila Kumi na Mbili aliyekuwa hai, alikuwa akihesabu siku katika miezi ile ya mwisho.

Ilipokuwa imebaki wiki mbili, Rayford na Chaim waliona ni bora waanze safari ya kuelekea Yerusalemi. Wote walifahamu kwamba ingaliishia kwa kufa, hivyo basi walipowaaga wenzao, ilikuwa ni kwa uzito kutoka ndani ya mioyo yao.

Jambo la kushangaza ni jinsi Irene alivyokuwa na amani kuhusu kuondoka kwa Rayford. Yeye ndiye aliyemjulisha ya kwamba walikuwa wameishi pamoja kwa miaka mingi kuliko wachumba wowote walio wajua. "Hesabu siku" alisema kwa kukumbatiana kwa mwisho. "Hesabu siku"

Mashahidi wale wawili waliwacha nyuma tarakilishi zao--chombo cha kipekee cha mawasiliano kati yao na Makabila Kumi na Mbili. Walichukua nguo chache za kujibadilisha na vifaa vingine vya usafi-- hakuna la ziada.

Rayford alikuwa na mbinu za kufika huko, lakini Chaim alipaswa kuabiri ndege ili kutoka kule Australia.

Chaim hakuwai kupata kuooa, na labda kutokana na hilo alikuwa na uhusiano wa karibu na waja kazi wake. Machozi yalimtoka alipowaaga. Alikuwa ni mkubwa kwa umri ukilinganisha na Rayford, na mwenye nywele ndefu za hudhurungi zilizokua kwa sababu ya kukosa wembe. "Ilikuwa ni hali ya kimaumbile kuziwacha nywele zangu kukua," alisema.

Mwishoni mwa mwezi wa Novemba jumapili moja jioni, Chaim alienda kwenye uwanja wa ndege wa Kingsford Smith kule Sydney. Hakuwa na uhakika jinsi ya kutoka nchini humo. Hakuwa na tiketi, pasipoti, visa, pesa, na wala kitambulisho, na muhimu zaidi, hakuwa na Alama. Alipita katika vitengo vya ukaguzi bila kizingiti.

Mamlaka ya uhamiaji nchini Australia yalikoma kukagua stakabadhi za wasafiri miaka kadha iliyopita.

Aliweza kupata ndege ya shirika la El Al kuelekea Tel Aviv kupitia Bangkok. Wakati wasafiri waliitwa, Chaim aliingia kwenye safu. Mwanamke aliyekuwa mbele yake alikuwa na kisulusuli cha kuanguka cha ajabu tiketi yake ilipokuwa ikikaguliwa. Huku wahudumu wa shirika lile walikuwa wakimhudumia mwanamke yule, Chaim alinyenyekea na kuingia ndani ya ndege. Ilikuwa ni rahisi tu kiasi hicho. Ndege ile haikuwa na wasafiri wengi, hivyo basi Chaim alingojea katika chumba cha mapumziko kwenye ndege ile hadi pale wasafiri wote walikuwa wameketi, na kisha kuchukua kiti ambacho hakikuwa kimekaliwa.

Kwa utaratibu ndege ile iling'oa nanga kuelekea Bangkok. Ilifikia kiasi chake na kisha kuanza mwendo. Chaim alikuwa akimshukuru Mungu jinsi mambo yalivyomuendea sawa, wakati mhudumu wa ndege alikuja alipokuwa akainama na kumuambia "kiti hiki hakijaorodheshwa kama kimelipiwa." alisema kwa upole. "Umesonga kutoka kiti kingine?"

"La, hiki ndicho kiti ambacho nimekalia tu," Chaim alimuambia yule mwanamke kwa kutabasamu na kuvinya jicho.

"Tafadhali waweza kunionyesh pasi ya kuingia?" yule mhudumu aliuliza.

"Nasikitika kwamba sina," Chaim alimuambia huku akitabasamu.

Yule mhudumu alionyesha sura ya ukali. "Waweza kunionyesha tiketi yako?"

"Ukweli ni kwamba sina hata tiketi," Chaim alimjibu kwa moyo wa mapenzi.

"Tafadhali ngojea tu hapo," yule mhudumu alisema akiondoka kwa haraka kutafuta wazo la pili kabla ya kuchukua hatua.

Sijui anafikiri nitaenda wapi huku juu, Chaim alifikiri huku akimngojea.

Katika chumba cha wahudumu, Hattie yule mhudumu alimuonyesha mhudumu mkuu alipokuwa ameketi Chaim.

"Wamuona yule mtu aliyeketi pale katikati kwenye safu ya sita kuelekea pale mwisho?" Hattie alimnong'onozea. "Hana tiketi".

"Kweli?" akasema mhudumu mkuu kama kwamba hilo lilitoa maelezo yote. "Nilimuona alipoingia. Nilidhani kwamba alifanana na mmoja kati ya wale mashahidi wawili. Uliwaona kwenye ?"

"Hakika ndio!" Hattie alisema huku akitazama maungo ya Chaim. Chaim aliona wawili hao wakimtazama na kisha kuwapungia mkono kama ishara ya salamu za kirafiki.

"Hii ni ajabu sana," Daudi alisema huku akielekea mahali Chaim alikuwa ameketi.

"Wewe ni mmoja kati ya wale Mashahidi, au sio?" Daudi aliuliza. "Nimeshautazama mtandao wenu."

Alimtazama Hattie, aliyempa matumaini kwa kusema, "Sio ajabu, Daudi. Kila mmoja ameutazama."

"Ahsante," Chaim alisema na kumsalamia Daudi.

"Sasa unafanya nini kwenye ndege hii?" Daudi aliuliza.

"Nasafiri kuelekea Tel Aviv. Kuna mambo fulani kule Yerusalemi."

"Lakini wahitaji tiketi ili kusafiri."

"Lazima muelewe kwamba siwezi kununua tiketi bila Alama; nami sina Alama,"

"Nitaongea na wakubwa wangu, na labda itabidi ndege ipinduliwe ili urudishwe Sydney. Hata iwapo watakuwacha, tutakuwa na askari wakikungojea kule Bangkok, unafahamu hayo?"

"Wadhani kwamba Mungu hawezi kunifikisha Yerusalemi?" Chaim alimuangalia Daudi na kumuuliza huku kichwa chake kimeegemea upande.

"Ndio, nimesikia hadithi. na hakika sitaki nikukasirishe!" alicheka. Lakini bila shaka hautatekeleza jambo baya, hasa kwenye ndege, ama?"

"Kusema kweli," Chaim alisema akimuashiria Daudi kuinama ili aweze kunong'ona, "Sina uwezo. Nafahamu tu muda mchache kabla ya tukio. Naamini kwamba Mungu ndiye anayefahamu aina ya kinga ninayohitaji."

"Nitaongea tu na Rubani kisha nikujulishe," kijana huyo alisema.

"Ahsante," Chaim alitabasamu, na kisha kurejelea kusoma gazeti alilokuwa akisoma walipo ng'oa nanga.

Katika chumba cha rubani kulikuwa na majadiliano ya faragha na kisha simu kupigwa Sydney.

"Anasema kwamba tutakuwa na hali ya makabiliano," Yule rubani alisema.

Maelezo yalitoka kule kwamba wasifanye lolote la kumkera Chaim, na kwamba waende tu Bangkok ambako mamlaka itajulishwa.

Lakini mtu mmoja katili aliyefanyia shirika hilo la ndege kazi, alipiga simu kule Israeli, na kutoa ujumbe kwamba habari ziwasilishwe kwenye makao ya ikulu. Wakati ndege ilipotua Bankok saa nne usiku saa za huko, mawaidha yalibadilishwa. Chaim alipaswa kubaki ndani ya ndege hadi saa sita za usiku kisha apelekwe Tel Aviv. Sherehe za kumkaribisha zilikuwa zaandaliwa katika uwanja Ben Gurion asubuhi itakayofuatia.

Ujumbe ulifika kule Tel Aviv, na habari kwenye runinga zilieleza kwamba Chaim alikuwa ameteka nyara ile ndege. Nusu ya wanahabari wote iliwasili katika ule uwanja wa ndege, kwa pamoja na kile kilichoonekana kama jeshi nzima la Umoja wa Mataifa.

Wakati ndege ilipotua kule Tel Aviv, ilielekea katika sehemu ya mapokezi ya raia wa nchi ambayo yalikuwa yamewekwa usalama. Chaim alikubaliwa kushuka kivyake huku ndege ikielekea mahali pa kupokea abiria wa kigeni pamoja na wale wasafiri wengine.

Chaim alipitia mlango ulioelekea chumba cha mapokezi huku mianga kutoka kwa wapiga picha ikiwaka. Alipungia mkono wale wanahabari, kisha kiongozi mmoja wa Umoja wa mataifa akaja mbele, akijaribu kuwa mjasiri kwa ajili ya wapiga picha, huku akijifanya asiyemuogopa Chaim kutokana na nguvu zake maalum.

"Nina kuarifu kwamba utaandamana nami" alisema huku akitaraji jibu.

"Bila shaka" Chaim alijibu. Alichukuliwa na kusukumwa kwenye gari la polisi.

Akachukuliwa, sio kwenye kituo cha polisi, lakini ndani ya jumba la kifahari kule Yerusalemi.

"Kwani! Hatimaye tumekutana! Dangchao aliwika huku Chaim akielekezwa kwenye chumba chake cha mamlaka. Kila mmoja aliinama na kusujudu mbele ya Katibu Mkuu, isipokuwa Chaim aliye simama wima.

"Wapi mwenzako?" Dangchao aliuliza.

"Sijui," Chaim alijibu.

"Labda nitakufungia hapa nione kama atakuja."

Chaim hakujibu.

"Tutakuwa na wakati mwema nawe hapa katika Hekalu," alisema kwa hali ya ukaidi machoni mwake.

"Halikadhalika Mungu atakuwa na wakati bora nawe," Chaim alijibu, kwa ujasiri jinsi alivyoongea mteka wake. Dangchao alihisi nguvu za tisho hilo na kunyamaza.

"Ni mzaha tu nataka kumuuliza rafiki yako maswali fulani tu. Twahitaji kufanya kazi pamoja. kwa wema wa dunia."

Kwa mara nyingine Chaim alinyamaza.

Habari ziliarifu kwamba Chaim alikuwa ameshikwa na kuzuiliwa katika ikulu. Dangchao alitumai kwamba hayo yangalimvutia Rayford.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Kufuatia mahangaiko makuu, Yesu alisema kwamba, Wakristo watasalitiwa na kuuawa kutokana na imani yao (Luka 21:16) na kisha kusema (aya ya 18) "Hakuna hata unywele wenu utakao angamia." Hali ya kukanganya inatokea pale Rayford anasema katika sura hii kwamba "Ulinzi sio hakikisho"

Twaweza kufa kutokana na imani yetu, lakini "hatutaangamia". Hiyo ndiyo maana ya "kuishi juu." Hakuna hakikisho kwamba hatutateseka. Kwa hakika mtazamo ni kinyume (Timoteo II 3:12) Bila shaka ulinzi wetu utakuwa wa kirohi na wa milele, na sio wa muda.

 

Hii ndio sababu kwamba maono ya "Mahangaiko" ni muhimu kwa yeyote aliyeamini, kwa kila umri. Tunapovumilia majaribio na hata kutazama mauti, tutajichagua kiroho. Maisha kwa wengi wetu yapaswa kuwa na utulivu na sio matayarisho ya mauti.

Bibilia inasema kwamba wakati wa Nuhu na ule wa Sodoma na Gomora, walikuwa wakifanya tu bidii ya kuoana na kuzaa tu bila kufikiri Mungu; na ni kwa sababu ya hayo kwamba (na sio tu mashoga na walawiti au wasio mtambua Mungu) waliangamizwa. (Luka 17:26-30)

Hata wale Mashahidi wawili watakuwa na upungufu, kama vile Chaim anavyoona katika sura hii.

 

 

23. Mpasuko

 

Ilikuwa ni Alhamisi asubuhi kabla ya Rayford kufika Yerusalemi. Alikuwa amechukua muda mrefu kuweza kujipenyeza kutoka Uropa hadi Mashariki ya Kati. Alisikia kuhusu kutekwa kwa Chaim akiwa safarini. Rayford alielekea moja kwa moja hadi alikokuwa akizuiliwa Chaim katika makazi ya Mtawala, alipofika mji mtakatifu.

Katika safari yake kutoka Uropa, ni watu wawili tu ndio waliomtambua, na hawakuwasilisha malalamishi au uzushi wowote. Lakini hakuwa ameingia Yerusalemi kwa muda usozidi nusu saa, ndiposa watu walianza kunyosha vidole na kunong'onezana. Alipoingia umati wa watu ulimfuata, kuona kitakachotokea. Mtu alipigia waandishi wa habari sumu na neno hilo kufikia ikulu, mahali palipodhaniwa kwamba Rayford anaelekea.

Jambo la ajabu ni kwamba hakuna aliyemuongelesha, kumshika au hata kumkaribia Rayford. Kulikuwa na kitu katika mwenendo wake kilichowafanya watu kumuondokea.

Alipofika mbele ya ukumbi mkubwa unaoelekea kwenye ikulu, alilakiwa na kikundi kikubwa cha waandishi wa habari na majemadari. Kamera ziling'aa na kuwaka huku Dangchao akitoka nje kuelekea kwenye jukwa lile akiwa pamoja na walinzi wake. Majasusi wengine wa umoja wa Mataifa walikuwa wametapakaa kila mahali kushuhudia.

"Karibu! Karibu!" alipaaza sauti Dangcha ili asikike na umati.

"Nimekuja kumchukua Chaim Rosenberg!" Rayford alisema kwa sauti. "Mlete hapa nje!"

"Yumo humu ndani. Tafadhali karibu ndani!" Dangchao alisema huku akisonga kumkaribia Rayford.

Rayford alikaa pale chini ya sakafu, alipokuwa akiketi, kulitokea mtetemeko uliotingisha eneo lile. Yeyote aliyekuwa amesimama alianguka ila tu Dangchao, aliyejikakamua na kuyumbayumba kisha kusimama. Majasusi walianguka kutoka kwa kuta za zilizokuwa katika eneo hilo, na wengi wao wakajeruhiwa. Wengine waliokota silaha zao na kusimama.

"Mlete Chaim hapa," Rayford alirudia huku akinyosha kidole kwenye sakafu kando na alipokuwa ameketi. "Hivi sasa!"

Mtetemeko mwingine uliwaangusha wote waliokuwa wamesimama. Wakati huu Dangchao alianguka vile vile. Kamera za waandishi wa habari waliokuwa werevu na kubaki pale chini zilimnasa katibu mkuu akianguka mbele ya Shahidi wa Magharibi. Rayford alikaa kwa utulivu huku miguu yake aliyokunja ikiwa mbele.

"Sawa basi! Sawa basi!" Dangchao alisema, huku akijaribu kusimama na kumtazama Rayford.

"Mleteni yule mateka!" alimuamuru mmoja wa walinzi wake, na yule mtu akaenda kwa haraka.

"Usijali utapata fursa yako,"Rayford alisema. Hivi karibuni. Lakini kwa sasa utapata matatizo usipomleta Chaim kwangu."

"Mpige risasi!" Dangchao alipaza sauti, kadiri alivyoweza. Lakini wakati huo, Rayford alipumua tu, na miale ya moto mkali ikatoka kumuelekea Dangchao. Waliomuasi Yesu walikimbia lakini hawakukosa miali hiyo, miali ile iligawanyika katika ndimi na kuelekea kila upande. Huku ikienda mbio kuliko mtu yeyote, ndimi zile za moto ziliwafikia kila mmoja wa askari aliyekuwa na bunduki iliyomuelekea Rayford. Wote waliteketea kabla ya kudhubutu kulenga bunduki zao.

"Haupaswi kunifanya nitende hayo," Rayford alimuambia Dangchao kwa upole.

"Mipango yako ni ipi?" Dangchao aliuliza, huku akiwa na wasiwasi. "Iwapo utanihakikishia kwamba hautawacha mji huu nitamuachilia rafiki yako ili muende naye."

"Utamuachilia rafiki yangu bila masharti," Rayford alimjibu kwa upole. "Lakini iwapo itakuridhisha.hatuna mpango waa kuondoka mjini kwa siku kumi zijazo."

Hapo ndipo Chaim alitokea na yule askari.

Dangchao hakuwa na lingine ila kusalimu amri ya wale Mashahidi wawili; lakini baadaye siku ile wale waganguzi wake walifanya isikike kama kwamba wale wanaume wawili walikuwa wamewachiliwa kwa dhamana wakingojea kutolewa kwa hukumu. Kulikuwa na manung'uniko mbona kumwachilia gaidi aliyekuwa na uwezo wa kuteka nyara ndege na mshukiwa wa mauaji kuwachiliwa warandarande hivyo; lakini Dangchao alisisitiza kwamba kila kitu kiko sawa. Kwa hakika ilikuwa. ila tu hakuwa ni yeye aliyekuwa akiendesha hali hiyo ya usawa.

Siku sita zilizofuata, Cham na Rayfoord walichukua muda mwingii karibu na Hekalu la Mlima, walipokuwa na fursa ya kuhutubia umati wa watu. Ilikuwa ni mwanzo wa mwezi wa Desemba, na hali ya hewa ilikuwa na baridi; Lakini wale Mashahidi wawili waliendelea kulala mitaani, huku wakilala kwa zamu. Walikuwa wamekusanya vipande vya nguo na kuni za kutosha, na viungo vingine kuwakinga kutokana na baridi. Waliwasha moto usiku kucha karibu na eneo walilo lala. Yeyote ambaye hakulala, alitengeza moto na kuwahutubia watu.

Usiku kucha watu walikuja kuwaona na kusikiza waliyokuwa wakisema kukashifu Dangchao na wale waliokuwa wakimuabudu. Mara mbili mtu alijaribu kuwaingilia, na mara mbili mshambulizi alikuwa ameangamizwa kwa moto. Ujumbe ulisambaa kupitia vyombo vya habari na haraka zaidi kupitia kwa wale waliokuja kushuhudia; kiasi kwamba umati haukudhubutu kuuliza maswali kuhusu Mitume wawili baadaye.hadi jioni ya Jumatano.

Rayford na Chaim walikuwa hawajapata kuwasiliana na wenzao watakatifu tangu waingie Yerusalemi siku kumi zilizopita. Hawakula sana lakini waliomba sana mara kwa mara siku zile za mwisho. Wakristo wote walifahamu kwamba nyakati za mwisho wa Chaim na Rayford zimewadia. Kulikuwa na vifo na kurudi nyuma miongoni mwa wafuasi wao kipindi hicho cha siku kumi.

Irene na Elaine walikuwa wamenaswa na mamlaka na kisha kuuawa wiki moja baada ya Rayford kuondoka London. Watakatifu fulani pale Yerusalemi walikuwa wamewaeleza wakati wa wiki ile ya mwisho. Ujumbe kuhusu mauaji ya Irene ulimuongezea Rayford uchovu; lakini hakukoma kuhubiri.

Matayo alikuwa amebaki kuwatunza wafuasi wa Makabila Kumi na Mbili na Msukumo wa Mahangaiko baada ya kupotea kwa Irene na Elaine; lakini fikira kuu ilikuwa ni kwamba mambo yanaenda mrama. Tulibakia tu na siku nne tangu muda uliosubiriwa kurudi kwa Yesu kufika.Iwapo hesabu yao ilikuwa sahihi, na wengi walihofu iwapo watadumu zile siku na viongozi wao.

Basi, Jumatano jioni ya ile wiki ya mwisho, mmoja kati ya wale askari wawili wa Umoja wa Mataifa waliokuwa wakiwachunga wale Mashahidi Wawili, kwa kimchezo tu alichora mduara kwa Rayford akitumia mtutu wa bunduki, kwa mzaha tu. Alikuwa amesimama mahali Rayford hakuwa anamuona, na Chaim alikuwa amelala kando ya moto. Hapo tu ndipo yule mwenzake alimfikia ghafla na kumshtua huku bunduki ikifyatuka, na kumpiga Rayford kichwani. Rayford alianguka chini.

"Umemua!" Yule mlinzi mwingine alisema. "Tazama umemuua!" Na kisha kumuona Chaim akitaka kuamuka. "Harakisha! mpige huyo mwingine kabla ya yeye kukuchoma!"

"Ni yeye au mimi, au sio?" askari yule alisema huku akilenga bunduki kwa mara nyingine. Na Chaim halikadhalika alianguka karibu na Rayford. Alikuwa ameuawa kwa kupigwa risasi kichwani.

Rayford alikuwa amekamilisha hotuba yake kwa umati mdogo kabla ya kupigwa risasi, na umati ulikuwa unaondoka tu wakati wa kupigwa risasi. Wale wachache waliobaki pale na kuona Rayford akianguka kisha Chaim, hawakuamini macho yao. Baada ya miaka mitatu na nusu bila mafanikio wakiwindwa na utawala, na kisha baada ya kushindwa kuwaangamiza, askari mmoja alifaulu kuwaua wote, kwa ajali, kisha kwa sekunde na risasi mbili tu!"

Wale askari wawili walikimbia kudhibitisha kwamba, kweli walikuwa wameua wale Mashahidi Wawili, na kisha kuwaarifu wakubwa wao. Ambalanzi ya kijeshi ilikuja mbio kuokota miili ile pamoja na askari wale, na ujumbe kuenea duniani kupitia kwa vyombo vya habari kwamba ulimwengu ulikuwa umeokoka; wale Wakimbizi Wawili (kama alivyozoea kuwaitaPius) walikuwa wamekufa.

Dangchao alikuwa ameamka akihutubia waandishi wa habari huku akipanga mipango mingine. Asubuhi ile alizindua kijengo cha kikatili kilichokuwa kimezingira miili ile ya Mashahidi Wawili. Walikuwa wamerejeshwa mahali walipouawa. Vigae vya moto vilikuwa vingali pale, na vile vifaa walivyookota kuwapa joto vilikuwa vimetapaka pale. Watu walikaribishwa kujionea wenyewe. Wale askari waliotekeleza mauaji yale walitumiwa kuzuia na kuongoza umati wa watu.

Dangchao aliamua kuweka miili hiyo hapo nje ili wakristo wasilete hadithi nyingine ya kufufuka, kama walivyofanya na Yesu wao. Alitaka pia watu kujionea kwamba ni wale Mashahidi wawili waliouawa, na hakika walikuwa wamekufa.

Alisonga hatua mbele zaidi, Krismasi ilikuwa wiki chache tu ili iweze kuadhimishwa., hata ingawa ilikuwa imebadilishwa jina na kuitwa Winterfest, miaka iliyo tangulia, alihisi kwamba huu ulikuwa wakati bora kubali tarehe ya maadhimisho. Alitangaza kwamba siku inayofuata, Ijuma, itakuwa ni tarehe mpya ya kuadhimisha Winterfest. Maduka yote yatakuwa wazi, Ijuma hiyo, katika pilkapilka na heka heka za ununuzi wa mwisho; lakini afisi na maeneo yasiyo ya dharura yatafungwa Alhamisi na Ijuma. Hii ilitoa fursa kwa watu kununua zawadi, vyakula, vinywaji, na siku mbili za kusherehekea. Maduka ya jumla yalipata na kushuhudia wateja wengi sana katika siku hizo mbili kuliko walivyopata kuona. Kila mmoja alifurahi.

Watu waliamini kwamba kizazi cha binadamu kilikuwa kimebadili mkondo. Amani na maendeleo yangalirejelewa! Hivyo basi walinunua vitu na kusherehekea ushindi wa binadumu juu ya "Wageni".

Sherehe zilianza siku ile na kuendelea siku mbili zilizofuata. Jumamosi jioni maduka yote yalipokuwa yamefunga na wafanyikazi kuruhusiwa kuenda kusherehekea, ulimwengu mzima ulikuwa katika maafa ya ulevi.

Lakini jumapili asubuhi kitu cha ajabu kilitendeka Mashariki ya Kati. Ukanda mzima wa maili kumi na tano kuelekea Baghdad, Cairo na Ankara), watu walipotazama juu, waliloona ni kama kio juu kabisa ya ardhi, kio kilichotambaa kila pembe za dunia. Mwangaza ulipenya ndani ya kio kile na kuwafanya kuona vitu vikisonga upande ule mwingine.

Ndege zilizokuwa zikiendeshwa juu ya futi 25,000 zililazimika kutua au kurudi zilipokaribia Mashariki ya Kati.

Dangchao alikutana na washahuri wake waliomuarifu kwamba ilikuwa ni nyota iliyokuwa ya kigeni. Swali kuu lilikuwa iwapo wale walinzi waliokuwa wakiitunza nyota ya kigeni ile walikuwa wazuri. Dangchao alibahatisha kilichokuwa kule juu na kuwaonya wachukue tahadhari.

Kisha, mchana, kulikuwa na mabadiliko katika Hekalu la Mlima. Mtu mmoja alisema aliona mkono mmoja wa wale Mashahidi ukisonga. Dangchao alishangaa na kukimbia katika eneo lile, kwa pamoja na umati uliojumuisha waandishi wa habari.

Kila mmoja aliyekuwa pale alitazama kwa dakika tano bila kuona dalili yoyote. Walipokuwa tayari kufutilia mbali habari ile kama fikira ya uongo, walioana mwili wa Chaim ukitetemeka.

"Uliona hilo?" Mtu alisema. Kwa hakika Dangchao alikuwa ameona, na kushikwa na hofu.

"Mpige risasi!" alipaaza sauti huku akinyosha kidole kueleka kwa Chaim.

"Lakini tayari amekufa!" mlinzi wake alisema. Yeye pia alikuwa ameogopa. Alikuwa amesikia yale yaliyowafika wote wale waliojaribu kuwalenga Mashahidi wawili.

"Sijali kama amekufa au la. Mpige risasi!" Dangchao alisema kwa hasira. Alinyakua ile bunduki kutoka kwa mkono wa yule mlinzi, katika juhudi za kutekeleza mwenyewe. Aliielekeza kwenye kichwa cha Chaim na kufinya ili kuwachilia risasi. Lakini alipokuwa akifanya hivyo, alipata msukumo kutoka kwa ardhi na risasi zake kuelekea upande mwingine. Alirusha mikono (na bunduki) juu hewani ili kupata kusimama wima. Mahali pale pakaanza kutingika na ile miili pia ikatetemeka.

Mtetemeko wa ardhi! Dangchao alifikiri. Kumbe ni hiyo miili ile haikutingika! ilikuwa ni ardhi iliyozitingisha.

Lakini baada ya muda mchache, mikono na miguu ya Rayford na Chaim ilianza kunyooka. Miili yao ikajipinda, na mikono yao kuinuliwa ili waweze kuamuka. wima kwa miguu yao. Walikuwa wameinama huku wakifungua macho yao na kutazama wapotevu.

Lile kovu la risasi lilipotea mara moja mbele ya macho ya Dangchao. Nywele zao ziliimarika huku mvi ukipotea mikunjo usoni ilipotea, na walionekana kama waliokuwa chini ya umri wa miaka thelathini. Matambara ya nguo walizokuwa nazo ilitoka na kuwacha kanzu safi nyeupe.

Wale wanaume walisimama wima huku sauti ikisikika kutoka mahali wasipoona na kusema: "Kujeni huku juu!" kila mmoja alitazama juu na, chini ya kile kio kilichokaribia juu ya Hekalu la Mlima, mlango wa mduara ulifunguka. Lakini "moshi" ulipokaribia, ulitawanyika na kuwa mamilioni ya viumbe wadogo walio na mavazi meupe. Katikati yao kulikuwepo na mmoja aliyeng'aa kiasi cha kusababisha upovu. Wale viumbe wengine walimzingira huku akikaribia chini.

Chaim na Rayford walianza kupaa ili kuwalaki viumbe wale, walipokuwa wakipaa, walishuhudia wengine wengi kutoka katika ardhi wakipaa na kuzingira Kiumbe Kilichokuwa na Mwangaza.

Wale wengine walikuwa wanang'ara na mavazi ya ufufuo, lakini kulikuwa na wachache walio tambuliwa kutokana na nguo zao za kawaida. Hawa walikuwa ni watakatifu waliokuwa hai. Hao pia walikuwa na sura mpya ya ujana. Kovu na aina yeyote ya ulemavu ilipotea. Yeyote aliyekuwa kati ya umati huo alihisi furaha na kujisikia mwenye afya, na habari njema ilikuwa ni kwamba hakuna aliyekosa mkono.

Chini ya ardhi, mtetemeko ulizidi, sasa kwa kasi muno. Mji mzima wa Yerusalemi ulikuwa ukitingizika. Majengo yalianza kuanguka. Kutoka juu walipokuwa wateule ilionekana kama kwamba mji wote ulikuwa ukianguka polepole. Lakini pale chini kulikuwa na garika ya vio, chuma, matofali, vigae na aina nyingi ya vifusi kutoka kwa majengo yaliyokuwa yakiwaangukia wakaazi. Watu waliokuwa wangali wanasherehekea walinaswa na kuangukiwa na majengo kote Yerusalemi.

Wateule walikuwa kule juu pasipo hewa ya kutosha na hali ya baridi, lakini hakuna hata mmoja aliyehitaji kifaa cha kufunika mapua au mwili, walikuwa salama, bila mahangaiko.

Viumbe vyote vilikuwa vikizingira Kile Kiumbe Cha Mwangaza. Rayford na wateule wengine waliozingira Kiumbe kile walifahamu ni nani. Alikuwa ni Mwokozi wao. Alikuwa ni Yesu wao!

Mtu mmoja alianza kuimba na wale wengine wakajiunga. Kila mtu alikuwa akiimba kwa lugha yake, lakini walihisi kwamba walikuwa wanaimba maneno sawa. Yalikuwa ni maneno na nyimbo kutoka kwa Nyimbo za Hallelluya za Handels Masia "Mfalme wa wafalme! Bwana wa mabwana! atatawala milele na milele!"

Walikariri na mara kwa mara; na kila mara sauti iliongezeka, hadi ilipodhaniwa kwamba dunia nzima ingalisikia Hii ilikuwa ndipo! Huu ulikuwa ni wakati ulio tazamiwa na kusubiriwa. Ilikuwa ni kilele cha mipango ya Mungu kwa viumbe wake.

Alikuwa amerudi, kwa hakika. kuhukumu ulimwengu!

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Kuna kitu kuhusu kurudi kwa Yesu kinachoonekana kama sio kweli kwa ulimwengu huu wa sasa. Na hakika sio cha kuaminika kama miiko na hekaya zingine (Ikiwemo jinsi viumbe walivyoumbika) vile binadamu alivyoumbika. Bila hicho, maisha hayatakuwa na dhamani-- ajali tu katika supu ya kiuongo kijulikanacho kama ulimwengu.

Lakini mbona tusiamini Bibilia inavyotueleza kuhusu kurudi kwa Yesu, juu ya maelezo mengine kuhusu maisha na uhai? Kila kitu kinaeleza Bibilia kama kitabu cha historia kinachoweza kuaminika; na kizazi cha binadamu kufaidika zaidi kuliko kitabu chochote kuwai kuandikwa Twapaswa kutenda mema kinavyoeleza huku tukingoja kurudi kwa Yesu.

Tukio hilo kubwa limeelezwa katika njia tofauti na waandishi. Paulo anatabiri kuhusu Mpasuko katika Wakorinzo wa I 15:32-58. Anaanza kwa kusema, "Iwapo maiti hawatafufuka, basi tule na kunywa kwani kesho tutakufa." Na kumaliza kwa maneno haya ya kutia moyo: "Mjue kwamba kazi mnayo fanyia Bwana sio ya bure." Hivyo basi kuna sababu ya kuishi. Yeye atarudi. Tutainuka tena.

Ufunuo wa Yohana 11:7-13 inaongea kuhusu kufa na kufufuka kwa wale Mashahidi wawili, na pia mtetemeeko wa ardhi uliokumba Yerusalemi wakati huo. Huu mlio wa saba (mwisho) wa tarumbeta unaadhimisha mwanzo wa adhabu ya Mungu, au kufunua kwa ndoo ya saba.

 

 

24. Yerusalemi Mpya

 

Mwanya uliokuwa juu ya wateule ulizidi kupanuka na Rayford kujihisi akiukaribia kwa kasi sana. Huku mamilioni ya wateule kutoka kote ulimwenguni wakisonga kuelekea katikati ya kio, wale (kama Rayford na Chaim) walio wasili kwanza walichukuliwa kupitia kwa mwanya ule. Rayford alitazama chini na kuona mawingu chini yake. Lazima wako maili nyingi kuelekea juu, na bado wanaendelea.

Hata baada ya kupita mwanya ule, waliendelea kuelekea juu kwa kasi, wakiwacha nafasi kwa wingu lililokuwa na malaika na wateule wengine wakiwafata nyuma.

Ndani ya chombo kile, Rayford hakuhisi mvuto wa chini au juu. Ulikuwa ni kama ulimwengu mwingine, bila kuwepo uzani. Hatukuwepo na upungufu wa hewa safi, iwapo miili yao ilikuwa ikitumia hewa.

Kwa ghafla Rayford alijihisi mwenye hatia. Alikasirishwa na mji ule kiasi cha kumsahau Yesu, yule ambaye aliwezesha haya yote.

"Usiwache hilo likakusumbue!" mtu akasema au kitu. Ilikuwa kama kwamba sauti ilifanyikia kichwani mwake. Hata hivyo, Rayford alitazama kando na kuona malaika akitabasamu. "Utakuwa na wakati wa kutosha kukutana na Bwana ana kwa ana," alifikiri alisikia malaika akisema.hata ingawa hakuona mdomo wake ukiashiria.

"Waweza.?" Rayford alianza. Lakini jawabu lilimrudia hata kabla ya kumaliza swali.

"Hiyo ndiyo sababu niko hapa. Ni jukumu langu kuwaonyesha hapa, na kujibu maswali yenu."

Wale watu wawili (kwani malaika walionekana kama watu isipokuwa kwa hali yao ya unyenyekevu na uerevu pamoja na mavazi) walikuwa pia wakisonga kwa kasi kupita ule mji mkubwa waliokuwa wameingia tu. Umati ulikuwa ukipunguka, na ikaonekana kwamba kila mteule alikuwa na malaika wake wa kumuongoza.

Fikira za Rayford zilijaa mshangao jinsi vile alivyokuwa amefufuka, kuingia katika chombo kile, kushuhudia kurudi kwa Yesu, na jinsi taratibu za kisayansi zilivunjwa huku akionekana kama kijana.

"Ni takribani maili elfu moja na mia tano juu", malaika alisema huku akisoma akili ya mwanagenzi wake. Akili ya Rayford ilikuwa imejaa maelezo kuhusu alipokuwa na kilichokuwa kikiendelea kwa haraka.

"Mamilioni ya wateule wamefufuka kutoka kote duniani na kuletwa kwa kasi. Yesu yu pale ili wote wamuone kabla ya kuingia Yerusalemi mpya. Ndio Yerusalemi mpya. hilo ndilo jina la mji huu. Sote tumekuwa tukifanya bidii kuona wakati huu.

"Wakati kila mtu atakuwa ameingia ndani, kufikia jioni Israeli, tutakusanyika kushuhudia arusi. La hatutakuwa na giza hapa. Uwepo wa Bwana huangaza mji huu milele. Hakuna kulala, sherehe yaweza kuendelea kwa wiki kadhaa kulingana na saa za dunia, bila kuchoka.

"Umati? haitakuwa shida. Utamsikia vizuri tu jinsi unavyonisikia. Tutakuwepo na vio iwapo utahitaji kumuona, lakini sio mwili wake tunaoabudu, ni ukweli wake na nguvu. Tumeandaa vyakula vya kutosha na nyimbo nzuri pamoja na kucheza. Sherehe kuu, haujui jinsi sisi huku juu tulikuwa tukisubiri wakati huu"

"Hii ni raha tupu!" Rayford alishangaa, kwa furaha kwamba malaika wake alikuwa amemueleza machache kuhusu yale aliyokuwa akifikiri.

"Tunaelewa kutaka kwenu kutoa shukrani," Malaika alisema Sisi pia tunahitaji hilo Utafurahia nyimbo hizo! Itakuwa ni furaha kuu ya kutukuza katika historia. Kwa hakika itakuwa ya kupendeza na kuvutia!"

Rayford alijisikia mwenye hamu ya kumkumbatia malaika, na kisha malaika kwa furaha alimkumbatia. "Niite Bob" alisema. Na Rayford kushanga kwa jina hilo lisiloonekana kama lakimalaika.

"Wafikiri ni la kawaida sana?" Bob aliuliza. "Kwa hakika majina hayana maana hapa juu. Watu hawawezi kupotea, na watu hufahamu wanapoelezwa kivyao-- kama ninavyofanya--- lakini Bob litafaa iwapo utaona haja ya kutumia jina."

Ahsante Bob Rayford alijibu. Na fikira zake zikamgeukia Irene.

"Yuko hapa," Bob alimhakikishia. "Utamuona baadaye. Lakini utampenda kila mmoja hapa jinsi unavyompenda. Na Bwana. mbona, atakuwa kipenzi cha wote!"

Rayford aliona ukweli ndani mwa yote aliyosema Bob. Duniani alikuwa na mapenzi kwa Irene; alikuwa jukumu lake. Lakini hapa.kila mmoja aliishi kumfurahisha Mungu. Sherehe ya harusi kama walivyosema ilikuwa ni kuwaunganisha na Mungu. Raha aliyoona Rayford tangu kuinuka kutoka pale Hekalu la Mlima ilikuwa ni raha ambayo alikuwa hajapata kuona akiwa kule duniani, ikiwemo ngono. Hakumkosa hata Irene, au kuwa na hamu ya kumuona. Alijua kwamba wako pamoja. sio tu na kila mmoja, lakini na wateule wote. Walikuwa kitu kimoja katika kumuabudu Mungu. Walikuwa wameingia katika ndoa mpya--harusi na Mungu.

Fikira za Rayford zilichukua mkondo mwingine, na mara moja Bob akabadili sawa naye.

"Kule duniani?" Bob aliuliza. Wamehangaika, siwezi kukueleza hayo!" alisema kwa kicheko. "Ol Dangchao anawaambia tu hii ni nyota ya wageni wanaokuja kuharibu dunia. Kwa kiwango ni kweli. Lakini hawezi kudhubutu kumtaja Mungu. Kama angaliweza, basi wangaliona adhabu ya kutupiga vita na labda wangaliungama.

"Israeli imepitia kwenye maafa kwa wakati huu. Karibu 7,000 wamekufa kutokana na mtetemeko. Lakini Dangchao hajaguswa. Hafikiri juu ya yote ila yeye binafsi. Sasa hivi analia na kuomba majeshi kutoka pembe zote za dunia. Manuwari, ndege za kivita, makombora, na chochote kinachoweza kulipua kile kio"

"Wanaweza.?

"La. Hakuna nafasi. Haingesababisha lolote laiti wakidhubutu. Kio hiki sio kinga, Mungu ndiye. Tuliweka tu pale. Sawa na mawe ya dhahabu na mawe mengine yanayong'aa kila mahali hapa. Yanavutia, au sio?"

Majengo yale ya kupendeza katika Yerusalemi Mpya yalikuwa yameongeza raha aliyohisi Rayford. Kulikuwa na manukato yaliyo toa harufu nzuri, na aina ya mlio wa mziki wa kupendeza uliokuwa ukichezwa kichwani mwake. Maji masafi yalipita kwenye mji ule, maji hayo hayakuwa yamezuiliwa na ukingo wa mto, yalikuwa yamejishikilia tuu yenyewe, Rayford alinyosha mkono kuyagusa, kwa hakika yalikuwa baridi bila kitu kilichofunika kama alivyodhani.

Kulikuwepo sehemu zilizokuwa na mimea kama jangwa. lakini haikuwa jangwa. Ungalitembea juu chini ya vichaka, na maua ya kuendeza. Mimea ilionekana kukosa shina, hata ingawa tulikuwa na mimea ya kutambaa iliyokuwa na maua ya kupendeza.

Mawe ya dhahabu aliyosema Bob yalikuwa kando ya sehemu za kupitia. Mijengo aliyokuwa akiona haikuwa "nyumba" kama zile za ardhi. Hapakuwepo haja ya kuta au sakafu, kwani watu hawakuwa na lakuficha na aliweza kuwaona wenzao kutoka juu, kando chini na kokote pale. Sehemu ambazo zilipitisha mwangaza nusu ndizo zilizotumiwa kugawanya sehemu za mji ule, ili kinachoendelea sehemu moja kisije kuadhiri ule upande mwingine. Mawe mazuri na mimea ya kuvutia ndio iliyogawa sehemu hizo.

Iwapo kulikuwepo na lolote lililo wasumbua wateule katika Yerusalemi mpya, ulikuwa ni wakati au saa. Haungali zungumza kuhusu "usiku" au "kesho", au siku ngapi kabla ya kitu fulani kutendeka, kwa sababu hatukuwepo na usiku, aidha watu hawakulala.

Lakini wangalichukua muda kujiburudisha katika bustani za maua, na kisha kuingiwa tu na uzuri wa mazingira yale.

Kulingana na siku za dunia, sherehe ya arusi ilichukua majuma kadhaa. Rayford alikutana na Irene, Elaine, Chloe, . hasa wale Jesans wote na mahakimu kumi na mbili. Walijadili kuhusu yaliyotukia walipokuwa mbali mbali, msisimuko wao ulikuwa juu ya kufufuka, na kilichofanyika, na yale ambayo walikuwa wamejifunza katika Yerusalemi Mpya.

"Tunaenda kuutawala ulimwengu baada ya `vita'kukamilika," Raymie alisema. Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mbili, na ataendelea kuzeeka katika Yerusalemi Mpya hadi atakapofikia thelathini. "Jukumu hili" alisema. "Litatolewa baada ya sherehe."

Rayford aliwatayarisha kwamba hawatakuwa na majukumu mengi au magumu kama waliyokuwa nayo kule duniani miaka saba ile ya mwisho. "Imeonekana kwamba sisi huonekana wachovu tunapoongoza, na Mungu hutambua vipawa vya wale wenye imani miongoni mwa wafuasi wake. Twataraji kuona baadhi ya wenzetu wachanga wakipewa mamlaka," alisema.

Neville alikuwa kule pia, na alikuwa na ujumbe wa kufurahisha aliopokea kutoka kwa malaika wake.

"Mnafahamu jinsi tulivyoweza kutuma barua-pepe bila kuunganishwa au kuwepo kwa tuvuti?" alisema. Hakika ilikuwa ikitayarishwa kupitia chumba fulani hapa juu. Mahali hapa paweza kubadilika. Ilikuwa kule nje kwa wakati ule ili kuweza kutoa kiunganishi kwenye mtandao na kutayarisha barua zetu. Hiyo ndiyo sababu hatkupata kulipa kodi baada ya kuharibiwa kwa Web Wonders.

"Jambo lingine! walikuwa ni watu hawa ndio walioyeyusha Web Wonders na wala sio Dangchao, ili orodha na anwani zetu zisiweze kutambuliwa na dangchao na wenzake.

"Nimekuwa nikijifunza jinsi mambo yanavyofanyika huku juu. Sio uganga au kitu kama hicho. Kuna mengi na fizikia ambayo watu wa dunia hawajavumbua. Vitu kama kuepuka mvuto wa ardhi, na jinsi ya kusoma akili. Hata miili yetu mpya inafanya tu kazi kama ile ya awali ilivyofanya. Aina mpya. Haihitaji kulala, haitazeeka, na ina kinga dhidi ya maradhi. Tutaendelea kula na kunywa, lakini nguvu zaidi inatoka kwa Mungu. Inatufikia kupitia mwangaza unaofikia sehemu hii. Nje ya eneo hili tungalizeeka, kama mtu mwingine yeyote.

"Kuna mengi tu ya kujifunza," alieleza

"Sio ajabu?"

Kila mtakatifu alipata furaha kutoka kwa jambo fulani. Maria alifurahi kuona mabadiliko baina ya wenzake, kwamba walikuwa wachanga na wenye afya. Alifurahia kumsikiza Neville aliyekuwa akipata maelezo ya ajabu ya Fizikia. Kuwatazama tu Maria Teresa na Sheila Armitage waliokuwa na umri wa miaka thelathini, kulimvutia sana. Na sasa nguvu maradufu!. Alitaka kuongea na kila mmoja kutaka kufahamu aliyotendewa na Mungu.

Fran Luis, Mike na Martin walijikuta wakicheza kufuatia ujuzi wao mpya wa kuruka. Walikuwa kama watoto,, hata ingawa walionywa dhidi ya kuruka ovyo.

Matayo Baker na Yohana Doorman walichukua muda mwingi kwenye makavazi wakitazama kanda zilizo rekodiwa kuhusu maisha yao na ya wengine. Waliweza kuelewa kiroho kilichotendeka wakati fulani katika maisha yao. Wangalifahamu wakati walipoomba na kubwenyeza mahali ili kuona kilichowapelekea kuomba. Walifurahi sana jinsi Mungu na malaika waliweza kuunda orodha ya kila mmoja na matendo yake.

Reinhard alifurahia tu kuzunguka katika bustani akitazama maua na mimea ya kupendeza, na viumbe kama wanyama waliokuwa hapo.

Kulikuwepo angalau kitu cha kumffurahisha kila mmoja na kumfanya kuwa na la kufanya na kufurahia hata zaidi ya miaka elfu moja, kilichokuwa kipindi watakacho tawala ulimwengu. Yatakayotukia baada ya miaka hiyo elfu moja lilikuwa jambo la kujali wakati utakapo karibia. Lakini kwa sasa kila mmoja kwa kuongozwa na malaika na Yesu, atapewa jukumu wakati wa kutawala ulimwengu kwa miaka hiyo elfu moja.

Huku wakisherehekea, Mungu alikuwa akiwaadhibu waliokuwa chini ya ardhi. Yale maafa na mahangaiko waliyopitia wateule hayakuwa lolote ukilinganisha na yale yaliyokuwa yakishuhudiwa kule chini. Majeshi ya Dunia yalikuwa yakijiandaa kwa vita kati yao na Yerusalemi Mpya. Dangchao alipanga kulenga makombora kupitia mwanya walioingilia wateule. Lakini wateule kwa pamoja na malaika walikuwa tayari kuzuia shambulizi.shambulizi linalojulikana sana kama Vita vya Magedoni.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Ufunuo wa Yohana 21, unaeleza zaidi kuhusu Yerusalemi mpya inapofikia ulimwengu (yaani baada ya vita vya Magedoni).

Hatujaeleza kuhusu yale majitu yanayoambatana na mitungi ile `saba' ya adhabu. Waweza kujisomea katika Ufunuo wa Yohana 16. Hata hivyo kutokana na yote Mungu anayodhihirisha, ulimwengu hauko tayari kuungama. Licha ya hayo ulimwengu unazidi kuwa na ukatili na kumuasi Mungu. Wanaungana na kumpiga vita Mwenyezi Mungu. (tazama sura inayofuatia.)

Bibilia inatuarifu kwamba hatutakuwa na ndoa mbinguni. (Matayo 22:30, Mariko 12:25 na Luka 20:34) Hii ni ngumu sana kwa baadhi ya watu kuelewa, kwani ndoa ndiyo huonekana kuwa karibu sawa na mbingu (hata hivyo wengine husema ni karibu sana na jehanamu aidha!) Lakini kama tusivyoelewa jinsi Mungu alivyotenda Mengi (kwa mfano kuumba), hatuwezi kuelewa raha na uzuri aliopangia waja wake wanaomuamini.

Bibilia inatuarifu kwamba Mungu atatoa mwangaza katika Yerusalemi Mpya. Kuonekana kwa Yesu akiwahubiria mamilioni ya watu hakuwezi kufanyiwa taswira kwa urahisi. Lakini kwa kuungana na Mwangaza wa Bwana (Uwepo wa roho mtakatifu) na malaika, Yesu ataweza kutimiza haja za waaminifu pasipo matatizo yoyote.

 

 

25. Magedoni

 

Vita vya Magedoni vilikuwa ni mwanzo wa hadithi nyingine. Wanajeshi wa kimataifa duniani, ilijulikana kwamba walikuwa wamejikusanya zaidi ya mwaka mmoja uliopita kabla ya kuanzisha vita. Dangchao alihisi kwamba alikuwa akipoteza, na kwa kisiri alikuwa ameamuru mpangilio fulani kuanzishwa kabla ya Rayford na Chaim kutoka London na Sydney kuenda Yerusalemi.

Kulikuwa na ufunzi mwingine kuhusu Dangchao uliojitokeza na kuonekana kwa usaidizi wa roho. kama kushiriki kwake, kutoka mwanzoni, katika kuharibu kwa Amerika kulikotekelezwa na Urusi na maovu mengine mengi. Kwa wale wasio na imani au wasio mtii Mungu, walimuona kama atakaye suluhisha matatizo yao yote. Wale waliokuwa na imani kama ya watoto na ufasaha, walikuwa wameepuka uongo huo.

Kuonekana kwa Yerusalemi Mpya juu ya anga ya Mashariki ya kati, kulitoa fursa kwa Dangchao kulenga silaha zilizo bora (au duni kulingana na jinsi unavyofikiri) kutoka kwa ulimwengu. Alishawishi serikali za dunia kwamba uvamizi ule ulikuwa umetokea katika sayari ya kigeni. Kuwepo maisha ya binadamu kutategemea na kuwafagilia au kuwazuia hawa wageni-- waliolaumiwa kutokana kuanguka kwa nyota hadi mawimbi, na hata wale nzige alioachilia Dangchao mwenyewe.

Ule mwanya ulio kuwa karibu maili moja katika kile kio walipoingilia wateule, ulikuwa haujafungwa tangu Yesu na majemedari malaika kuufungua. Ilionekana kwa Dangchao kama mahali bora pa kuanzisha shambulizi.

Dangchao kama amri-jeshi-mkuu wa majeshi ya dunia, alikusanya zana zote za kivita zilizokuwa bora duniani kuanzia kwa makombora ya ndege hadi silaha za maangamizi makubwa na nuklia. Iwapo wachache kati ya marubani wake wangaliingia kule mbinguni, wangalipeleka uchafu wa jehanamu mbinguni. Na iwapo hilo halingalifaulu, alikuwa ameagiza kila aina ya mizinga ya hewa na ardhi hadi Israeli, na kujenga sehemu za kuanzisha mashambulizi kote nchini, ili mashambulizi yaweze kulenga dunia mpya na watakatifu punde atakapo toa ilani.

Karibu na ukamilisho wa sherehe ile ya harusi katika Yerusalemi Mpya, wateule walipata mawaidha jinsi ya kujikinga na kutetea mji wao. Walipaswa kukabili maadui bila silaha, ila uwepo wa Mungu.na ukweli. Kila mteule alipaswa kuchukua muda wa saa moja akioga katika Mwangaza wa Yerusalemi Mpya, iliyokuwa kama kuota jua katika dunia. lakini sio moto. Wangalipata nguvu za kutosha kutenda vyema hata wakiwa nje ya Yerusalemi Mpya. Walipewa tahadhari na mawaidha ya kumfuata malaika wao bila kuuliza swali kuhusu mwenendo.

Wakati ulipowadia, wateule na malaika walitumwa kwenda kukutana na wale waasi. Yesu alikuwa pale chini karibu na mwanya. Mwangaza wake uling'aa kiasi cha kupeleka miali mbali sana pande zote. Alikuwa mlengwa wa kila rubani kutoka kwa jeshi la maadui.na kejeli la Dangchao na umati wake.

Wale watakatifu na malaika walikuwa wakiruka kwa kasi muno. Wengine walienda kama umeme kukaripia ndege zilizokuwa zimewachiliwa. Nakuzunguka mkondo wa maelekezi ya ndegee za kivita. Walikuwa kila mahali (juu, chini, na mbele ya) kuelekea ndege za kivita huku zikielekea kwenye mwanya

"Hamna haja kufanya haya," mmoja wa watakatifu alisema (au maneno karibu na hayo) kwa wale marubani.

"Hatujakuja hapa kuwadhuru," wakaendelea.

"Mjiokoe ninyi pamoja na ulimwengu wenu kwa kurudi mtokako sasa hivi." "Mungu anawapenda." "Hataki kuwaona mkifa." Ujumbe huu ulingiia katika kila chumba cha rubani, na kwa akili za wote waliokuwemo katika zile ndege kubwa. Baadhi ya wateule na malaika walionekana nje ya zile ndege.

Lakini kila waliposema hivyo, wale viumbe wakatili waliomuasi Mungu walidhani ni stihizai tu ya kuwatisha na kutatanisha akili yo kutoka kwa viumbe hawa wa mbinguni. Uoga uliwafanya kuwa viziwi wa kusikia ukweli. Uoga huo ukabadili na kuwa hasira. Walijaribu kuelekeza ndege na kufyatua mizinga yao ili kuwalenga wale wateule na malaika waliozingira vyombo vyao. Zile ndege zilitawanyika na kupoteza mwelekeo. Walipodhani wanawalenga wale wateule na malaika waliona mizinga yao ikiwapiga wenzao. Baadhi ya ndege kwa ajabu ziligeuka kuanguka na kuangamiza yale majeshi yaliyokuwa pale chini, bila kuwatingisha au kushutua Yerusalemi Mpya. Ilikuwa ni kupotea kwa mwelekeo na kurudi chini na vifaa vyote walivyokuwa navyo.

Walikuwa wakijitungua wenyewe na kuteketea kwa kumuasi Mungu wenyewe kwa wenyewe. Hakuna yeyote aliyekiri wito huo wa mwisho wa kuungama uliotolewa na wale wateule.

Pale chini Dangchao alitoa amri kwa mizinga ya ardhi kuanza kulipuliwa. Lakini bawa kubwa la jeshi la mbinguni lilikuwa limefikia mahali pale. Wateule na malaika walionekana wakipita mahali pale, huku wakizunguka na kupita katika vile vyumba ambavyo vilikuwa na mikondo ya kubovya kuanzisha shambulizi. Kwa kutumia ujuzi wa tarakilishi waliokuwa nao, baadhi ya watakatifu walionekana kwenye vio vya tarakilishi wakiongea na wale waongozaji wa shambulizi.

(Wakati ule wa mpasuko, utaalamu huu ulitumiwa kumuonyesha Yesu juu ya Yerusalemi kupitia kwa kote duniani.)

Ujumbe wa upendo, amani na wito wa wokovu ulimfikia kila aliyeshiriki kwenye vita vile; na halikadhalika ujumbe huu kupuuzwa. Badala yake jeshi la dunia lilichanganyikiwa. Watu wote walitoka, mizinga ilifyatuliwa lakini haikufanya chochote, kwani mwendo wa watakatifu na malaika ulikuwa wa kasi sana kushinda mbio ya mizinga. Kila wafuasi wa Dangchao walijaribu kushambulia, mizinga hiyo iliwarudia na kuuana wenyewe kwa wenyewe.

Ilikuwa katika hali hiyo ya masikitiko ndiposa Dangchao akaamuru kufyatuliwa kwa mizinga yote ya ardhi. Kitu cha kushangaza sana kilitokea kwani vitu hivyo vililipuka kabla ya kujaribu kulenga, na kuharibu kwa njia ya mizinga ya "kirafiki" iwapo kulikuwepo na mizinga kama hiyo.

Hakuna kombora lolote lililotolewa, kwa sababu waliopaswa kulenga walikuwa tayari wamekufa au kujeruhiwa kabla ya kudhubutu. Wale watakatifu walifaulu kwa kulemaza vyombo hivyo, na kufanya baadhi yao kukosa mwelekeo. Ule ukuta wao wa kioo haukupata kuguswa na ukawa kama ngao, na kusababisha maafa zaidi pale chini kuliko walivyotaraji kufanya Yerusalemi mpya.

Watakatifu walibaki karibu na malaika wao, ambao walikuwa na uwezo wa kuona mbele na kuwaelekeza hadi mahali pa kuhudumu, au kurudi Yerusalemi Mpya. Waliweza kueepuka maeneo yaliyokuwa yakishambuliwa na jeshi la Dangchao.

Baada ya vita hivyo, Dangchao, pius na wafuasi wake walishikwa na kuwekwa gerezani kwa miaka elfu moja, na kuwekwa ndani ya shimo lisilofikia kikomo liliowachwa baada ya mtetemeko wa ardhi kule Jerusalami. Kwa miaka hiyo elfu moja watajulishwa kuhusu maendeleo yaliyokuwa yakitokea katika dunia ambayo waliwahi kutawala.

Mwanzo mpya ulikuwa umezinduliwa. Ubaya wote ulikuwa umezimwa kwa miaka elfu moja, na mwangaza na uzuri wa Mungu kuonyesha watu jinsi mambo yalitarajiwa kufanywa, iwapo tungalitumia hiari yetu kumtii na kumtumikia Mungu, na kuwapenda wenzetu.

Kinyume na maelezo ya Rayford kwamba pande zote katika vita hupata majeruhi, vita vya Magedoni vilikuwa vya pande moja na ile nyingine haikupata kuadhirika. Majeshi ya Mbinguni hayakupata jereha lolote. Sio kwamba walikuwa na kinga dhidi ya shambulizi, bali walifuata na kutii maagizo ya Mungu. Hili lilikuwa funzo ambalo walimwengu ulimwenguni walikosa kutilia mkazo. Kila mara Mungu alipotoa mawaidha kwa viumbe hawa, walichukua tu jukumu la kusahau na kupuuza, na kufanya mambo kwa njia yao wenyewe. Sasa kwa miaka 1000 ulimwengu utashuhudia, faida ya watu walionyenyekea na kutii Mungu.

Wale malaika walionekana kuwa wenye huruma na kutaka kusaidia kila mara kuliko wale watakatifu, hivyo basi, kila mmoja alitakikana kubaki na malaika wake na kisha kujipata wakitenda yafaayo, mahali panapofaa na katika wakati ufaao. hivyo ndivyo walivyofanya, wakati wa vita na baada ya vita.

Baada tu ya vita, wateule walichukua miezi kadhaa kusafisha mahali palipokuwa pamekumbwa na vita hivyo, na kutayarisha sehemu itakapokaa Yerusalemi Mpya. Hatukuwa na manusura katika Israeli, lakini manusura katika nchi zile zingine walipaswa kuondolewa. Wateule walihakikisha kwamba kuondolewa kwa watu na kusafisha eneo lile kuliendelea ipasavyo. Walipaswa pia kujifunza ujuzi wa kuchukua ile miali kutoka Yerusalemi Mpya.

Wakati matayarisho hayo yalipo kamilika, sakafu nzima ya mji mkubwa ilijigawa katika sehemu nne, na kuchukua alama ya almasi. Vigae hivyo vilibadilika na kuwa kuta nzito za maili 1500 na urefu wa futi 200. Na kujenga ukuta wa mraba kuzunguka Yerusalemi Mpya. Moja kati ya kuta hizo nne ilikuwa na lango kubwa lililokuwa wazi kila wakati.

Kwa ukuta uliojikunja, mji ule uliweza kutua maili tano zilizosalia kukaribia dunia, na kuchukua muundo wa ardhi.

Kwa miaka ijayo elfu moja, wateule watatawala dunia-- yaani wale walioepuka adhabu ya Mungu, na vizazi vyao--kutoka Yerusalemi Mpya. Mabalozi watatoka humo na kuenda pembe zote za dunia huku wakileta ujumbe kuhusu yaliyokuwa yakiendelea duniani, wale waliokuwa nje ya mji waliweza kujaribu kujifunza kutoka kwa wateule waliokuwa wamepata haki ya kutawala.

Kazi ya wateule ilikuwa kuufundisha ulimwengu jinsi ya kuishi kwa amani, jinsi ya kuwahudumia wenzao kwa upendo, jinsi ya kugawana milki ya dunia kwa usawa, jinsi ya kuishi bila pesa,, na zaidi jinsi ya kuishi na kumtii Mwenyezi Mungu-- kuomba kusikiza na kufuata maagizo yake katika maisha yao.

Watakatifu waliongozwa katika kutekeleza majukumu hayo na malaika; na yale waliyojifunza (na waliyoendelea kujifunza) kutoka kwa mafundisho ya Yesu--Mwanawe Mungu, na Ufunuo wa Yohana wa Mungu kwa mwanadamu. Hakuwa tu mkombozi wao, lakini pia Bwana na Mkuu.

Na hivyo ndivyo yapaswa kuwa.

 

 

Zion Ben-Jonah Aandika

 

Siri ya ujenzi wa zana za kivita duniani na wasio mtii Yesu, kwa matayarisho ya vita vya Magedoni, inaelezwa katika kitabu cha Ufunuo wa Yohana kama mlio wa sita wa tarumbeta. Inaeleza kwamba walijiandaa kwa miezi kumi na tatu na siku moja. (Ufunuo wa Yohana 9:13-19)

Mlio wa saba wa parapanda ya mwisho unaadhimisha mwisho wa uvumilivu wa Mungu, na kuanza kwa Adhabu yake juu ya wale wanaomuasi na kukataa kumfuata: (Ufunuo wa Yohana 9:20-10:7, na 11:15-19). Kipindi hicho kifupi cha adhabu kinaenda sambamba na sherehe za Harusi ya Bwana mbinguni (Ufunuo wa Yohana 19:7-9). Sababu vyombo sita vya kwanza imeelezwa katika Ufunuo wa Yohana (16:1-6).

Vita vya Magedoni ni katika kile chombo cha saba (Ufunuo wa Yohana 16:16-21) Yesu ameonekana akiwaelekeza majeshi yake kwenye vita Vikuu. (Ufunuo wa Yohana 19:11-14). Lakini muhimu ni kwamba silaha katika vita hivi inatoka katika mdomo wa Yesu. (Ufunuo wa Yohana 19:15)

Yesu anashinda vita, na kumkamata shetani pamoja na manabii wake wa uongo kwa miaka elfu moja. (Ufunuo wa Yohana 19:16-20:2)

Hatukuchukua jukumu la kuchambua kila aina ya maelezo kuhusu Ufunuo wa Yohana katika kitabu hiki. Lakini tunatumai utatumia kitabu hiki kama muongozo, na waweza kusoma Ufunuo wa Yohana kivyako, na itadhihirisha na kutoa maana kuliko ilivyokuwa hapo awali.

Chukua tahadhari; kwani atarudi! na muda ni mfupi.

 

Tafsiri na,

Patrick Bunyali Kamoyani,

Maragoli Kenya.

Email: pbkamoyani@excite.com or

pbkamoyani@lycos.co.uk

Impressum

Tag der Veröffentlichung: 09.01.2016

Alle Rechte vorbehalten

Nächste Seite
Seite 1 /